FT : Yanga 0-1 Simba

Mabingwa wa soka Tanzania Bara Simba wameendeleza ubabe wao dhidi ya Yanga baada ya kuondoka na ushindi wa bao 1-0 katika mchezo baina ya timu hizo uliopigwa leo uwanja wa Taifa

Ulikuwa ni mchezo ambao mzani ulielemea upande wa Simba hata kabla mchezo huo haujapigwa kutokana na ubora wa kikosi cha Simba

Dakika 45 za kipindi cha kwanza zilimalizika kwa timu hizo kutofungana licha ya Simba kutawala kwa muda mwingi

Mabadiliko yaliyofanywa na kocha Patrick Aussems kwa kumtoa Chama na kumuingiza Dilunga kwenye kipindi cha pili yaliongeza umakini kwa wekundu wa Msimbazi na Dilunga ndiye aliyesaidia kupatikana kwa bao la Simba

Bao hilo pekee lilifungwa na Meddie Kagere katika dakika ya 72 akimalizia pasi murua ya nahodha John Bocco

Hilo lilikuwa bao la tisa kwa Kagere kwenye ligi msimu huu

Ushindi huo umeiweka Simba katika nafasi nzuri ya kutetea ubingwa wake dhidi ya wapinzani wao Yanga

Imefikisha alama 39 na kuchupa mpaka nafasi ya tatu.

Kama Simba itashinda michezo yake yote ya viporo itakuwa na uhakika wa kuwazidi alama tano wapinzani wao Yanga.