Niyonzima ampagawisha Aussems, aapa kumbakisha Simba

Kocha Mkuu wa Simba Patrick Aussems amesema anajivunia uwepo wa kiungo Haruna Niyonzima katika kikosi chake na amesisitiza kiungo huyo hatauzwa

Katika siku za karibuni Niyonzima ameonekana kufanya vyema hali inayoashiria amerejea katika kiwango chake cha zamani

Ukizungumzia ushindi wa mabao 2-1 iliyopata Simba dhidi ya AS Vita na kutinga robo fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika, ni lazima utaje jina la Niyonzima kwani alikuwa miongoni mwa wachezaji waliojituma zaidi katika mchezo huo

Aussems amefichua kuwa wakati alipokutana na Niyonzima kwa mara ya kwanza baada ya kuanza kuinoa Simba, alibaini kiungo huyo alikuwa amekata tamaa

Aussems amesema alifanya kazi ya ziada kumrejesha nahodha huyo wa zamani wa timu ya Taifa ya Rwanda katika kiwango chake baada ya kubaini ni mchezaji mwenye kipaji cha hali ya juu

Anaamini uongozi wa Simba utamuongezea mkataba kwani ni miongoni mwa wachezaji anaowahitaji kwa ajili ya msimu ujao

Simba yaifuata Mbao Fc Morogoro

Msafara wa kikosi cha Simba umeondoka jijini Dar es salaam asubuhi ya leo Ijumaa, kuelekea Morogoro kwa ajili ya maandalizi ya mwisho kabla ya mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Mbao FC ambao utapigwa siku ya Jumapili kwenye uwanja wa Jamhuri

Leo jioni Simba inatarajiwa kufanya mazoezi yake ya kwanza katika uwanja wa Jamhuri ambao uongozi wa timu hiyo uliufanyia ukarabati wa sehemu ya kuchezea ‘pitch’

Baada ya mchezo dhidi ya Mbao Fc, Simba itaendelea kubaki mkoani Morogoro kuendelea na maandalizi ya mchezo wa robo fainali ligi ya mabingwa dhidi ya TP Mazembe

Simba tayari kuifuata Mbao Fc Morogoro

Mabingwa watetezi ligi kuu ya Tanzania Bara Simba kesho Ijumaa wanaelekea mkoani Morogoro tayari kwa mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Mbao Fc

Mchezo huo utapigwa siku ya Jumapili, March 31 katika uwanja wa Jamhuri

Kocha Mkuu wa Simba Patrick Aussems amesema wamedhamiria kutetea ubingwa wao, hivyo wanahitaji kushinda mchezo huo

“Tulipoteza mechi ya kwanza na Mbao Mwanza na sasa tumejipanga kuchukua pointi hizo tatu na kuhakikisha tunaanza kuutumia vyema uwanja wetu wa Jamhuri ambao tunaanza nao katika mchezo huo,” amesema Aussems

Hata hivyo licha maboresho yaliyofanywa, uwanja wa Jamhuri bado hauko katika kiwango bora, hali itakayomfanya Aussems alazimike kubadili mbinu ili kwendana na hali ya uwanja huo

“Kutumia Uwanja wa Jamhuri kama nyumbani hatuna jinsi, kutokana na tayari uwanja wa Taifa umefungwa, lakini kuna tofauti kubwa kati ya viwanja hivi”

“Tutajiandaa kucheza kufuatana na hali ya uwanja, muhimu tunahitaji ushindi”

Aussems amesema kikosi chake kitafanya mazoezi kwenye uwanja wa Jamhuri kesho jioni na pengine Jumamosi asubuhi kabla ya kuikabili Mbao Fc Jumapili

Simba inashika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi ikiwa imejikusanyia alama 54, huku ikiwa na michezo nane kibindoni

Hesabu za kutetea ubingwa kwa kocha Aussems zinakwenda sawa mpaka sasa kwani kama Simba itashinda michezo yake yote ya viporo, itaizidi Yanga inayoongoza ligi hiyo kwa alama nane

Simba ilivyoizidi ujanja AS Vita kwa Tuyisenge

Uongozi wa klabu ya Simba tayari umemalizana na mshambuliaji wa Gor Mahia Jacques Tuyisenge ambaye pia alikuwa akiwaniwa na AS Vita Club ya DR Congo

Baada ya kumpoteza mshambuliaji wake Jean Mark Makusu aliyetimkia nchini Morocco, Vita ilikuwa mbioni kumsajili Tuyisenge kuchukua nafasi yake

Hata hivyo Meddie Kagere aliyekuwa ‘pacha’ wa Tuyisenge katika klabu ya Gor Mahia ambaye pia ni pacha wake katika kikosi cha timu ya Taifa ya Rwanda, amechangia kwa kiasi kikubwa kumshawishi Tuyisenge kutua Simba

Simba imempa Tuyisenge mkataba wa awali wa miaka miwili akitarajiwa kuanza kazi mwishoni mwa msimu

Tuyisenge alikutana na mabosi wa Simba juzi usiku katika kikao ambacho kilikuwa na mafanikio kwa pande zote mbili kufikia makubaliano

Dida anolewa kuibeba Simba mchezo dhidi ya Mbao Fc

Mlinda lango namba moja wa Simba Aishi Manula alipata majeraha ya kiganja cha mkono wakati akiitumikia timu ya Taifa kwenye mchezo dhidi ya Uganda

