Yanga kupata viongozi wapya kesho

Wagombea wa nafasi mbalimbali za uongozi katika klabu ya Yanga leo wanahitimisha zoezi la kampeni kuelekea uchaguzi Mkuu wa klabu hiyo utakaofanyika kesho Jumapili ukumbi wa Bwalo la Polisi, Osterbay jijini Dar es salaam

Wagombea walianza kunadi sera zao kwa Wanachama Jumanne iliyopita

Nafasi ya Mwenyekiti wa Yanga inawaniwa na wagombea watatu Barak Igangula, Dk Jonas Tiboroha na Dk Mshindo Msolla wakati nafasi ya Makamu Mwenyekiti inawaniwa na wagombea wanne ambao ni Fredrick Mwakalebela, Janeth Mbene, Titus Osoro na Yono Kevela

Aidha wagombea 21 wanawania nafasi nane za wajumbe wa Kamati ya Utendaji

Wanachama wa Yanga wametakiwa kutofanya makosa kwenye uchaguzi wa kesho kwa kuwachagua viongozi ambao wataweza kuipeleka Yanga mbele

Suala la Mabadiliko limekuwa kilio cha Wanayanga. Wagombea wote wameahidi kufanya mabadiliko, ni jukumu la Wanachama kujiridhisha na uwezo wao na ahadi walizotoa katika kutatua changamoto zinazoikabili Yanga

Wanachama wameaswa kutochagua viongozi kwa mazoea badala yake wachague viongozi ambao wana upeo mkubwa

Ni vyema kiongozi atakayechaguliwa awe na uwezo wa kutengeneza mikakati ya kuipeleka Yanga kule ambako kila mdau anahitaji kuona klabu ikielekea

Huu sio wakati wa kujaribu viongozi, Wanachama wawaweke madarakani ‘watu wa kazi’

Wanachama wasichague viongozi kwa papara, mihemko na makundi, kila mmoja afanye uamuzi kwa maslahi ya klabu kwa kuchagua viongozi wenye tija

Yanga ikipata viongozi wazuri, utakuwa mwanzo wa kutengeneza Yanga imara ambayo itagombewa na wawekezaji na kuifanya timu hiyo kongwe zaidi Tanzania kuondokana na dimbwi la ‘umasikini’