Yanga kuunda Kamati ya Usajili

Uongozi wa klabu ya Yanga uko katika mchakato wa kuunda Kamati ya usajili ambayo itashirikiana na Kocha Mwinyi Zahera kusimamia usajili wa timu hiyo

Akizungumza na waandishi wa habari leo katika Mkutano uliofanyika Makao Makuu ya Yanga jijini Dar es salaam, Mwenyekiti wa timu hiyo Dk Mshindo Msolla amesema tayari uteuzi umeshafanyika kwa sasa wanafanya majadiliano na wajumbe walioteuliwa kabla ya kuwaweka hadharani

“Wajumbe wa Kamati hiyo tumeshawateua lakini hatuwezi kuwatangaza kabla nao hawajaridhia,” amesema Dk Msolla

“Wiki ijayo tutakuwa na kikao na benchi la Ufundi, pengine katika kikao hicho tutaitangaza Kamati”

“Msimu huu tumedhamiria kufanya usajili makini wenye tija”

Aidha Dk Msolla amesema hata hivyo jukumu la kutafuta wachezaji litabaki kwa kocha Zahera na benchi lake la ufundi, Kamati hiyo itakuwa na jukumu la kumsaidia kukamilisha michakato ya usajili baada ya makubaliano kufikiwa

Dk Msolla amesema kuanzia msimu ujao watawatumia wachezaji waliocheza Yanga zamani kutafuta wachezaji

“Msimu ujao kazi kubwa itafanywa na wachezaji wetu wa zamani kwani tutawapa jukumu la kutembea mikoani kutafuta wachezaji wenye vipaji”

Azam yanyemelea nyota Simba

Wakati klabu ya Simba ikiwa ‘busy’ kuhakikisha inatetea ubingwa wake, baadhi ya nyota wake ambao mikataba yao imemalizika, wameingia kwenye rada za Azam Fc

Aishi Manula, Shomari Kapombe, Erasto Nyoni na John Bocco waliotua Simba kutoka Azam Fc misimu miwili iliyopita, wanatajwa kuwaniwa tena na timu hiyo

Baada ya kuachana na mpango wa kubana matumizi, Azam Fc imepanga kufanya usajili mkubwa ili kuwa washindani wa kweli katika kuwania ubingwa wa ligi kuu msimu ujao

Inaelezwa uongozi wa Simba umepanga kuanza michakato ya usajili baada ya kukamilisha mpango wa kutetea ubingwa

Zaidi ya nyota 10 wa kikosi cha Simba mikataba yao inamalizika mwishoni mwa msimu

Tiketi Mechi dhidi ya Sevilla zimeanza kuuzwa

Tiketi kwa ajili ya kuushuhudia mchezo wa Kimataifa wa Kirafiki kati ya Simba dhidi ya Sevilla tayari zimeanza kuuzwa kupitia Selcom

Kiingilio cha chini cha mchezo huo utakaopigwa May 23 saa moja jioni, Mzunguuko ni Tsh 5,000/- wakati majukwaa ya VIP ni Tsh 15,000/-

Pia kutakuwa na tiketi za Platinumambazo zitapatikana kwa Tsh 100,000/-, kwa wanaohitaji tiketi hizi wawasilane na 0745346687

Mchezo huu wa Kimataifa utakuwa wa kihistoria, sio wa kukosa!

SIMBA WASHUSHA MAJEMBE MAPYA

MABOSI wa Simba kwa msimu ujao hawataki mchezo kwani wamedhamiria kukisuka hasa kikosi chao kiwe cha ushindani na kwa kuanza hivi karibuni watazishusha sura mpya nne za kigeni, akiwemo mshambuliaji Mzambia, Lazarus Kambole.
Mabosi wa Simba wanataka kukiboresha kikosi chao kwa kuleta wachezaji wenye viwango vikubwa kutokana na aina ya matokeo ambayo walikuwa wanayapata kwenye michezo ya Ligi ya Mabingwa Afrika ya ugenini kwa msimu huu.
Chanzo kutoka Simba kimeliambia Championi Jumatatu, kuwa wachezaji hao wane wanatarajiwa kuingia nchini hivi karibuni ambapo wanaweza kuwemo kwenye mechi ya kirafiki ya kimataifa kati ya Simba na Sevilla ya Hispania.

