Lwandamina Amtaka Tshishimbi ZESCO

Baadhi ya magazeti nchini Zambia yameripoti kuwa klabu ya ZESCO United itamsajili kiungo wa Yanga Papi Tshishimbi mwishoni mwa msimu.

ZESCO inanolewa na kocha wa zamani wa Yanga, George Lwandamina aliyejiunga na timu hiyo mwishoni mwa msimu uliopita.

Mkataba wa Tshishimbi wa kuitumikia Yanga unamalizika mwishoni mwa msimu huu kama Yanga itashindwa kumshawishi asaini mkataba mpya basi huenda akaenda kujiunga na timu hiyo akiwa mchezaji huru.

Alipotua Yanga msimu uliopita akitokea Mbabane Swallows, Tshishimbi alionyesha kiwango cha hali ya juu.

Hata hivyo msimu huu bado haujawa mzuri sana kwake kutokana na kukabiliwa na majeruhi ya mara kwa mara. Ameshindwa kufikia makali yake ya msimu uliopita

Mzee Akilimali Apinga MANJI Kurudi Yanga

Katibu wa Baraza la Wazee la Yanga Ibrahim Akilimali amepinga kurejea kwa Mwenyekiti wa klabu hiyo Yusufu Manji na ameitilia shaka barua inayodaiwa kuwa ameiandika kuridhia kurejea katika nafasi yake.

Akizungumza na waandishi wa habari leo, Akilimali ambaye tayari amechukua fomu ya kugombea nafasi ya Uwenyekiti ameitaka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) iichunguze barua hiyo iliyosomwa na Mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini Kapteni George Mkuchika.

Aidha Akilimali amedai kushangazwa na viongozi wa Yanga kuendelea kumsemea Manji wakati yeye mwenyewe yupo.

Akilimali amemtaka Manji ajitokeze hadharani kuwaambia WanaYanga kama amerejea au la na sio kusemewa na watu wengine kila siku.

Katika hatua nyingine, Mwenyekiti kamati ya Uchaguzi ya TFF Malange Mchungahela amewataka viongozi wa Baraza la Wadhamini Yanga pamoja na wajumbe Kamati ya Utendaji wajieleze kwanini wasichukuliwe hatua kutokana na kutaka kuvuruga mchakato wa Uchaguzi wa klabu hiyo.

Mchungahela amesisitiza kuwa zoezi la utolewaji wa fomu kwa ajili ya nafasi zote za uchaguzi zilizotangazwa (ikiwemo ya Mwenyekiti) linaendekea na litafikia tamati 14/11/2018.

Amesema wale wanaomtaka Manji arejee Yanga basi ni vyema wakaenda kumchukulia fomu

Rasmi: Yusuf MANJI Arejea Yanga Sc

Mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini wa Yanga Kapteni George Mkuchika amesema Yussuf Manji amerejea katika nafasi yake baada ya kumuandikia burua ya kukubali ombi la Wanachama wa klabu hiyo kumtaka atengue uamuzi wake wa kujiuzulu

Akizungumza na waandishi wa habari leo baada ya kikao kilichoitishwa na Baraza hilo, Kapteni Mkuchika ameonyesha barua iliyoandikwa na Manji kuridhia kurejea katika nafasi ya Uwenyekiti wa Yanga.

Kapteni Mkuchika amesema Manji aliandika barua ya kujiuzulu lakini wanachama walilikataa ombi lake kupitia Mkutano halali wa klabu hiyo na kumuomba arejee katika nafasi yake.

Barua hiyo aliyoandika ni uthibitisho kuwa ameridhia maombi ya wanachama wa Yanga na sasa ni rasmi amerejea katika nafasi yake.

