Taarifa kuhusu mechi ya Simba vs JKT Tanzania

Taarifa kuhusu mechi ya Simba vs JKT Tanzania
Mechi kati ya Simba dhidi ya JKT Tanzania iliyopangwa kuchezwa leo katika uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro huenda isichezwe kutokana na hali ya mvua kubwa kunyesha na uwanja kujaa maji.

Kwasasa kinachosubiriwa ni nusu saa kupita kulingana na kanuni za kuahirisha mechi, ambayo kanuni mojawapo inataka angalau ipite nusu saa ndipo mechi ihairishwe.

Hiki hapa Kikosi cha Simba kitakacho cheza leo dhidi ya JKT Tanzania

Kikosi cha Simba dhidi ya JKT Tanzania leo

1. Deogratius Munish
2. Nicolas Gyan
3. Asante Kwasi
4. Yusuf Mlipili
5. Juuko Murshid
6. Said Ndemla
7. Hassan Dilunga
8. Jonas Mkude
9. Adam Salamba
10. John Bocco (c)
11. Clatous Chama

Wachezaji wa Akiba
1. Aishi Manula
2. Erasto Nyoni
3. Paul Bukaba
4. James Kotei
5. Rashid Juma
6. Meddie Kagere
7. Emmanuel Okwi

Okwi, Chama hawakugoma – Manara

Msemaji wa klabu ya Simba Haji Manara amesema wachezaji Emmanuel Okwi na Clatous Chama walichelewa kujiunga na kambi ya Simba mkoani Morogoro kutokana na sababu maalum na sio kweli kuwa wachezaji hao walifanya mgomo

Akizungumza na waandishi wa habari leo Makao Makuu ya klabu ya Simba yaliyopo mtaa wa Msimbazi, Manara amesema klabu iliwapa ruhusa wachezaji hao kushughulikia masuala yao ya kifamilia na tayari wamesharipoti mkoani Morogoro kujiunga na wenzao

“Hakuna mchezaji aliyegoma kama taarifa zinavyoenezwa huko mitandaoni hivi timu inayocheza klabu bingwa Africa kuna mchezaji anaweza kugoma?”, amehoji Manara

“Okwi na Chama walipewa ruhusa maalum na tayari wapo kambini toka jana”

“Sisi kwa sasa tunaweza chukua mchezaji yeyote hata Tp Mazembe sio kama kipindi kile kwa sasa simba ni giant inabeba yeyote”

“Tuna barua zaidi ya 100 za wachezaji mbalimbali wameomba kuchezea Simba msimu ujao tena wengine wametoka vilabu vikubwa hapa Tanzania wanahitaji kucheza hata bure”

Wasauzi wampagawisha Okwi,aanza mbwembwe

Simba huenda ikalazimika kufanya kazi ya ziada kumbakisha mshambuliaji wake hatari Emmanuel Okwi ambaye timu nyingi zimeonyesha nia ya kutaka kumsajili

Mkataba wa Okwi unatarajiwa kumalizika ndani ya siku 60 huku mchezaji huyo raia wa Uganda akionyesha dalili zote za kutaka kuondoka Msimbazi

Okwi anahusishwa na vilabu kadhaa vinavyoshiriki ligi kuu ya Afrika Kusini, Orlando Pirates na Kaizer Chiefs

Kocha Patrick Aussems alimuondoa Okwi katika kikosi kilichokwenda mkoani Morogoro baada ya mchezaji huyo kuchelewa kuripoti kambini

Meneja wa Simba Patrick Rweyemamu amesema hana taarifa kuhusu mshambuliaji huyo ambaye alikuja nchini na kikosi cha timu ya Taifa ya Uganda Cranes na alicheza mchezo dhidi ya Stars

“Mimi sijui chochote kuhusiana na Okwi labda waulizwe viongozi wangu wa juu, hayupo kwenye msafara wetu huu unaoelekea Morogoro, hivyo waulizwe viongozi wa juu suala lake,”Rweyemamu alinukuliwa na Championi jana

Hata hivyo Okwi amekuwa na kawaida ya kuchelewa kuripoti kambini kila anapotoka kutimiza majukumu ya timu ya Taifa

Hali ni tofauti kwa Juuko Murshid ambaye tangu aliporejeshwa kikosini, amekuwa akiwajibika ipasavyo

Juuko alikuwa miongoni mwa wachezaji waliowahi kuripoti kambini baada ya kumalizika michezo ya AFCON

Taarifa zilizopatikana mapema leo zimebainisha Okwi amerejea na ameshatua mkoani Morogoro kuungana na wenzake

Okwi, Chama waongeza nguvu Simba ikijiandaa kuikabili JKT Tanzania

Mshambuliaji Mganda Emannuel Okwi na kiungo Mzambia Clatous Chama tayari wamejiunga kwenye kambi ya Simba mkoani Morogoro kuelekea mchezo wa kesho dhidi ya JKT Tanzania

Okwi na Chama hawakuwa sehemu ya kikosi cha Simba kilichoifumua Mbao Fc mabao 3-0 baada ya wachezaji hao kuchelewa kurudi kutoka nchini kwao walikokwenda kutimiza majukumu ya timu ya Taifa

Baada ya mchezo wa kesho, Simba itaendelea kubaki mkoani Morogoro kuendelea na maandalizi ya mchezo wa robo fainali ligi ya mabingwa dhidi ya TP Mazembe

