Yanga yatenga Bilioni Mbili kwa ajili ya usajili

Uongozi wa Yanga umetenga kati ya Tsh Bilioni 1.5 hadi Bilioni mbili kwa ajili ya usajili wa msimu ujao

Katika Mkutano na Waandishi wa Habari uliofanyika Makao Makuu ya Yanga jijini Dar es salaam leo, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Hamasa Lucas Mashauri amesema walikutana na kocha Mwinyi Zahera ambapo aliwapa mchanganuo wa mahitaji yake kwa ajili ya usajili

“Bajeti ya usajili mara nyingi inatolewa baada ya kukamisha zoezi la usajili”

“Lakini kwa sasa tunakuwa na makisio ya Bajeti tunayohitaji ambapo Kamati yetu ilipewa kazi ya kutafuta kati Bilioni 1.5 na Bilioni mbili,” amesema

“lengo letu kubwa ni kuwa na Yanga imara msimu ujao. Kazi tumemuachia kocha Mwinyi Zahera ili atuambie wachezaji anaowahitaji”

“Bajeti halisi itafahamika baada ya kocha kujadiliana na wachezaji anaotaka waje”

“Lakini tumemuhakikishia, hakuna mchezaji ambaye atamuhitaji tutashindwa kumsajili. Awe Tanzania, nje ya Tanzania hata Ulaya akipatikana mchezaji tutamsajili. Yanga imeshawahi kusajili wachezaji kutoka Ulaya”

“Kamati yetu inaendelea na zoezi la kutafuta fedha ili tuweze kutimiza lengo la kusajili timu bora kadiri kocha atavyopendekeza”

Katika hatua nyingine, Mashauri amewataka Wanayanga waendelee kuichangia timu yao waepuke upotoshaji unaosambazwa kwenye mitandao ya kijamii

“Tunawataka wapenzi, wanachama na mashabiki wetu waendelee kuichangia timu wasipotoshwe na taarifa zinazosambazwa kwenye mitandao”

“Taarifa nyingi zinazosambazwa kuwa tumepokea Bilioni mbili hazina ukweli wowote. Wanaoanzisha taarifa hizo wana lengo la kupunguza kasi ya kuichangia timu yetu”

“Yanga ni timu ya Wananchi na safari hii tumeamua kuisimamia sisi wenyewe. Na kama alivyosema Mwenyekiti, zoezi hili la uchangiaji litandelea kwa kuwa ni wajibu kwa kila Mwanchama wa Yanga kuichangia timu kila mwezi Tsh 1000/- ambayo ni ada ya uanachama”

Azam yanyemelea nyota Simba

Wakati klabu ya Simba ikiwa ‘busy’ kuhakikisha inatetea ubingwa wake, baadhi ya nyota wake ambao mikataba yao imemalizika, wameingia kwenye rada za Azam Fc

Aishi Manula, Shomari Kapombe, Erasto Nyoni na John Bocco waliotua Simba kutoka Azam Fc misimu miwili iliyopita, wanatajwa kuwaniwa tena na timu hiyo

Baada ya kuachana na mpango wa kubana matumizi, Azam Fc imepanga kufanya usajili mkubwa ili kuwa washindani wa kweli katika kuwania ubingwa wa ligi kuu msimu ujao

Inaelezwa uongozi wa Simba umepanga kuanza michakato ya usajili baada ya kukamilisha mpango wa kutetea ubingwa

Zaidi ya nyota 10 wa kikosi cha Simba mikataba yao inamalizika mwishoni mwa msimu

Tiketi Mechi dhidi ya Sevilla zimeanza kuuzwa

Tiketi kwa ajili ya kuushuhudia mchezo wa Kimataifa wa Kirafiki kati ya Simba dhidi ya Sevilla tayari zimeanza kuuzwa kupitia Selcom

Kiingilio cha chini cha mchezo huo utakaopigwa May 23 saa moja jioni, Mzunguuko ni Tsh 5,000/- wakati majukwaa ya VIP ni Tsh 15,000/-

Pia kutakuwa na tiketi za Platinumambazo zitapatikana kwa Tsh 100,000/-, kwa wanaohitaji tiketi hizi wawasilane na 0745346687

Mchezo huu wa Kimataifa utakuwa wa kihistoria, sio wa kukosa!

