Uganda kumpaisha au kumponza Amunike

Kikosi cha Stars leo kitakuwa katika dimba la Taifa kuikabili Uganda Cranes katika mchezo wa kusaka tiketi ya kutinga fainali za AFCON 2019

Mchezo huo ambao ushindi ni lazima kwa Stars, utapigwa saa 12 jioni

Kocha Mkuu wa Stars Emmanuel Amunike amesema wamefanya maandalizi ya kutosha na anaamini vijana wake watafuata maelekezo na hatimaye kuibuka na ushindi

Ni mchezo ambao umeshikilia hatma ya Amunike kuendelea kuinoa Stars au kurejea kwao Nigeria kama atashindwa kuiongoza Stars kupata matokeo leo

Katika michezo iliyopita Amunike alikumbana na ukosoaji mkubwa kutoka kwa wadau wa soka nchini kutokana kutofurahishwa na uteuzi wa wachezaji, mbinu pamoja na upangaji wa kikosi chake

Stars ilikuwa na nafasi ya kufuzu mapema kama ingeweza kushinda mchezo uliopita dhidi ya Lesotho. Hata hivyo Amunike alipanga kikosi cha kujihami zaidi katika mchezo huo na kupelekea Stars kuchapwa bao 1-0 ugenini

Wengi wanasubiri kwa hamu kikosi atakachopanga leo dhidi ya Uganda ambapo Stars haihitaji matokeo mengine tofauti na ushindi

Lakini ni dhahiri hatma yake itakuwa mikononi mwake mwenyewe, kwani kama Stars haitashinda nae safari ya kurejea Nigeria itakuwa imewadia