Licha ya kuhudhuria mazoezi ya Simba leo, Manula bado anaonekana hayuko vizuri, ambapo benchi la ufundi limelazimika kumuandaa kikamilifu golikipa namba mbili Deo Munishi ‘Dida’ kuelekea mchezo dhidi ya Mbao Fc

Baada ya mlinda lango kinda Ali Salim kuitwa katika kikosi cha timu ya Taifa U20, Simba imebaki na walinda lango wawili wa kikosi cha kwanza Manula na Dida

Hakuna uhakika kama Manula atakuwa ‘fit’ kabla ya Jumapili lakini huenda Simba ikalazimika kuongeza mlinda lango mwingine kutoka kikosi cha pili kuelekea mchezo wa Jumapili

UWANJA WA SIMBA SC BUNJU

Ujenzi wa uwanja wa Simba ulioko Bunju nje kidogo ya jiji la Dar es salaam ulisimama kwa muda kutokana na nyasi bandia za uwanja huo kushikiliwa na TAKUKURU kwa ajili ya uchunguzi wa kesi iliyokuwa ikiendelea

Hata hivyo Mtendaji Mkuu wa Simba Crescentius Magori amesema tayari TAKUKURU imeziachia nyasi hizo hivyo wakati wowote ujenzi wa uwanja huo utaendelea

Awali uwanja huo ulitarajiwa kukamilika mwezi wa pili lakini sasa baada ya nyasi hizo kuachiwa, Magori amesema ujenzi utakamilika baada ya wiki mbili

Mwekezaji wa klabu ya Simba Mohammed Dewji ‘Mo’ aliahidi kuukamilisha uwanja huo tayari kuanza kutumika kabla ya msimu huu kumalizika

AISHI MANULA : MAJERUHI

Mlinda lango namba moja wa Simba na Stars Aishi Manula, huenda akahitaji siku kadhaa za mapumziko baada ya kupata majeraha wakati akiitumikia Taifa Stars kwenye mchezo dhidi ya Uganda juzi

Kocha Mkuu wa Simba Patrick Aussems amesema Manula hatakuwa sehemu ya kikosi cha Simba kilichofanya maandalizi kuelekea mchezo dhidi ya Mbao Fc Jumapili

Wakati huo huo Aussems amesema wachezaji wote wa Simba waliokuwa na majukumu ya timu za Taifa wanatarajiwa kuanza kuwasili leo kuungana na wenzao ambao walianza mazoezi juzi kwa ajili ya maandalizi ya michezo inayofuata

Ukiondoa Aishi Manula, wachezaji wengine wanaotarajiwa kuripoti kambini kuanzia leo ni John Bocco, Jonas Mkude, Erasto Nyoni, Emmanuel Okwi, Juuko Murshid, Meddie Kagere na Clatous Chama

Ajib, Tuyisenge watajwa Msimbazi

Nahodha wa Yanga Ibrahim Ajib huenda akarejea katika klabu ya Simba, mahali alipokuza jina lake kwenye soka

Inaelezwa Ajib ambaye mkataba wake na Yanga unamalizika mwishoni mwa msimu, tayari amesaini mkataba wa awali kurudi Msimbazi

Ajib alisajiliwa na Yanga mwaka juzi akipishana na Haruna Niyonzima aliyetua Msimbazi

Simba tayari imeanza mkakati wa kukiboresha kikosi chake kwa ajili ya msimu ujao ambapo mbali na Ajib, mabingwa hao wa Tanzania Bara inaelezwa tayari wametua nchini Kenya kumnyakua mshambuliaji wa Gor Mahia, Jacques Tuyisenge

Tuyisenge aliyeisaidia Gor Mahia kutinga robo fainali ya kombe la Shirikisho Barani Afrika, ataondoka Gor Mahia mwishoni mwa msimu mkataba wake utakapokuwa umemalizika

Msimu uliopita Tuyisenge alikuwa pacha wa Meddie Kagere katika kikosi cha Gor Mahia kilichokuwa kikinolewa na Dylan Kerr

Simba kwenda Morogoro Ijumaa, kuivaa Mbao Fc Jamhuri Stadium

Mchezo wa ligi kuu kati ya Simba dhidi ya Mbao Fc utapigwa kwenye dimba la Jamhuri Jumapili, March 31 2019 ambapo kikosi cha Simba kinatarajiwa kuelekea mkoani Morogoro Ijumaa ya wiki hii

Meneja wa Simba Patrick Reyemamu amesema wanatarajia kuweka kambi ya mkoani Morogoro kujiandaa na mchezo dhidi ya TP Mazembe

Aidha Simba imechagua kutumia uwanja wa Jamhuri kwa ajili ya michezo yake ya nyumbani wakati ambao uwanja wa Taifa utakuwa umefungwa kupisha michuano ya AFCON kwa vijana inayoanza April 14-28 2019

Kwa sasa Simba inafanya mazoezi uwanja wa Boko Veterans ambapo wachezaji waliokuwa na majukumu katika timu za Taifa wanatarajiwa kuanza kuwasili kesho

Simba yarejea mazoezini kuiwinda Mbao Fc

Baada ya mapumziko ya sikua tano, kikosi cha Simba kimerejea mazoezini leo kujiandaa na mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara dhidi ya Mbao Fc

Mchezo huo unatarajiwa kupigwa Jumapili, March 31 na huenda ukapigwa kwenye uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro

Mazoezi ya leo yalihusisha wachezaji ambao hawakuitwa katika timu za Taifa