SIMBA WASHUSHA MAJEMBE MAPYA

MABOSI wa Simba kwa msimu ujao hawataki mchezo kwani wamedhamiria kukisuka hasa kikosi chao kiwe cha ushindani na kwa kuanza hivi karibuni watazishusha sura mpya nne za kigeni, akiwemo mshambuliaji Mzambia, Lazarus Kambole.
Mabosi wa Simba wanataka kukiboresha kikosi chao kwa kuleta wachezaji wenye viwango vikubwa kutokana na aina ya matokeo ambayo walikuwa wanayapata kwenye michezo ya Ligi ya Mabingwa Afrika ya ugenini kwa msimu huu.
Chanzo kutoka Simba kimeliambia Championi Jumatatu, kuwa wachezaji hao wane wanatarajiwa kuingia nchini hivi karibuni ambapo wanaweza kuwemo kwenye mechi ya kirafiki ya kimataifa kati ya Simba na Sevilla ya Hispania.

“Viongozi wanataka kuboresha kikosi kiwe na uwezo wa hali ya juu kwenye michezo ya kimataifa kuliko msimu huu, ndiyo maana viongozi wanaleta wachezaji wenye uwezo wa hali ya juu kuliko ambao wapo kwa sasa.

“Wachezaji hao wanaweza kuwepo hapa nchini kwenye mechi na Sevilla kwa ajili ya kuangaliwa na kuongea na viongozi kabla ya kusaini mikataba kwa msimu ujao.
“Huyo Kambole unayesema anaweza kuwemo katika orodha hiyo, lakini ni suala la kusubiri kuona kama ni yeye ambaye atakuja hapa ama la,” kilisema chanzo hicho.

Katibu wa Simba, Anord Kashembe amesema: “Huu siyo wakati wa kufanya usajili, hatuwezi kulizungumzia hilo, ukifika muda wake kila kitu kitakuwa sawa.”

Chanzo: championi & gpl

TETESI ZA USAJILI YANGA: Kifaa kipya Yanga hiki hapa, ni hatari tupu, kutua nchini mwezi ujao

Kwa mujibu wa mtandao wa michezo wa ‘Kawowo Sports’ kutoka nchini Uganda umeripoti kuwa mshambauliaji wa zamani wa klabu ya Onduparaka FC, Agau Rashid ambaye kwa sasa anaichezea timu ya Maroons FC anatarajiwa kuwasili Tanzania mwezi Juni kwa ajili ya majaribio katika miamba ya soka ya ligi kuu Young Africans SC.
Rashid ni mzuri wa kumiliki mipira na mfumaniaji mzuri wa mabao

Kwa mujibu wa wakala wa mchezaji huyo, amesema kuwa Agau amepata mualiko kwaajili ya kwenda kufanya majaribio kufuatia kufanya vizuri zaidi msimu huu.
Nyota huyo wazamani wa Onduparaka, amejiunga na Maroons msimu wa mwaka 2018/19 akiwa kama mchezaji huru kwa mkataba wa miaka mitatu hata hivyo kama atajiunga na Yanga atakuwa amewatumikia waajiri wake hao mwaka mmoja pekee.

Ndani ya msimu huu mmoja, Agau Rashid amefanikiwa kufunga jumla ya mabao saba na kuwaacha mbali baadhi ya wachezaji wenzake kama Pius Obuya na Seif Batte wenye mabao manne kila mmoja ikiwa pamoja na Isaac Otto, Bronson Nsubuga waliyosajiliwa msimu huu mwezi Januari wakiwa na mabao matatu.

Klabu ya Maroons imetoa baraka zote kwa, Agau endapo atafanikiwa kufuzu majaribio yake ndani ya Yanga, hata hivyo kama atafanikuwa atajiunga na baadhi ya Waganda wenzake kama Emmanuel Arnold Okwi na Murushid Jjuuko wanaotumikia klabu ya Simba.

