Yanga yakanusha Zahera, Ajib kuondolewa watia saini akaunti CRDB

Yanga yakanusha Zahera, Ajib kuondolewa watia saini akaunti CRDB

Uongozi wa klabu ya Yanga umewataka wapenzi, wanachama na mashabiki wa timu hiyo kupuuza taarifa zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii kuwa Kamati ya kuhamasisha uchangiaji iliyochini ya Mh Athony Mavunde imependekeza kuondolewa kwa Kocha Mwinyi Zahera na nahodha Ibrahim Ajib katika miongoni mwa watia saini wa akaunti ya kukusanya michango iliyofunguliwa benki ya CRBD

Msemaji wa klabu ya Yanga Dismas Ten ambaye ni mmoja wa wajumbe wa Kamati hiyo amesema hakuna ukweli wowote katika taarifa hiyo na amesisitiza wanaoisambaza ni wenye malengo ya kutaka kuikwamisha Yanga katika mpango wa kujijenga kwa ajili ya msimu ujao

“Hakuna sehemu hata moja kamati imekaa na kuzungumza haya. Huu ni uzushi upuuzwe na apuuzwe aliyeuandika,” amesema Ten

“Uongozi kupitia kamati hii ya Mh Mavunde ipo kwenye mikakati mizuri kuhakikisha klabu inavuka kwenye kipindi hiki kifupi wakati ikielekea kwenye mkutano mkuu wa uchaguzi na mabadiliko mengine”

“Tukumbuke fedha hizi zinakusanywa maaalumu kwa ajili ya usajili na mambo mengine yenye manufaa kwa klabu”

Jana Kamati ya Uhamasishaji ilikutana kwa mara ya kwanza ambapo mpango wa kuchangisha kiasi cha Bil 1.5 uliandaliwa mkakati wa utekelezaji katika kila mkoa