“Viongozi wanataka kuboresha kikosi kiwe na uwezo wa hali ya juu kwenye michezo ya kimataifa kuliko msimu huu, ndiyo maana viongozi wanaleta wachezaji wenye uwezo wa hali ya juu kuliko ambao wapo kwa sasa.

“Wachezaji hao wanaweza kuwepo hapa nchini kwenye mechi na Sevilla kwa ajili ya kuangaliwa na kuongea na viongozi kabla ya kusaini mikataba kwa msimu ujao.
“Huyo Kambole unayesema anaweza kuwemo katika orodha hiyo, lakini ni suala la kusubiri kuona kama ni yeye ambaye atakuja hapa ama la,” kilisema chanzo hicho.

Katibu wa Simba, Anord Kashembe amesema: “Huu siyo wakati wa kufanya usajili, hatuwezi kulizungumzia hilo, ukifika muda wake kila kitu kitakuwa sawa.”

Chanzo: championi & gpl

TFF yafafanua kutoikabidhi Simba ubingwa mchezo dhidi ya Sevilla

Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), limeamua kumuondoa wasiwasi kocha wa Yanga, Mwinyi Zahera ambaye alikerwa na maneno ya msemaji wa Simba Haji Manara kwamba ubingwa watakabidhiwi wakati wa mechi yao na Sevilla inayoshiriki Ligi Kuu nchini Hispania (La Liga).

Kupitia msemaji wa TFF, Clifford Marion Ndimbo aliliweka sawa jambo hilo kwamba hakuna kanuni ya shirikisho inayoruhusu bingwa akabidhiwa kombe nje na mechi ya Ligi Kuu Bara.

“TFF ina kanuni zake hata Simba wakiandika barua kama alivyosema msemaji wao Manara kwamba endapo wangeshinda mechi zao wakabidhiwe taji la ubingwa kwenye mechi yao na Sevilla hakuna kitu kama hicho na hakitafanyika.

“Kama Zahera ana wasiwasi na hilo basi ajue kabisa kwamba TFF ina kanuni zake hata wakiandika barua hiyo, majibu yao ni rahisi kuwa kanuni haziruhusu mambo hayo”anasema.

Kuna video inayomuonyesha Zahera kwamba Simba watakabidhiwa ubingwa wakati sio mabingwa baada ya kusikia kauli ya msemaji wa Simba, Manara kuwa wataiomba TFF wawakabidhi kombe wakati wa mchezo wao na Sevilla.

Mwanaspoti

Mechi tano za kumaliza msimu Simba

Licha ya kutopata ushindi kwenye michezo miwili iliyopita, hesabu za ubingwa kwa Simba bado ziko salama ikihitaji kushinda angalau michezo mitatu kati ya mitano iliyobaki

Ratiba ya mechi zilizobaki za Wekundu hao wa Msimbazi inaonyesha keshokutwa May 16 watakuwa uwanja wa Uhuru kuikabli Mtibwa Sugar kisha kurejea tena uwanjani hapo May 19 kucheza na Ndanda Fc

May 21 Simba itasafiri kwenda mkoani Singida kuikabili Singida United kisha kurejea jijini Dar es salaam kucheza mchezo wa Kimataifa wa kirafiki dhidi ya Sevilla May 23

May 25 itarudi uwanja wa Uhuru kuikabili Biashara United na itamaliza msimu mkoani Morogoro kwa kuikabili Mtibwa Sugar May 28

Mo Simba awards kutolewa May 30 2019

Hafla ya utoaji Tuzo za Mo Simba 2019 itafanyika siku ya Ijumaa Mei 30, 2019 katika hoteli ya Hyatt Regency, The Kilimanjaro iliyopo Jijini Dar es Salaam

Tuzo za mwaka huu zitahusisha wachezaji na mashabiki wa Simba ambao juhudi zao zimesaidia kupatikana kwa mafanikio makubwa msimu huu

Tuzo hizo zitakuwa na vipengele 11 ambavyo ni Mchezaji Bora, Goli Bora, Golikipa Bora, Beki Bora, Kiungo Bora na Mshambuliaji Bora

Nyingine ni Mchezaji Bora Mwanamke, Mchezaji Bora Mdogo, Shabiki Bora, Tuzo ya Heshima na Mhamasishaji Bora katika mitandao ya kijamii