Simba kurudi ‘machinjioni’ baada ya AFCON U17 kumalizika

Michuano ya vijana ya AFCON U17 inayoendelea jijini Dar es salaam, inatarajiwa kumalizika April 28 2019 kwa mchezo wa fainali kupigwa ambapo baada ya mchezo huo, uwanja wa Taifa utaruhusiwa kwa matumizi ya michezo ya ligi

Hii ni taarifa njema sana kwa Simba ambayo katika kipindi cha wiki mbili zijazo inakabiliwa na michezo mingi ya viporo inayopigwa ugenini

Mwanzoni mwa mwezi wa tano Simba itarejea kumalizia michezo iliyobaki katika uwanja wa Taifa ambao umepachikwa jina la ‘machinjioni’

Msimu huu Simba imeweka rekodi ya kipekee uwanja wa Taifa kwa kushinda michezo yote iliyocheza kwenye michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika na kulazimishwa sare michezo miwili tu kwenye ligi

Simba yarejea Dar usiku kwa usiku, tayari kwa safari ya Kanda ya Ziwa

Kikosi cha Simba kimerejea jijini Dar es salaam usiku kikitokea Tanga ambapo jana kilipata ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Coastal Union

Kutokana na ukaribu wa michezo yake Simba imelazimika kusafiri usiku na mchana ili kwendana na ratiba ya viporo iliyopangwa na Bodi ya Ligi

Simba inaelekea Kanda ya Ziwa ambapo keshokutwa Jumamosi, April 20 2019 itakuwa dimba la Kaitaba kuikabili Kagera Sugar

Baada ya ushindi Tanga, Simba kurejea Dar

Baada ya ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Coastal Union leo, kikosi cha Simba kinarejea jijini Dar es salaam tayari kuifuata Kagera Sugar

Simba itacheza na Kagera Sugar Jumamosi April 20 katika mchezo utakaopigwa uwanja wa Kaitaba

Kocha Mkuu wa Simba Patrick Aussems amesema licha ya kukabiliwa na ratiba isiyo rafiki watapambana kuhakikisha wanapata matokeo

Akizungumzia matokeo ya mchezo wa leo, Aussems amewapongeza wachezaji kwa kupata ushindi licha ya mazingira yasiyo rafiki ya uwanja wa Mkwakwani

“Haikuwa rahisi sababu uwanja haukuwa mzuri lakini tulifanikiwa kumiliki mchezo na baadae tulifanya mabadiliko ambayo yametuletea magoli. Kubwa zaidi nawapongeza wachezaji kwa kuibuka na ushindi”

Simba au Yanga kuchuana na Sevilla May 23

Wadhamini wa vilabu vya Simba na Yanga kampuni ya SportPesa, imetangaza kuileta nchini Sevilla Fc inayoshiriki ligi kuu ya Hispania, La Liga

Mkurugenzi wa Utawala na Utekelezaji wa kampuni ya SportPesa Abbas Tarimba amesema Sevilla itakuja nchini May 23 kuchuana na kati ya Simba au Yanga kwenye mchezo utakaopigwa uwanja wa Taifa

SportPesa pia inadhamini ligi kuu ya Hispania, La Liga

Kagere amfikia Aiyee, afikisha mabao 16 ligi kuu

Mabao mawili aliyofunga Meddie Kagere leo, yamemuwezesha kufikisha mabao 16 na kumfikia Salim Aiyee ambaye amekuwa akiongoza kwa muda mrefu mbio za kuwania kiatu cha dhahabu

Katika kipindi cha wiki mbili hivi Kagere huenda akajiimarisha kileleni katika mbio hizo kwani Simba itacheza michezo saba ya viporo

Leo Kagere ameiongoza Simba kuondoka na ushindi muhimu wa mabao 2-1 dhidi ya Coastal Union na kuiweka Simba katika nafasi nzuri ya kutetea ubingwa hasa baada ya Yanga kukubali kipigo cha bao 1-0 kutoka kwa Mtibwa Sugar

Simba inaelekea mkoani Kagera tayari kwa mchezo mwingine wa kiporo dhidi ya Kagera Sugar ambao utapigwa Jumamosi, April 20 2019 katika dimba la Kaitaba

Simba yasaka alama tatu dhidi ya Coastal Union leo

Mabingwa watetezi ligi kuu ya Tanzania Bara Simba leo wanarejea ‘mzigoni’ kwa kuikabili Coastal Union katika mchezo utakaopigwa uwanja wa Mkwakwani, saa nane mchana

Simba iko mkoani Tanga tangu juzi ambapo jana jioni ilifanya mazoezi ya mwisho Mkwakwani kuelekea mchezo huo unaosubiriwa kwa hamu

Baada ya kuondoshwa katika hatua ya robo fainali michuano ya ligi ya mabingwa, Simba imejizatiti kutetea ubingwa iliyotwaa msimu uliopita ili kujihakikishia nafasi ya kushiriki michuano ya hiyo msimu ujao

Ikiwa imeshuka dimbani mara 22 na kuvuna alama 57, ushindi katika mchezo wa leo utaifanya Simba ifikishe alama 60 na kuendelea kuzifukuzia Azam Fc (66) na Yanga (74) ambazo hata hivyo zimecheza michezo tisa zaidi

Kocha Patrick Aussems amesema wachezaji wake wanafahamu umuhimu wa mchezo wa leo na baada ya kupoteza mchezo dhidi ya TP Mazembe, leo watakuwa na nafasi ya kufuta makosa waliyofanya kwenye mchezo huo kwa kuibuka na ushindi mnono

Mchezo utapigwa saa nane mchana ili kuwapa nafasi mashabiki kushuhudia mchezo wa michuano ya AFCON U17 kati ya Tanzania dhidi ya Uganda ambao utaanza saa kumi kamili jioni