Yanga kuikabili Lipuli Fc ikiwa na mzuka wa kutosha

Yanga iko mkoani Iringa ambapo leo jioni itashuka uwanja wa Samora kuikabili Lipuli Fc katika mchezo wa nusu fainali kombe la FA (ASFC)

Habari njema kwa wachezaji wa Yanga ni kuwa leo watashuka dimbani wakiwa na sapoti ya viongozi wao wapya waliopatikana baada ya uchaguzi jana

Makamu Mwenyekiti Fredrick Mwakalebela anatarajiwa kuwepo uwanjani leo kuwaunga mkono wachezaji kuhakikisha wanashinda mchezo huo

Jana baada ya zoezi la uchaguzi kumalizika, Mwakalebela alisema ataondoka jijini Dar es salaam usiku huo kuwahi mchezo

“Mimi na wenzangu wachache tunaondoka usiku huu kuelekea Iringa kwenda kuwaunga mkono wachezaji wetu. Tunahitaji kushinda mchezo dhidi ya Lipuli ili tuingie fainali”

“Lengo letu ni kushiriki michuano ya kimataifa msimu ujao, tunahitaji kutwaa kombe la FA”

Aidha fedha taslim zaidi ya Mil 20 zilichangishwa na Wanachama wa Yanga jana ili kuipa motisha timu kuelekea mchezo huo

Yanga inahitaji kukomaa na kombe la FA ili kujihakikishia nafasi ya kushiriki michuano ya CAF msimu ujao

Simba mwendo mdundo, ubingwa huoooo

Ni suala la muda tu kabla ya mabingwa wa nchi, Simba kutangazwa tena kuwa wameuhifadhi ubingwa wao kwa msimu wa pili mfululizo baada ya ushindi wa leo wa bao 1-0 dhidi ya Tanzania Prisons

Simba imejiweka katika mazingira mzuri ya kutetea ubingwa wake baada ya kuondoka na alama zote sita mkoani Mbeya

Mbeya City na Tanzania Prisons zilikuwa zikiangaliwa kuwa na uwezo wa ‘kuitibulia’ Simba hesabu zake kuelekea ubingwa

Simba imesalia na michezo nane, michezo sita itapigwa jijini Dar es salaam kunako uwanja wa Taifa au Uhuru

Simba itatoka nje ya jiji kuzifuata Singida United na Mtibwa Sugar (mchezo wa pili) wakati Coastal Union, Kagera Sugar, Azam Fc, Mtibwa Sugar(mchezo wa kwanza), Ndanda na Biashara United zote zitaifuata Simba ‘majinjioni’ uwanja wa Taifa

Simba huenda ikarejea rasmi kileleni mwa msimamo wa ligi Jumatano May 08 itakapocheza na Coastal Union mchezo utakaopigwa uwanja wa Taifa/Uhuru

FT : Prisons 0-1 Simba

Simba imeendelea kuukaribia ubingwa wa pili mfululizo baada ya leo kuichapa Tanzania Prisons bao 1-0 katika mchezo uliopigwa uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya

Bao pekee la Simba lilipatikana kwenye kipindi cha kwanza likiwekwa kambani na Emmanuel Okwi katika dakika ya 11 baada ya shambulizi la kushitukiza

Ushindi huo umeendelea kuisogeza Simba kileleni baada ya kufikisha alama 78 sasa ikihitaji alama mbili tu kuweza kuifikia Yanga

Yanga ina alama 80 ikiwa imecheza michezo minne zaidi ya Simba pia

Okwi ameendelea kuwasogelea vinara wa mabao leo akifikisha mabao 11

Mchezo unaofuata ni dhidi ya Coastal Union na utapigwa May 08 kwenye uwanja wa Taifa

Mashabiki Mbeya kama kawaida uwanja wa Sokoine leo

Simba leo iko ugenini mkoani Mbeya ikiikabili Tanzania Prisons katika mchezo wa pili utakaopigwa uwanja wa Sokoine katika kipinci cha siku tatu

Lakini asikwambie mtu, mzuka wa mashabiki wa timu hiyo mkoani Mbeya, unawafanya mabingwa hao wa Tanzania Bara kutojihisi kabisa kama wako ugenini

Katika mchezo dhidi ya Mbeya City ambao Simba iliibuka na ushindi wa mabao 2-1, mashabiki wa ‘Mnyama’ walifunika dimba la Sokoine.

Leo tena wameahidi kuwa sambamba na timu yao kuhakikisha alama zote tatu zinakwenda Msimbazi

Mchezo unatarajiwa kuanza saa kumi kamili jioni na tayari mashabiki wameanza kujisogeza uwanja wa Sokoine

Simba yasaka alama nyingine tatu Mbeya

Baada ya ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Mbeya City juzi, leo Simba inarejea tena uwanja wa Sokoine kuikabili Tanzania Prisons

Mchezo ambayo kama Simba itaibuka na ushindi, itasogea zaidi kileleni mwa msimamo wa kwani itabakisha alama mbili tu kuifikia Yanga

Meneja wa Simba Patrick Rweyemamu amesema wachezaji wa timu yake wako katika hali nzuri, wamejiandaa vyema kuweza kupata alama nyingine tatu leo

Tanzania Prisons ilitua mkoani Mbeya juzi ikitokea Dar es salaam ambako ilifungwa na Yanga mabao 2-1

Kocha Mkuu wa timu hiyo Adolph Richard amesema wanatarajia mchezo hautakuwa mwepesi lakini wamepania kupata matokeo ili kujiweka salama na hatari ya kuteremka daraja

Baada ya mchezo huo Simba itarejea jijini Dar es salaam ambako itakuwa na nafasi ya kutwaa ubingwa katika michezo sita itakayocheza uwanja wa Taifa/Uhuru