Simba yapania kufuta makosa CCM Kirumba leo

Mabingwa watetezi ligi kuu ya Tanzania Bara Simba leo wanashuka kwenye uwanja wa CCM Kirumba kuikabili Alliance Fc katika mchezo unaotarajiwa kupigwa saa kumi kamili jioni

Kikosi cha Simba kiko jijini Mwanza tangu juzi kikiendelea na maandalizi ya mchezo huo unaosubiriwa kwa hamu na mashabiki wa soka

Baada ya kupoteza mchezo uliopita dhidi ya Kagera Sugar, Simba imepania kusahihisha makosa yake na kuibuka na ushindi dhidi ya Alliance Fc leo

Kocha Mkuu wa Simba Patrick Aussems amesema anafahamu mchezo hautakuwa mwepesi lakini wanahitaji kuondoka na alama zote tatu

Katika mchezo wa leo Simba itamkosa beki kiraka Erasto Nyoni ambaye ni mgonjwa

Meneja wa Simba Patrick Rweyemamu amewataja Nyoni, Paschal Wawa na Shomari Kapombe kuwa wachezaji pekee watakaokosekana kwenye mchezo huo

Simba iliyoshuka dimbani mara 24 inashika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi ikiwa imejikusanyia alama 60

Bado mabingwa hao watetezi wana michezo nane ya viporo ambayo kama watashinda yote watajikita kileleni mwa msimamo wa ligi kwa tofauti ya alama 10 dhidi ya Yanga inayoongoza