Simba inahitaji ushindi wa aina yoyote kwenye mchezo huo ili iweze kutinga robo fainali ya michuano hiyo kwa mara ya pili katika historia yake
Simba iliwahi kutinga robo fainali ya michuano hiyo mwaka 1974
Kwenye msimamo wa kundi D JS Saoura inaongoza ikiwa imejikusanyia alama nane ikifuatiwa na Al Ahly yenye alama saba sawa na Vita Club ambayo inashika nafasi ya tatu
Simba inashika nafasi ya nne ikiwa na alama sita
Bila ya kujali matokeo kati ya Al Ahly dhidi ya JS Saoura, ushindi utaihakikishia Simba kufikisha alama tisa na kujihakikishia moja ya tiketi mbili za kutinga robo fainali
Habari njema kwa Simba ni kwamba itakuwa ikicheza mchezo huo mbele ya mashabiki wake ambapo mkakati uliopo ni kuhakikisha siti zote elfu 60 katika uwanja wa Taifa zinakaliwa
Simba imejijengea rekodi ya kipekee inapocheza uwanja wa Taifa.
Msimu huu imefanikiwa kushinda michezo yake yote iliyocheza kwenye dimba hilo katika michuano ya ligi ya mabingwa
Miongoni mwa timu ambazo zilichezea kichapo ni Al Ahly, mabingwa mara nane wa taji la ligi ya mabingwa na vigogo wa soka barani Afrika
Al Ahly iliifunga Simba mabao 5-0 katika mchezo wa duru ya kwanza lakini ilishindwa kufua dafu ilipokuja ‘kwa Mkapa’
Morali hiyo iliyotumika kwa Al Ahly ndio hiyo itakayotumika kuimaliza Vita Club ambayo pia ilishinda kwa mabao 5-0 katika mchezo wa kwanza uliopigwa DR Congo
Katika mchezo huo Simba haina cha kupoteza, kwani matokeo yoyote tofauti na ushindi yataiondosha mashindanoni.
Hivyo hakuna shaka vijana wa Aussems watacheza mpira wa kushambulia mwanzo mwisho
Kocha Patrick Aussems amewaalika mashabiki wote wa soka Tanzania kujitokeza kwa wingi uwanja wa Taifa Jumamosi ili kuweza kuandika Historia pamoja na Simba