Kapteni Mkuchika amesema Manji ndio Mwenyekiti wa Yanga huku Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Thobas Langalanga aliyekuwa ameteuliwa kukaimu wadhifa huo hatambuliki

TFF yawatahadharisha Wanaopanga kuvuruga mchakato wa UCHAGUZI Yanga

Mwenyekiti Kamati ya Uchaguzi ya TFF Malangwe Ally Mchungahela amesema wanazo taarifa kuwa kuna wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya Yanga kwa kushirikiana na baadhi ya Wanachama wamepanga kuitisha Mkutano kesho Jumapili kutangaza kumtambua Yusufu Manji kuwa Mwenyekiti halali wa Yanga na kupinga uchaguzi wa kujaza nafasi yake.

TFF imewatahadharisha wote wanaopanga ajenda hiyo na kusisitiza kuwa mchakato wa uchaguzi kwa nafasi zote zilizotangazwa utaendelea kama ulivyopangwa.

Mchungahela amesema wote wanatakaoshiriki katika ajenda hiyo watachukuliwa hatua za kinidhamu na TFF bila ya kujali nafasi zao

Aidha, kutokana na kuchelewa kwa zoezi la utolewaji wa fomu, zoezi hilo sasa litafikia tamati Jumatano Novemba 14 baada ya TFF kuongeza siku moja

CHIRWA: Sina Kinyongo na ZAHERA

Baada ya kutua Azam Fc mshambuliaji wa zamani wa Yanga Obrey Chirwa amesema hana kinyongo na kocha wa timu hiyo Mwinyi Zahera aliyemuwekea ngumu kurejea Jangwani.

“Kocha alisema mimi simtaki Chirwa sababu ana tabia ya kugoma. Ni kweli mimi niko hivyo hivyo na siwezi kubadilika,” Chirwa aliwaambia waandishi wa habari jana baada ya kutambulishwa na Azam Fc.

“Mpira ni kazi yangu, kama silipwi stahiki zangu lazima nidai kwa njia yoyote. Na kama nikishindwa nitavunja mkataba”

“Sina tatizo na kocha wala klabu ya Yanga, ninamtakia kila la kheri aweze kuipa mafanikio Young Africans,” amesema

Katika hatua nyingine Chirwa ameeleza kushangazwa na wachezaji wengi hapa nchini kutokana na kushindwa kuwa na misimamo jambo ambalo linawafanya waendelee kuzipigania timu zao bila kulipwa chochote.

“Unajua wachezaji wengi hapa nchini wamekosa msimamo wa kulinda mikataba yao, niko tayari kuvunja mkataba wangu na kwenda mahala pengine ninapoona stahiki zangu hazilipwi kwasababu nina familia na inanitegemea” alisema.

Nafasi ya MANJI kujazwa January 13 2019

Kamati ya uchaguzi ya Shirikisho la soka nchini (TFF) ambayo ilipewa jukumu na BMT ya kusimamia mchakato wa uchaguzi wa kujaza nafasi zilizowazi katika klabu ya Yanga, imetangza rasmi kuanza kwa zoezi hilo.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo Ally Mchungahela amesema zoezi la kutolewa fomu kwa wagombea wa nafasi hizo ikiwemo ya Mwenyekiti wa Yanga litaanza rasmi Alhamisi, Novemba 08, 2018

Aidha, Mchungahela ametangaza tarehe ya uchaguzi kuwa ni Januari 13 2019.

Wakati TFF ikitangaza hayo, hali si shwari upande wa klabu ya Yanga ambayo kupitia viongozi wa Matawi wa klabu hiyo, wametangaza kupinga uchaguzi wa timu hiyo kusimamiwa na TFF.

BMT iliipa Kamati ya uchaguzi ya TFF jukumu la kusimamia uchaguzi huo baada ya kubaini Kamati ya uchaguzi ya Yanga ina mapungufu.

Wanachama hao pia walipinga uchaguzi wa nafasi ya Mwenyekiti wakiutaka uongozi wa klabu hiyo kwanza uwahakikishie kama kweli Mwenyekiti wao Yusufu Manji amekataa kurejea katika nafasi yake.

