SIMBA : Yaapa kuikomalia JS Saoura LEO

Mabingwa wa soka Tanzania Bara Simba wako nchini Algeria ambapo leo Jumamosi March 09 2019 watashuka dimba la Agosti 20 kuikabili JS Saoura katika mchezo wa ligi ya mabingwa utakaopigwa saa nne usiku

Simba inaweza kuandika historia nyingine leo kwa kutinga robo fainali ya michuano hiyo mikubwa kabisa barani Afrika kwa ngazi ya vilabu

Mashabiki wa Simba na Watanzania wote kwa ujumla wametakiwa kuiombea timu dua njema ili iweze kupeperusha vyema bendera ya nchi huko ugenini

Aidha mafanikio ya Simba kwenye michuano hii ni mafanikio ya Tanzania kwani iwapo itafanikiwa kusonga mbele, itaiongezea Tanzania alama na pengine msimu ujao nchi inaweza kuongezewa idadi ya wawakilishi kwenye michuano hiyo

Kwa sasa Tanzania ina nafasi mbili tu kwenye michuano ya CAF wakati baadhi ya nchi zina nafasi hadi nne kutokana na vilabu vyao kufanya vizuri

Kocha Mkuu wa Simba Patrick Aussems amesema vijana wake wana ari ya kupata matokeo mazuri kwenye mchezo huo

“Hatukuja hapa kwa malengo ya kutafuta sare, tunataka kushinda mchezo huu,” amesema Aussems

Ushindi unaweza kuihakikishia Simba kutinga robo fainali kama Vital Club itashindwa kupata ushindi dhidi ya Al Ahly katika mchezo utakaopigwa mapema saa moja jioni

Lakini hata alama moja itaifaa Simba kuelekea mchezo wake wa mwisho dhidi ya Vita Club utakaopigwa uwanja wa Taifa Jumamosi ijayo March 16 2019