Waziri Mkuu mgeni rasmi mchezo wa Stars vs Uganda

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh Kassim Majaliwa keshokutwa Jumapili, March 24 2019 atawaongoza Watanzania kuiunga mkono timu ya Taifa ya Tanzania katika mchezo wa kusaka tiketi ya kutinga fainali za AFCON 2019 akiwa mgeni rasmi katika mcheoz huo dhidi ya Uganda

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam Mh Paul Makonda ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati Maalum ya Uhamasishaji, amesema Waziri Mkuu amekubali kuwa mgeni rasmi wa mchezo huo na hivyo kuwataka wakazi wa jiji la Dar es salaam na maeneo ya jirani kujitokeza kwa wingi kwenye uwanja wa Taifa kuungana na Waziri Mkuu katika kuipa sapoti Stars inayohitaji matokeo ya ushindi dhidi ya Uganda

Kikosi cha Stars kimeendelea kujifua katika dimba la Taifa kujiandaa na mchezo huo utakaopigwa saa kumi na mbili jioni

Stars imedhamiria kuvunja rekodi ya miaka 39 ya kukosa nafasi ya kushiriki fainali za michuano ya AFCON. Inaweza kufikia malengo hayo kama itaifunga Uganda huku ikiomba Lesotho ambayo itakuwa ugenini ikichuana na Cape Verde itashindwa kupata ushindi

Uganda tayari imefuzu ikiongoza kundi L ikiwa na alama 13, Lesotho inafuatia nafasi ya pili ikiwa na alama tano sawa na Stars lakini Lesotho imeipiku Stars kutokana na faida ya kupata alama nne katika michezo miwili ambayo timu hizo zilikutana

Cape Verde inashika mkia ikiwa na alama nne lakini pia inaweza kufuzu kama Stars itashindwa kupata ushindi dhidi ya Uganda huku yenyewe ikiichapa Lesotho