Wasauzi wampagawisha Okwi,aanza mbwembwe

Simba huenda ikalazimika kufanya kazi ya ziada kumbakisha mshambuliaji wake hatari Emmanuel Okwi ambaye timu nyingi zimeonyesha nia ya kutaka kumsajili

Mkataba wa Okwi unatarajiwa kumalizika ndani ya siku 60 huku mchezaji huyo raia wa Uganda akionyesha dalili zote za kutaka kuondoka Msimbazi

Okwi anahusishwa na vilabu kadhaa vinavyoshiriki ligi kuu ya Afrika Kusini, Orlando Pirates na Kaizer Chiefs

Kocha Patrick Aussems alimuondoa Okwi katika kikosi kilichokwenda mkoani Morogoro baada ya mchezaji huyo kuchelewa kuripoti kambini

Meneja wa Simba Patrick Rweyemamu amesema hana taarifa kuhusu mshambuliaji huyo ambaye alikuja nchini na kikosi cha timu ya Taifa ya Uganda Cranes na alicheza mchezo dhidi ya Stars

“Mimi sijui chochote kuhusiana na Okwi labda waulizwe viongozi wangu wa juu, hayupo kwenye msafara wetu huu unaoelekea Morogoro, hivyo waulizwe viongozi wa juu suala lake,”Rweyemamu alinukuliwa na Championi jana

Hata hivyo Okwi amekuwa na kawaida ya kuchelewa kuripoti kambini kila anapotoka kutimiza majukumu ya timu ya Taifa

Hali ni tofauti kwa Juuko Murshid ambaye tangu aliporejeshwa kikosini, amekuwa akiwajibika ipasavyo

Juuko alikuwa miongoni mwa wachezaji waliowahi kuripoti kambini baada ya kumalizika michezo ya AFCON

Taarifa zilizopatikana mapema leo zimebainisha Okwi amerejea na ameshatua mkoani Morogoro kuungana na wenzake