Nafasi zinazotarajiwa kujazwa kwenye uchaguzi huo ni Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na nafasi nne za wajumbe wa Kamati ya Utendaj

YANGA: Kumsajili Kiungo Huyu

Dirisha dogo la usajili linafunguliwa Novemba 15, ni wazi kwamba kila timu sasa inahaha kuhakikisha inaziba mapengo ambayo yamejitokeza katika Ligi Kuu inayoendelea.
Yanga nayo haichezi mbali, inasaka wakali ambao wanaweza kuwapaisha na kutikisa katika ligi ikiwa ni pamoja na kukata tiketi ya kushiriki michuano ya kimataifa.
Yanga waliibuka na straika Heritier Makambo katika dirisha la usajili lililopita, lakini wamegundua kwamba mchezaji huyo hajafikia kiwango thabiti walichokuwa wakikihitaji na sasa wameamua kumtafuta winga wa kumlisha raia huyo wa DR Congo.
Wanajangwani hao wamefanikiwa kumshawishi winga Ruben Bomba raia wa DR Congo, ambaye tayari ameshakubali kutua katika klabu hiyo.
Juzi kati Kocha wa Yanga Mwinyi Zahera aliweka wazi kwamba anataka kuletewa winga mmoja matata atakayekuwa na kazi ya kuwalisha washambuliaji, ni wazi karibia azma yake itatimia.
Pia juzi Jumapili mara baada ya mechi dhidi ya Ndanda ambayo walitoka sare ya 1-1, kocha Zahera alisema kuwa kupungua makali kwa Makambo kunatokana na kutolishwa mipira ipasavyo huku wachezaji wa wake wa pembeni wakishindwa kuwa na muendelezo mzuri wa viwango vyao.
Zahera alisema nyota wake wawili Deus Kaseke na mkongwe Mrisho Ngassa bado hawajaweza kufanya anachokitaka na kuwa ndiyo maana ametaka kusajiliwa kwa mtu muafaka angalau mmoja kutoka katika eneo hilo.
“Kaseke hayuko kwenye kiwango cha juu sana kwasasa lakini Makambo naye amekuwa akikosa mabao kirahisi huku wakati mwingine hapewi mipira sahihi,”alisema Zahera.
“Ndiyo maana nataka mtu wa kuongeza nguvu tunayoitaka katika safu yetu ya ushambuliaji, ngoja tuone kipi tutafanya muda wa kusajili ukifika.”
Bomba, ndiye chaguo la kwanza la Zahera na tayari mabosi wa usajili chini ya Mwenyekiti Hussein Nyika walishaanza kazi ya kuhakikisha anatua nchini.
Taarifa kutoka ndani ya kamati inasema kwamba Bomba ameshakubali kutua Yanga ambapo raia huyo wa DR Congo anataka kuungana na Zahera ambaye pia ni Kocha Msaidizi wa timu ya taifa ya DR Congo.
“Tumeshafanya naye mazungumzo kilichokuwa kinahitajika ni utulivu ndani ya klabu yetu,”alisema bosi huyo.
“Huyu Bomba (Ruben) ni winga mzuri, tumeona kasi yake uwanjani. Akifika hapa mashabiki watakubali ninayosema.”

ZAHERA: Akerwa na Ubutu wa Safu ya Ushambuliaji YANGA

Kocha Mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera amekerwa na ubutu wa safu yake ya ushambuliaji baada ya timu yake kulazimishwa sare ya bao 1-1 na Ndanda Fc kwenye mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara uliopigwa jana usiku.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya mchezo ya mchezo jana, Zahera alisema timu yake ingeweza kuondoka na ushindi mnono kama wangetumia vyema nafasi walizotengeneza.

“Jana tulicheza sana mpira tofauti na michezo mingine. Tulitengeneza nafasi nyingi sana ambazo hatukuzitumia,”amesema

Zahera amemshukia mshambuliaji Heritier Makambo aliyekosa nafasi kadhaa za wazi

“Kila mechi tunatengeneza nafasi nyingi lakini washambuliaji hawafungi. Mfano goli la kichwa alilokosa Makambo hata Mama yangu angeweza kufunga,” alisema aliyeonekana kukerwa na hali hiyo.