Wanachama Yanga wakumbushwa kuhakiki majina yao

Yanga iko ndani ya mchakato wa uchaguzi ambao utahitimishwa May 05 mwaka huu kwa Wanachama wa klabu hiyo kuchagua viongozi wapya

Uongozi wa Yanga umewataka viongozi wa Matawi kuwakumbusha wanachama wahakiki majina yao kwenye ‘ledger’ zilizo kwenye matawi yao

Wanachama wa Yanga pia wamekumbushwa kulipia ada za uanachama ili kuwa na sifa ya kuchagua viongozi katika uchaguzi utakaofanyika May 05

Uchaguzi utahusisha wanachama wote wenye kadi za kitabu na wale wenye kadi za posta.

Ten awapiga ‘dongo’ Simba, ‘vumilieni ndio ukubwa huo’

Afisa Habari wa Yanga Dismas Ten amewataka mashabiki wa Simba wavumilie ‘madongo’ wanayovurumishiwa baada ya jana kufumuliwa mabao 4-1 na TP Mazembe na kuondoshwa katika michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika hatua ya robo fainali

Kutupwa nje ya michuano hiyo kwa Simba kuliibua shangwe kubwa miongoni mwa mashabiki wa Yanga na hii inatokana na Simba kutumia mafanikio yao msimu huu ‘kuwanyanyasa’ watani zao Yanga ambao wanapita katika kipindi kigumu

Ten amesema Yanga na Simba ni watani wa jadi hivyo ni vyema wakavumilia matani wanayokutana nayo mtaani kwani na wao wamekuwa wakifanya hivyo wakati wote ambao Yanga inakumbwa na changamoto

“Ndiyo Sisi na ninyi ni watani na tunataniana kweli hasa timu zetu zinapokosa matokeo,” ameandika Ten kwenye ukurasa wake wa mtandao wa Instagram

“Bahati mbaya ni kwamba ninyi mnapenda kutania wenzenu lakini mkitaniwa ninyi ‘Nongwa’ mnahamia kwenye kashfa..! Mkikashifiwa nanyi mnaanza kulialia”

“Hongereni kwa hatua mliyofika, muhimu ni kuangalia wapi mmekosea ili mfanikiwe zaidi siku za usoni”

“Wakati sisi tunajiuliza nanyi mjiulize zaidi. Msimvuruge @moodewji ili aendelee kuwabeba..!”

Aidha Ten amewakaribisha Simba kwenye ligi kuu huku akiwatupia ‘dongo’ kuwa mitandao yao ya simu itakuwa imejaa tayari kwa kufanya miamala

“La huko limeisha, mrudi bongo sasa najua simu zenu zina line mbili mbili yaani full network kama siyo Mpesa basi Tigopesa…!”

Baada ya kutolewa Simba inarejea kwenye ligi ikikumbana na rundo la ‘viporo’ ambavyo watatakiwa wavimalize ndani ya kipindi cha mwezi mmoja

Katika kipindi hicho Simba wanapaswa kucheza michezo 16 kwani ligi imepangwa kumalizika mwishoni mwa mwezi wa tano ili kupisha maandalizi ya timu ya Taifa ambayo mwezi Juni inaelekea Misri kushiriki fainali za AFCON 2019

Njooni mtuunge mkono mchezo dhidi ya Nigeria – Nahodha Serengeti Boyz

Kikosi cha timu ya Taifa ya vijana umri chini ya miaka 17 Serengeti Boyz leo kinashuka dimba la Taifa kuikabili Nigeria kwenye mchezo wa ufunguzi wa michuano ya AFCON U17, mchezo utakaopigwa saa kumi kamili jioni

Tanzania ni mwenyeji wa michuano hiyo inayoanza kutimua vumbi leo katika viwanja vya Azam Complex na Taifa

Nahodha wa kikosi cha Serengeti Boyz Morris Michael amewataka Watanzania wajitokeze kwa wingi uwanja wa Taifa watakapokuwa wakiikabili Nigeria leo

“Nimezungumza na wenzangu na kuwashusha presha kwamba tunaenda kucheza mchezo wa kawaida kama michezo mingine ambayo tumecheza, kwa hiyo tuuone wa kawaida,” amesema

“Ni mechi kubwa lakini hatutakiwi kuwa na presha, tunatakiwa kupambana hadi mwisho kupata ushindi.”

