Nasumbuliwa na nyonga, hayo mengine tuyapuuze – Ajib

Nahodha wa Yanga Ibrahim Ajib amesema kukosekana kwake kikosini kunatokana na maumivu ya nyonga ambayo yamekuwa yakimsumbua siku za hivi karibuni

Ajib hakujumuishwa kwenye kikosi cha Yanga ambacho kiko Mtwara kesho kikitarajiwa kucheza na Ndanda Fc. Pia alikosa mchezo wa robo fainali kombe la FA dhidi ya Alliance Fc

Aidha kuhusu taarifa zinazotawala katika vyombo vya habari kuwa yuko mbioni kurejea Simba, Ajib amesema ukweli au uongo wa taarifa hizo utafahamika msimu ukimalizika

“Mimi nina mkataba na klabu ya Yanga, nitaendelea kuitumikia timu yangu. Hizo taarifa za mimi kusajiliwa na Simba ukweli au uongo wake utafahamika mwishoni mwa msimu”

“Mimi ni mchezaji wa Yanga ni vyema nikaulizwa mambo yanayoihusu Yanga, hayo mengine tuwaachie wanaotumia kalamu zao kujinufaisha kwa kuuza magazeti lakini ifahamike mimi ni mchezaji wa Yanga,” Ajib amenukuliwa na Mwanaspoti

Kwa siku za karibuni baadhi ya magazeti yameripoti kuwa Ajib tayari amemalizana na mabosi wa Simba ambao wamemtengea mkataba wa miaka miwili

Hata hivyo hivi karibuni kaka yake Athumani Ajib ambaye ndiye wakala wake, alikanusha taarifa hizo huku akibainisha kuwa wamefanya mazungumzo ya mkataba mpya na Yanga lakini wamekubaliana ni vyema wakasubiri mpaka mwishoni mwa msimu ndio aweze kusaini mkataba mpya

Ni kawaida kwa wachezaji wa soka Tanzania kusubiri mikataba yao imalizike kabisa kabla ya kusaini mikataba mipya.

Utaratibu huo wamekuwa wakiutumia ili kujiongezea thamani hasa inapotokea timu zaidi ya moja zimewasilisha ofa ya kutaka kuwasajili