Kagera Sugar vs Simba, mchezo wa kisasi leo

Simba mabingwa watetezi ligi kuu ya Tanzania Bara, leo Jumamosi saa kumi kamili jioni watashuka kwenye uwanja wa Kaitaba mkoani Kagera kuikabili Kagera Sugar katika mchezo muhimu kwa kila timu

Wakati Simba ikihitaji alama tatu kuendelea kusogea kileleni katika mpango wake wa kutetea ubingwa, Kagera Sugar iko katika hatari ya kuteremka daraja

Lakini pia, ukiachana na mazingira hayo, kwa misimu miwili iliyopita, Kagera Sugar ilihusika katika kuvuruga mipango ya Simba

Msimu wa 2016/17 Kagera Sugar iliisababishia Simba isitwae ubingwa baada ya kunyan’ganywa alama tatu ambazo walikuwa wamepewa awali na Bodi ya Ligi kufuatia Kagera Sugar kumchezesha mchezaji aliyekuwa na kadi tatu za njano katika mchezo ambao Kagera Sugar ilishinda 2-1

Tukio hilo lilisababisha uongozi wa Simba kupeleka malalamiko FIFA, malalamiko ambayo yalitupiliwa mbali

Aidha mwaka jana wakati Simba ikiwa tayari imetangaza ubingwa, Kagera Sugar ikatibua tena siku muhimu kwa mabingwa hao ambayo walikuwa wakikabidhiwa kombe na Rais Dk John Magufuli kwa kuwachapa bao 1-0 kwenye uwanja wa Taifa

Kagera Sugar ndiyo timu pekee iliyopata ushindi dhidi ya Simba msimu uliopita

Msimu huu Simba imejipambanua kwa kuwa na kikosi bora zaidi ikiwa imeshinda michezo yote 11 iliyopita kwenye ligi na kuweka rekodi mpya

Ushindi katika mchezo wa leo utakuwa wa 12

Kocha Patrick Aussems amesema vijana wake wako tayari kuelekea mchezo huo na wamedhamiria kuondoka na alama zote tatu kama walivyofanya katika michezo 11 iliyopita