Licha ya kuwakosa wachezaji saba wanaougua Malaria, kocha Mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera amewapongeza wachezaji wa timu hiyo kwa kufanikiwa kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Mbeya City
Zahera amesema katika mchezo wa leo alitumia wachezaji wanne kutoka katika kikosi cha U20
“Tulikosa wachezaji wetu saba wanaumwa Malaria, nimetumia vijana wanne wa U20, nafurahi wachezaji wameweza kutupatia matokeo,” amesema
“Tulitengeneza nafasi nyingi, tulipaswa kufunga mabao zaidi, nafikiri leo hatukuwa na nidhamu ya mchezo”
Kuhusu maoni yake baada ya Simba kutwaa ubingwa jana, Zahera ameshikilia msimamo wake kuwa hawakustahili kutwaa ubingwa kutokana na upindishwaji mkubwa wa sheria uliofanywa kuwawezesha washinde taji hilo
“Simba waliwapa ubingwa jana, maoni yangu mie nilicheza mpira ambao uko na sheria, ule sio ubingwa,” amesema
“Ninapoishi nakaa na watu wa Simba, wananiambia kweli hata kama mpira wetu tunapenda Simba, tunaona kama sio hivyo”
“Tunapata kikombe lakini ukiangalia sheria kabisa mwaka huu hatungepata kikombe”
Wadau mbalimbali wametoa maoni tofauti juu ya ubingwa wa Simba
Wakati wengine wakiamini kuwa Simba ilistahili ubingwa huo, wapo wanaoamini mazingira yaliyotengenezwa na TFF kwa kuiacha timu hiyo isicheze mpaka michezo 12 wakati nyingine zikiendelea na ligi, yameirahisishia timu hiyo kutwaa ubingwa
“Simba walikuwa na michezo 12 ya viporo. Walikuwa wanafahamu matokeo ambayo wanatakiwa wapate ili watwae ubingwa, pengine hali ingekuwa tofauti kama wangecheza sambamba na timu nyingine,” amesema Rajabu Issa kutoka Buguruni
“Umeona wapi na ligi gani duniani ambapo timu moja inakuwa na michezo ya viporo 12? kushiriki ligi ya mabingwa haitoshi kuwa sababu ya kurundikiwa michezo mingi kiasi hicho mbona timu walizokuwa wakishindana nazo zilikuwa zikicheza ligi zao?”
“Hawa Simba baada ya kutolewa kombe la FA walipanga mkakati na TFF kuhakikisha wanatwaa ubingwa wa ligi kuu kupitia ratiba na hujuma kwa Yanga”
“Angalia mchezo dhidi ya KMC ilikuwa wafungwe lakini refa akawatafutia ushindi kwa nguvu halafu baadae TFF wanatangaza kumfungia mwamuzi wakati mpango umeshakamilishwa”