Ibenge aivulia kofia Simba

Kocha Mkuu wa AS Vita Club Florent Ibenge amesema Simba ilistahili kushinda mchezo wa jana kutokana na kuwa katika kiwango bora kuliko timu yake

Vita Club ilikubali kichapo cha mabao 2-1 kutoka kwa Simba na kuondoshwa kwenye michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika ikiiacha Simba ikitinga robo fainali

Akizungumza baada ya mchezo jana, Ibenge alisema Simba ina wachezaji wazuri

Aidha, Ibenge alifichua kuwa walimuwekea ulinzi mkali Meddie Kagere kwa kuwa ndio mchezaji waliokuwa wakimuhofia zaidi

“Simba walionyesha ushindani mkali kwetu, walicheza vizuri matokeo waliyopata walistahili, tunawapongeza,” amesema

“Kagere ndio mchezaji tuliyekuwa tunamuhofia zaidi na niliwaagiza wachezaji wangu wamchunge lakini mwisho wa siku mpira ni mchezo wa makosa, tumefanya makosa tumeadhibiwa”

Mabao ya Simba yalifungwa na Mohammed Hussein na Clatous Chama aliyefunga bao la ushindi katika dakika za lala salama

Manara amtahadharisha Zahera

Afisa Habari wa Simba Haji Manara amesema wamebaini kocha wa Yanga Mwinyi Zahera hajasafiri na timu yake ambayo kesho inamchezo dhidi ya Lipuli Fc akibaki jijini Dar es salaam kuipokea AS Vita Club

Zahera ameonekana akiambatana na viongozi wa timu ya Vita Club itakayochuana na Simba hapo kesho

“Hii ni mechi ya kitaifa na ya kimataifa, tunaiwakilisha nchi, kuna kocha yeye kazi yake imekuwa ni kuzunguka na Vita tu na aliaga anaenda kwao Congo hata Iringa hajaenda.

“Hii ni mechi ambayo nchi inajua, Rais anajua, sasa ole wake aendelee kutuharibia mipango,” amesema Manara kwenye mahojiano yake na eFM radio

Akizungumzia maandalizi ya mchezo huo, Manara amesema kikosi kiko tayari, ari na morali ya wachezaji iko juu kuelekea mchezo huo

Amewataka mashabiki kuwahi mapema uwanja wa Taifa hapo kesho ili wawe sehemu ya historia ambayo Simba imepania kuiandika