“Tukishinda mchezo huu tutapata picha nzuri ya matarajio yetu hapo mbele tofauti na tukipoteza au kupata sare.”

“Watanzania waje kutuunga mkono kwa sababu tupo nyumbani naamini tutafanya kitu ambacho watanzania hawataamini”

Viingilio vya mchezo huo VIP ni Tsh 5,000/- na upande wa mzunguuko ni Tsh 2,000/-

Ajib mbioni kurejea kikosini Yanga

Nahodha wa Yanga Ibrahim Ajib amekosekana dimbani kwa takribani wiki tatu akisumbuliwa na majeraha ya nyonga

Kinara huyo wa kutengeneza mabao ligi kuu huenda akarejea kikosini kwenye mchezo ujao dhidi ya Mtibwa Sugar utakaopigwa mkoani Morogoro April 17 2019

Kukosekana kwake katika michezo iliyopita kumeibua maswali mengi miongoni mwa mashabiki wa Yanga hasa baada ya kuibuka tetesi kuwa anataka kurudi katika timu yake ya zamani, Simba

Hata hivyo Msemaji wa Yanga Dismas Ten amesisitiza kuwa Ajib amekosa michezo iliyopita kutokana na kuwa majeruhi na si vinginevyo

Amesema atarejea kikosini baada ya kupona majeraha hayo

MAKUNDI AFCON 2019

MAKUNDI YOTE SITA: #AFCON2019

Kundi A
Misri
DR Congo
Uganda
Zimbabwe

Kundi B
Nigeria
Guinea
Madagascar
Burundi

Kundi C
Senegal
Algeria
Kenya
Tanzania

Kundi D
Morocco
Ivory Coast
South Africa,
Namibia

Kundi E
Tunisia
Mali
Mauritania,
Angola

Kundi F
Cameroon
Ghana
Benin,
Guinea-Bissau

Makambo amuwashia taa nyekundu Aiyee

Bao alilofunga Heritier Makambo leo limemfanya mshambuliaji huyo Mcongoman afikishe mabao 15 akimuacha Meddie Kagere wa Simba mwenye mabao 14.

Leo Makambo aliisaidia Yanga kuibuka na ushindi muhimu wa mabao 3-2 dhidi ya Kagera Sugar

Makambo sasa anahitaji kufunga bao moja zaidi ili aweze kumfikia Salim Aiyee wa Mwadui Fc anayeongoza kwa ufungaji akiwa na mabao 16

Katika michezo miwili iliyopita, Makambo ameifungia Yanga mabao matatu

Waziri Mkuu aichangia Yanga Milioni moja, kupewa cheti Maalum

KAMATI YA HAMASA YA KUCHANGIA YANGA 2019

Kamati ya Hamasa ya Kuchangia Klabu ya Yanga inatoa shukurani kwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Majaliwa Kassim Majaliwa (MB) Kwa kuwa mchangiaji wa Kwanza kuichangia Klabu ya Yanga ambayo ina historia kubwa ya upatikanaji wa Uhuru wa Nchi yetu ya Tanzania.

Waziri Mkuu ameichangia Klabu ya Yanga kiasi cha shilingi milioni moja (1,000,000/=).

Kamati ya Hamasa kwa niaba ya Wanachama, Mashabiki na Wapenzi wa Klabu ya Yanga ina imani kubwa kuwa, mchango huu utakuwa chachu kwa Viongozi wengine wa ngazi zote kwa Taasisi za Umma na Binafsi bila kujali Itikadi, Jinsia na hata Ushabiki wa kijadi wa Yanga na Simba na hatimaye kuunga mkono jitihada hizi za Kiukombozi za KLABU YA YANGAzenye kauli mbiu ya Timu ya Wananchi Wawekezaji ni Wananchi Wenyewe

Cheti Maalumu kitatolewa kwa Mh. Waziri Mkuu na Mwenyekiti wa Kamati Mh. Anthony Peter Mavunde (MB) wakati wa kuhitimisha zoezi hili Maalumu

Deo Mutta
KNY – Kamati ya Hamasa ya Kuchangia

Makambo ataja siri ya kufunga mfululizo CCM Kirumba

Kinara wa mabao wa kikosi cha Yanga Heritier Makambo amesema ubora wa uwanja wa CCM Kirumba ni moja ya sababu inayomfanya aendelee ‘kutupia mabao’ kila anashuka katika dimba hilo

Makambo amefunga mabao matano CCM Kirumba, manne akifunga kwenye michezo ya ligi na moja akifunga kwenye michuano ya kombe la FA (ASFC)

Mabao matatu ameyafunga katika michezo miwili iliyopita dhidi ya African Lyon na jana dhidi ya Kagera Sugar

“Najisikia tofauti ninapocheza kwenye uwanja wa CCM Kirumba. Nadhani ubora wa uwanja unachangia mimi kufanya vizuri,” amesema

“Tumekuwa tukipata matokeo mazuri kila tunapocheza hapa, hakuna tofauti na tulivyokuwa tukicheza uwanja wa Taifa”

“Nawapongeza wachezaji wenzangu pia kwani wanachangia mimi kufanya vizuri”

Msimu huu Yanga imeshinda michezo yote ya ligi na kombe la FA iliyocheza katika uwanja wa CCM Kirumba

Aidha akizungumzia mbio za kuwania kiatu cha dhahabu, Makambo amesema ataendelea kufunga kila anapopata nafasi ili kuisaidia Yanga kupata matokeo. Ligi bado inaendelea na lengo lake ni kuendelea kufanya vizuri

Makambo amefunga mabao 15, anashika nafasi ya pili katika orodha ya wafungaji bora nyuma ya Salim Aiyee wa Mwadui Fc mwenye mabao 16

FT: YANGA 3-2 KAGERA SUGAR

Vinara wa ligi kuu ya Tanzania Bara Yanga wameendeleza ubabe katika uwanja wa CCM Kirumba baada ya kuifumua Kagera Sugar mabao 3-2
Kagera Sugar ilitangulia kufunga bao la kuongoza kwenye dakika ya 30 likiwekwa kambani na Paul Ngalyoma aliyeunganisha kwa kichwa mpira wa kona

Dakika nne baadae Yanga ilisawazisha bao hilo baada ya Kassim Khamis kujifunga wakati akijaribu kuokoa mpira wa kichwa uliopigwa na Papi Tshishimbi
Mpaka wakati wa mapumziko matokeo yalikuwa 1-1

Yanga ilihitaji dakika tatu tu za kipindi cha pili kuandika bao la pili lililowekwa kimiani na Heritier Makambo aliyeunganisha kwa kichwa mpira wa juu uliovushwa na Kelvin Yondani

Kagera Sugar wakasawazisha tena kwenye dakika ya 58 baada ya shuti la Kassim Khamis kumshinda mlinda lango Klaus Kindoki na kutinga kimiani
Kiungo Thabani Kamusoko aliihakikishia Yanga alama tatu muhimu baada ya kufunga bao la tatu kwenye dakika ya 72
Kamusoko aliukwamisha nyavuni mpira wa adhabu kwa ustadi mkubwa

Kwenye dakika ya 82 Yanga ilipata pigo baada ya kelvin Yondani kuonyeshwa kadi nyekundu kufuatia tukio la kumpiga kiwiko mchezaji wa Kagera Sugar

Matokeo hayo yameifanya Yanga ifikishe alama 74 na kuendelea kujikita kileleni mwa msimamo wa ligi kwa tofauti ya alama 11 dhidi ya Azam Fc inayoshika nafasi ya pili