Zahera ataja sababu ya Ngasa kukosekana mchezo dhidi ya Ruvu Shooting

Kocha Mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera amesema winga Mrisho Ngasa hakuweza kucheza jana mchezo dhidi ya Ruvu Shooting baada ya kuugua ghafla

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya mchezo, Zahera alisema Daktari wa timu Dk Bavu alishauri mchezaji huyo asitumike kwenye mchezo huo hivyo kuamua kumtumia Paulo Godfrey ‘Boxer’ wingi ya kulia

“Ngasa alipata matatizo muda mfupi baada ya kuwa tumepata kifungua kinywa. Alianza kutapika mfululizo na baada ya kupatiwa huduma na Daktari wa timu Dk Bavu, alishauri asicheze,” alisema Zahera

Akizungumzia mchezo huo ambao Yanga iliibuka na ushindi wa bao 1-0, Zahera aliwapongeza wachezaji wake kwa ushindi huo huku akifichua hawakuwa wamefanya mazoezi tangu walipocheza na Biashara United May 10

“Tulipata changamoto ya usafiri kutoka Mwanza hali iliyopelekea tuchelewe kurudi jijini Dar es salaam kujiandaa na mchezo. Hata baada ya kurudi tulilazimika kuwapa wachezaji mapumziko kwani walikuwa wamechoka”

“Nilifahamu mchezo wa leo (jana) hautakuwa mwepesi kwetu, lakini nimefurahi tumeweza kutumia moja ya nafasi tulizotengeneza ingawa tulikuwa na uwezo wa kufunga mabao zaidi kwenye kipindi cha kwanza”

TFF yafafanua kutoikabidhi Simba ubingwa mchezo dhidi ya Sevilla

Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), limeamua kumuondoa wasiwasi kocha wa Yanga, Mwinyi Zahera ambaye alikerwa na maneno ya msemaji wa Simba Haji Manara kwamba ubingwa watakabidhiwi wakati wa mechi yao na Sevilla inayoshiriki Ligi Kuu nchini Hispania (La Liga).

Kupitia msemaji wa TFF, Clifford Marion Ndimbo aliliweka sawa jambo hilo kwamba hakuna kanuni ya shirikisho inayoruhusu bingwa akabidhiwa kombe nje na mechi ya Ligi Kuu Bara.

“TFF ina kanuni zake hata Simba wakiandika barua kama alivyosema msemaji wao Manara kwamba endapo wangeshinda mechi zao wakabidhiwe taji la ubingwa kwenye mechi yao na Sevilla hakuna kitu kama hicho na hakitafanyika.

“Kama Zahera ana wasiwasi na hilo basi ajue kabisa kwamba TFF ina kanuni zake hata wakiandika barua hiyo, majibu yao ni rahisi kuwa kanuni haziruhusu mambo hayo”anasema.

Kuna video inayomuonyesha Zahera kwamba Simba watakabidhiwa ubingwa wakati sio mabingwa baada ya kusikia kauli ya msemaji wa Simba, Manara kuwa wataiomba TFF wawakabidhi kombe wakati wa mchezo wao na Sevilla.

Mwanaspoti

Mechi tano za kumaliza msimu Simba

Licha ya kutopata ushindi kwenye michezo miwili iliyopita, hesabu za ubingwa kwa Simba bado ziko salama ikihitaji kushinda angalau michezo mitatu kati ya mitano iliyobaki

Ratiba ya mechi zilizobaki za Wekundu hao wa Msimbazi inaonyesha keshokutwa May 16 watakuwa uwanja wa Uhuru kuikabli Mtibwa Sugar kisha kurejea tena uwanjani hapo May 19 kucheza na Ndanda Fc

May 21 Simba itasafiri kwenda mkoani Singida kuikabili Singida United kisha kurejea jijini Dar es salaam kucheza mchezo wa Kimataifa wa kirafiki dhidi ya Sevilla May 23

May 25 itarudi uwanja wa Uhuru kuikabili Biashara United na itamaliza msimu mkoani Morogoro kwa kuikabili Mtibwa Sugar May 28