SIMBA : Yaapa kuikomalia JS Saoura LEO

Mabingwa wa soka Tanzania Bara Simba wako nchini Algeria ambapo leo Jumamosi March 09 2019 watashuka dimba la Agosti 20 kuikabili JS Saoura katika mchezo wa ligi ya mabingwa utakaopigwa saa nne usiku

Simba inaweza kuandika historia nyingine leo kwa kutinga robo fainali ya michuano hiyo mikubwa kabisa barani Afrika kwa ngazi ya vilabu

Mashabiki wa Simba na Watanzania wote kwa ujumla wametakiwa kuiombea timu dua njema ili iweze kupeperusha vyema bendera ya nchi huko ugenini

Aidha mafanikio ya Simba kwenye michuano hii ni mafanikio ya Tanzania kwani iwapo itafanikiwa kusonga mbele, itaiongezea Tanzania alama na pengine msimu ujao nchi inaweza kuongezewa idadi ya wawakilishi kwenye michuano hiyo

Kwa sasa Tanzania ina nafasi mbili tu kwenye michuano ya CAF wakati baadhi ya nchi zina nafasi hadi nne kutokana na vilabu vyao kufanya vizuri

Kocha Mkuu wa Simba Patrick Aussems amesema vijana wake wana ari ya kupata matokeo mazuri kwenye mchezo huo

“Hatukuja hapa kwa malengo ya kutafuta sare, tunataka kushinda mchezo huu,” amesema Aussems

Ushindi unaweza kuihakikishia Simba kutinga robo fainali kama Vital Club itashindwa kupata ushindi dhidi ya Al Ahly katika mchezo utakaopigwa mapema saa moja jioni

Lakini hata alama moja itaifaa Simba kuelekea mchezo wake wa mwisho dhidi ya Vita Club utakaopigwa uwanja wa Taifa Jumamosi ijayo March 16 2019

Kabwili augua Yanga ikijiandaa kuikabili KMC

Kesho Jumapili kikosi cha Yanga kitashuka dimba la Taifa kuikabili KMC katika mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara unaotarajiwa kuanza saa kumi kamili jioni

Katika mchezo wa kesho Yanga itakosa huduma ya mlinda lango wake kinda Ramadhani Kabwili ambaye ni mgonjwa

Hata hivyo, mkufunzi wa makipa Juma Pondamali amesema hana wasiwasi na kusokena kwa Kabwili kwa kuwa Kindoki na Hamid wapo

Yanga itaingia kwenye mchezo wa kesho ikiwa na kumbukumbu ya kuibuka na ushindi wa bao 1-0 kwenye mchezo wa mzunguuko wa kwanza, bao lililowekwa kimiani na Feisal Salum ‘Fei Toto’ kwa mkwaju wa adhabu kwenye dakika za lala salama

Ligi Kuu ya Tanzania Bara inaendelea leo kwa michezo minne kupigwa kwenye viwanja mbalimbali