FT : Azam Fc 0-1 Yanga

Mabingwa wa kihistoria wa Tanzania Yanga wameendelea kujiimarisha kileleni mwa msimamo wa ligi kuu baada ya kuichapa Azam Fc bao 1-0 katika mchezo uliopigwa uwanja wa Uhuru jijini Dar es salaam

Ikicheza kwa nidhamu na tahadhari kubwa, Yanga ilifunga bao lake pekee kwenye dakika ya 13 kupitia kwa winga Mrisho Ngasa aliyeunganisha mpira wa krosi uliochongwa na Ibrahim Ajib kutoka winga ya kulia

Krosi hiyo ya Ajib ilikuwa zao la shambulizi la kushitukizwa lililofanywa na Yanga

Ngasa sasa amefikisha mabao 5 msimu huu wakati Ajib ametengeneza bao la 16

Azam Fc ilitawala mchezo huo kwa muda mwingi hata hivyo mbinu ya mahiri ya kujilinda ya kocha Zahera iliwapa wakati mgumu wana ‘rambaramba’ hao kuipenya ngome ngumu ya Yanga iliyokuwa chini ya Abdallah Shaibu ‘Ninja’ na Andrew Vicent ‘Dante’

Azam ilipoteza nafasi pekee adimu kwenye dakika ya 84 baada ya Dani Lyanga kushindwa kuutumbukiza mpira kimiani akiwa amebaki na kipa Klaus Kindoki

Ushindi huo umeendelea kuiweka Yanga kileleni mwa msimamo wa ligi ikiwa imefikisha alama 77, ikiongoza kwa tofauti ya alama 8 dhidi ya Simba na alama 11 dhidi ya Azam Fc

Mchezo unaofuata ni dhidi ya Tanzania Prisons na utapigwa May 02 kwenye uwanja wa Taifa/Uhuru