Mchezo huo utapigwa Jumamosi, April 06 kwenye uwanja wa Taifa

Simba vs JKT Tanzania kupigwa Jumatano

Mabingwa watetezi ligi kuu ya Tanzania Bara Simba keshokutwa Jumatano watashuka uwanja wa Jamhuri kuikabili JKT Tanzania katika mchezo wa ligi hiyo

Licha ya kukabiliwa na mchezo wa robo fainali ligi ya mabingwa siku ya Jumamosi, April 06 dhidi ya TP Mazembe, TFF imegoma kusogeza mbele mchezo dhidi ya JKT Tanzania ambao utapigwa April 03 2019 kama ulivyopangwa

Kocha Mkuu wa Simba Patrick Aussems amesema kwa sasa wanaelekeza nguvu zao kuelekea mchezo huo kabla ya kuanza maandalizi ya mchezo dhidi ya TP Mazembe

“Nitalazimika kubadili kikosi ili kila mchezaji apate nafasi kwani baada ya mchezo huo tutakuwa na siku mbili tu za kujiandaa kabla ya kuivaa TP Mazembe,” amesema

Akizungumzia ushindi wa mabao 3-0 ambao Simba ilipata jana dhidi ya Mbao Fc, Aussems alisema mipango yao ni kuhakikisha wanashinda kila mchezo ili waweze kutetea ubingwa hivyo ushindi huo unaendelea kuweka hai mipango yao

“Kila mechi tunacheza kushinda, hata huu mchezo tulistahili kushinda, tulianza kushambulia tangu mwanzo hadi mwisho, mchezo ulikuwa mgumu lakini tulitengeneza nafasi”

SIMBA 3-0 MBAO FC

Mabingwa watetezi ligi kuu ya Tanzania Bara Simba ni kama hawakamatiki baada ya leo kushinda mchezo wa 10 mfululizo kwa kuifumua Mbao Fc mabao 3-0 katika mchezo uliopigwa uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro

Mabao mawili ya nahodha John Bocco na moja la Meddie Kagere yametosha kuihakikishia Simba ushindi muhimu ambao umewasogeza karibu ya Azam Fc inayoshika nafasi ya pili baada ya kufikisha alama 57

Azam Fc ina alama 59 hata hivyo Simba ina michezo sita mkononi hivyo ni suala la muda tu mnyama atakaa katika nafasi yake na hatimaye kutetea ubingwa waliotwaa msimu uliopita

Mabao mawili aliyofunga Bocco leo yamemfanya afikishe mabao 11 akihitaji kufunga bao moja tu kumfikia Heritier Makambo wa Yanga

Kagere amezidi kumkaribia Salim Aiyee wa Mwadui Fc mwenye mabao 16, baada ya bao lake la mkwaju wa penati alilofunga leo kumfanya afikishe mabao 14

Baada ya ushindi wa leo kikosi cha Simba kitaendelea na maandalizi ya mchezo wa robo fainali ligi ya mabingwa dhidi ya TP Mazembe

Simba itaendelea kujifua mkoani Morogoro kujiandaa na mchezo huo utakaopigwa April 06 katika dimba la Taifa

Bocco, Kagere kuongoza maangamizi ya Mbao Fc leo

Nahodha wa kikosi cha Simba John Bocco ‘Adebayor’ yuko kwenye kiwango bora sana, leo anatarajiwa kuwaongoza mabingwa hao watetezi wa ligi kuu ya Tanzania Bara kuikabili Mbao Fc mkoani Morogoro

Baada ya kufanya kazi kubwa ya kuivusha Simba hatua ya robo fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa dhidi ya AS Vita, kisha akaivusha Stars fainali za AFCON 2019 katika mchezo dhidi ya Uganda kwa kutengeneza mabao mawili kati ya matatu yaliyofungwa na Stars, Bocco leo atakuwa dimbani kufanya kazi maalum ya kuitafutia Simba alama tatu muhimu

Aidha kinara wa upachikaji mabao katika kikosi cha Simba, Meddie Kagere naye atakuwa na nafasi ya kuongeza mabao yake na kumkaribia Salum Aiyee wa Mwadui Fc mwenye mabao 16

Kagere yuko nafasi ya pili kwenye orodha ya vinara wa upachikaji mabao akiwa na mabao 13

Bocco na Kagere wamerejea kikosini baada ya kutumikia timu zao za Taifa wakiwa ‘fit’ na hakuna shaka Aussems anazihitaji silaha hizi kuweza kuimaliza Mbao Fc baadae leo

Wadau wa Simba Morogoro wapongezwa kwa ukarabati uwanja wa Jamhuri

Simba itaweka makazi ya muda mkoani Morogoro ikitumia uwanja wa Jamhuri kwa baadhi ya michezo yake ya ligi wakati wote ambao uwanja wa Taifa utakuwa umefungwa

Katika kuhakikisha uwanja huo unakuwa na hali nzuri, wanachama na mashabiki wa klabu ya Simba mkoani Morogoro walijitolea kuufanyia ukarabati

Ukarabati uliofanywa ni pamoja na kun’goa magugu, kujaza vifusi sehemu zenye mashimo na kuotesha nyasi pamoja na kumwagilia katika kipindi cha wiki tatu zilizopita

Pia ukarabati umefanywa kwenye vyoo na vyumba vya kubadilishia nguo

Meneja wa uwanja huo John Simkoko amewapongeza Wanasimba kwa jitihada zao za kuuboresha uwanja huo

Simba itaanza rasmi kuutumia uwanja wa Jamhuri kama uwanja wake wa nyumbani kesho Jumapili itakapochuana na Mbao Fc katika mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara