Simba yawasili salama Mbeya

Msafara wa kikosi cha Simba umewasili salama mkoani Mbeya tayari kwa michezo miwili ya ligi kuu ya Tanzania Bara dhidi ya Mbeya City na Tanzania Prisons

Simba iliondoka jijini Dar es salaam mchana wa leo Alhamisi kwa usafiri wa Ndege

Kesho May 03 itacheza mchezo wa kwanza dhidi ya Mbeya City kwenye uwanja wa Sokoine na siku mbili baadae kurudi tena katika uwanja huo kuikabili Tanzania Prisons

Prisons iko jijini Dar es salaam ambapo leo imecheza na Yanga na kufungwa mabao 2-1, itachuana na Simba May 05

FT : Yanga 2-1 Prisons

Yanga imeendelea kujiimarisha kileleni mwa msimamo wa ligi baada ya kuichapa Tanzania Prisons mabao 2-1 katika mchezo uliopigwa uwanja wa Uhuru jijini Dar es salaam

Yanga iliyokuwa bora katika mchezo wa leo, ilifunga mabao yake kupitia kwa Wacongomani Papi Tshishimbi na Heritier Makambo wakati bao la kufutia machozi kwa upande wa Prisons lilifungwa na Ismail Kada

Tshishimbi ndiye aliyeanza kuifungia Yanga bao la kuongoza kwenye dakika ya 23 akimalizia mpira wa adhabu uliochongwa na Ibrahim Ajib

Hilo lilikuwa bao la 16 kutengenezwa na Ajib msimu huu

Dakika tisa baadae Kada aliisawazishia Prisons akiujaza mpira wavuni baada ya walinzi wa Yanga kuzembea kuondoa mpira wa kona

Makambo aliihakikishia Yanga ushindi kwenye dakika ya 66 akiunganisha kwa kichwa krosi ya Paulo Godfrey ‘Boxer’

Ushindi huo umeifanya Yanga kuwa timu ya kwanza kufikisha alama 80 msimu huu na kuendelea kujikitia kileleni mwa msimamo wa ligi kwa tofauti ya alama nane dhidi ya Simba inayoshika nafasi ya pili ikiwa na alama 72

Baada ya ushindi huo, Yanga itaelekea mkoani Iringa tayari kwa mchezo wa nusu fainali kombe la FA (ASFC) dhidi ya Lipuli, mchezo ukitarajiwa kupigwa Jumapili, May 05

Makambo awafikia Aiyee, Kagere

Bao alilofunga Heritier Makambo katika mchezo dhidi ya Tanzania Prisons limemfanya mshambuliaji huyo afikishe mabao 16 na kuwafikia Salum Aiyee wa Mwadui Fc na Meddie Kagere wa Simba

Leo Makambo ameiongoza Yanga kuibuka na ushindi muhimu wa mabao 2-1 dhidi ya Tanzania Prisons

Mshambuliaji huyo kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, anayo nafasi ya kuibuka mfungaji bora msimu huu kama ataweza kuitumia vyema michezo minne iliyobaki kujiongezea mabao

Michezo iliyobaki ni dhidi ya Ruvu Shooting, Mbeya City, Biashara United na Azam Fc

Ni mchezo mmoja tu dhidi ya Biashara United ambao utapigwa nje ya jiji la Dar es salaam

Wawa aanza mazoezi, kurejea kikosini karibuni

Beki kisiki wa Simba Paschal Serge Wawa ameanza mazoezi mepesi tayari kurejea dimbani baada ya kuwa nje kwa zaidi ya wiki tatu

Wawa aliumia kwenye mchezo wa kwanza wa robo fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika kati ya Simba dhidi ya TP Mazembe uliopigwa uwanja wa Taifa

Wawa ameanza mazoezi binafsi na huenda akajumuishwa kwenye kikosi cha Simba kitakaporudi kutoka mkoani Mbeya

Mwenyewe amethibitisha kuwa hali yake inaendelea vizuri na tayari ameshaanza mazoezi binafsi

“Ninaendelea vizuri kwa sasa tofauti na awali na nimeanza mazoezi binafsi na sasa hivi ninafanya mazoezi ya Gmy,” amesema

Simba imecheza michezo sita ya ligi bila ya Wawa na imefanikiwa kushinda michezo mitano

Walinzi Juuko Murshidi, Paul Bukaba na Yusufu Mlipili wameweza kutimiza ipasavyo majukumu ya ulinzi wa kati wakishirikiana na mkongwe kiraka Erasto Nyoni

Igangula kuanza na uwanja wa Kaunda

Mgombea wa nafasi ya Mwenyekiti wa klabu ya Yanga Baraka Igangula amesema kama atachaguliwa kuwa Mwenyekiti wa klabu hiyo, atahitaji miezi mitatu tu kukamilisha ukarabati wa uwanja wa Kaunda ambao unamilikiwa na Yanga

Aidha Igangula anayechuana na Dk Mshindo Msolla, Dr Jonas Tiboroha na Elias Mwanjala kuwania uwenyekiti wa Yanga, amesema kutokana na uzoefu mkubwa aliyokuwa nao kwenye uongozi wa Yanga, ana lengo la kuifanyia timu hiyo mambo makubwa na kamwe hataweka mbele maslahi binafsi

“Tutakuwa na mpango wa muda mfupi ambao tutaukarabati uwanja wetu pale klabuni, huku tukiwa na mpango wa muda mrefu wa kujenga uwanja nje ya mji, hata ikiwezekana Kibaha, Pwani ambao utakuwa na hosteli, maduka na ofisi mbalimbali,” amesema Igangula

Igangula pia ameunga mkono mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji wa Yanga akiahidi kulikamilisha zoezi hilo haraka

“Nitasimamia mchakato wa mabadiliko na kuhakikisha unakamiliki punde tu nitakapoingia madarakani. Nitaajiri wataalamu wenye ujuzi wa masuala ya kampuni ili tuachane na utaratibu huu wa kuendesha klabu kwa mazoea”

Ahadi nyingine alizotoa Igangula ni kuanzisha bima ya afya itakayowalenga wanachama, saccos, vicoba na mfuko wa kufa na kuzikana, kama sehemu ya kuimarisha umoja, upendo na mshikamano baina ya wanachama na viongozi wa Yanga

Pia atahakikisha wachezaji na benchi la ufundi wanalipwa mishahara kwa wakati, kusimamia mikataba na mapato ili kudhibiti ufisadi

Uchaguzi wa Yanga utafanyika Jumapili, May 05 ukumbi wa bwalo la Polisi, Osterbay jijini Dar es salaam

Watatu kuikosa Tanzania Prisons leo

Leo Alhamisi jioni Yanga itakuwa dimba la Uhuru kuikabili Tanzania Prisons katika mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara

Yanga itamkosa mlinda lango Klaus Kindoki anayetumikia adhabu ya kadi tatu za njano

Pia beki wa kushoto Gadiel Michael alipata majeraha katika mchezo uliopita dhidi ya Azam Fc anatarajiwa kukosekana pamoja na mkongwe Kelvin Yondani ambaye leo anamaliza adhabu ya kukosa michezo mitatu

Yondani atarejea kikosini kwenye mchezo wa nusu fainali kombe la FA (ASFC) dhidi ya Lipuli Fc utakaopigwa mkoani Iringa, May 06 uwanja wa Samora

Yanga kusaka alama tatu mchezo dhidi ya Prisons leo

Ligi Kuu ya Tanzania Bara inaendelea leo kwa mchezo mmoja kupigwa ambapo vinara wa ligi hiyo Yanga watakuwa uwanja wa Uhuru kuikabili Tanzania Prisons

Yanga inahitaji kushinda mchezo huo ili kuendelea kuipa ‘presha’ Simba kwenye mbio za kuwania ubingwa msimu

Aidha, itakuwa ikisaka rekodi ya kuwa timu kwanza kufikisha alama 80 msimu huu

Wapinzani wao katika mbio za upingwa Simba wao wanaelekea mkoani Mbeya ambapo kesho May 03 watacheza na Mbeya City kisha May 05 watacheza na Tanzania Prisons

Mratibu wa Yanga Hafidh Saleh amesema wachezaji wote wako katika hali nzuri, tayari kwa mchezo huo utakaopigwa kuanzia saa kumi kamili jioni

Dk Msolla azindua kampeni Yanga

Mgombea wa nafasi ya Mwenyekiti katika uchaguzi wa Yanga utakaofanyika May 05, Dk Mshindo Msolla amezindua kampeni zake leo Makao Makuu ya klabu ya Yanga, jijini Dar es salaam

Dk Msolla ambaye kitaalamu ni Mwalimu wa mpira wa miguu (kocha) aliyewahi kuinoa Taifa Stars, ametaja vipaumbele vyake ambavyo atavitekeleza kama atachaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Yanga

Baadhi ya vipaumbele hivyo ni pamoja na Kujenga umoja na ushirikiano, Kuendeleza mchakato wa mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji, Kuendeleza miradi yote ya klabu iliyopo pia kuanzisha mipya, Kuweka na kusimamia misingi ya utawala bora pia kuweka misingi ya Yanga kuwa na timu imara

Dk Msolla amesema anataka kuona ushirikiano baina ya timu na mashabiki na wanachama wake unaimarika zaidi na ameunga mkono zoezi la kuichangia Yanga linaloendeshwa

“Nataka kujenga umoja ndani ya klabu kwa maana ya kuirudisha timu kwa wanachi hivyo sio vibaya wenye timu kuichangia klabu yao”

Aidha DK Msolla amesema atabadili mfumo wa uchaguzi wa Yanga unaotoa fursa pekee kwa wanachama wa Dar es salaam kushiriki michakato ya uchaguzi

“Natambua kuwa wanachama wengi wa Yanga ambao hushiriki uchaguzi ni wale ambao wapo Dar, ndani ya uongozi wangu kama nikipewa nafasi basi wa mkoani nao watapata haki hiyo.

“Tutakuwa na mfumo ambao utawawezesha kupiga kura wakiwa kwenye matawi yao”

Kuhusu utawala bora Dk Msolla amesema uongozi wake hautaingilia majukumu ya kocha Mwinyi Zahera

Amesema kocha huyo ni mtu muhimu kwa klabu ya Yanga, ni bahati kuwa nae hasa ikizingatiwa timu inapita katika kipindi kigumu sana

“Mimi ni kocha wengi wananifahamu, akihitaji ushauri wa kiufundi nitampatia lakini nitaingia Yanga kama mwenyekiti hivyo niseme wazi kuwa nitamwacha awe huru kutekeleza majukumu yake.

“Uongozi wangu hautakuwa na mipango ya kuachana naye, mara kadhaa nimekuwa nikisema wazi kuwa Yanga tunabahati ya kupata kocha wa namna hii”

Pia Dk Msolla amesema atahakikisha Yanga inakuwa na misingi mizuri ya kuendeleza vijana wa kikosi B kwa lengo la kuja kuwatumia kikosi cha kwanza

Wagombea wa nafasi mbalimbali za uongozi Yanga wameendelea kuzindua kampeni ambazo zitadumu hadi Jumamosi, May 04 siku moja kabla ya uchaguzi

Sevilla itawajengea wachezaji uzoefu wa Kimataifa

Mafanikio ya Simba kwenye michuano ya SportPesa Super Cup msimu huu yameipelekea mabingwa hao wa Tanzania Bara kuteuliwa kuivaa Sevilla katika mchezo wa Kimataifa wa kirafiki utakaopigwa May 23 jijini Dar es salaam

Uongozi wa Simba umesema mchezo huo ni fursa adimu kwa wachezaji wake kwani utawasaidia kuwajengea uzoefu wa Kimataifa

Aidha Simba imesema itautumia mchezo huo kuitangaza Tanzania Kimataifa kwani wanajua utafuatiliwa na mamilioni ya mashabiki wa soka duniani kwani utarushwa mbashara na runinga mbalimbali kote duniani

Msemaji wa klabu ya Simba Haji Manara amesema uteuzi huo ni sahihi kwa Simba kwani ukiachilia mbali mafanikio waliyopata kwenye michuano ya SportPesa ukilinganisha na timu nyingine za Tanzania, Simba iko kwenye kiwango cha juu zaidi kwa sasa hapa nchini

“Simba kwa sasa ipo katika kiwango cha juu na kucheza na Sevilla kutasaidia kujua viwango vya wachezaji wetu katika mechi za kimataifa,” amesema

“Mechi hii inaiweka Tanzania katika historia kubwa sana katika soka. Historia zinaonyesha kuwa miaka ya nyuma, timu mbalimbali kutoka nje ya mipaka ya Afrika zilikuja hapa Tanzania na kucheza na Yanga na Simba, miaka ya hivi karibuni hakukuwa na ujio huo zaidi ya mwaka 2017 ambapo SportPesa iliileta timu ya Everton na kucheza timu ya Gor Mahia ya Kenya”

Sevilla ni moja ya timu kongwe na maarufu nchini Hispania na barani Ulaya. Imewahi kutwaa taji la Europa kwa misimu mitatu mfululizo katika kipindi cha miaka mitano iliyopita

Simba yaelekea mkoani Mbeya

Mabingwa watetezi wa ligi kuu ya Tanzania Bara, Simba wanaondoka asubuhi hii kuelekea mkoani Mbeya tayari nkwa michezo miwili ya ligi dhidi ya Mbeya City na Tanzania Prisons

Kesho Ijumaa May 03, Simba itashuka uwanja wa Sokoine kuikabili Mbeya City kisha kurejea tena katika uwanja huo May 05 kuikabili Tanzania Prisons

Ikiwa imesalia na michezo 10, Simba inahitaji kushinda michezo saba tu ili iweze kutetea ubingwa wake kwa msimu wa pili mfululizo

Hii hapa ratiba ya michezo yote iliyobaki