Okwi, Kagere waweka rekodi ya ‘hat-trik’ ligi kuu

Washambuliaji Emmanuel Okwi na Meddie Kagere wameweka rekodi ya kufunga hat-trik mbili kwenye mchezo mmoja wa ligi kuu

Washambuliaji hao hatari wa Simba wamefunga mabao matatu kila mmoja katika mchezo dhidi ya Coastal Union uliomalizika kwa Simba kuibuka na ushindi wa mabao 8-1

Mwamuzi wa mchezo huo Jonesia Rikiyaa aliwakabidhi mpira kila mmoja baada ya mchezo kumalizika

Hizo zilikuwa hat-trik za sita kufungwa kwenye ligi msimu huu

Kagere amefikisha mabao 20 na kujiimarisha kileleni katika mbio za kuwania kiatu cha dhahabu akiwaacha Heritier Makambo na Salim Aiyee wakibaki na mabao 16

Okwi mfungaji bora wa ligi msimu uliopita, amerejea katika mbio za kuwania kiatu hicho baada ya leo kufikisha mabao 14 akimfikisha mshambuliaji mwingine wa Simba John Bocco

Kagere, Okwi na Bocco wameifungia Simba mabao 48 kwa pamoja

FT : Simba 8-1 Coastal Union

Mabingwa watetezi ligi kuu ya Tanzania Bara Simba wamerejea kileleni mwa msimamo wa ligi kibabe baada ya kuifumua Coastal Union mabao 8-1 kwenye mchezo uliopigwa uwanja wa Uhuru

Leo ilikuwa siku ya sherehe ya mabao kwa washambuliaji wawili wa Simba Emmanuel Okwi na Meddie Kagere ambao wamefunga ‘hat-trik’ kila mmoja

Alianza Okwi kupiga hat-trik kabla ya Kagere kupata ya kwake kwenye kipindi cha pili

Mabao mengine mawili yalifungwa na viungo Hassani Dilunga na Clatous Chama aliyefunga bao lake kwenye dakika za majeruhi

Kagere amejichimbia kileleni katika mbio za kuwania kiatu cha dhahabu akiwa amefikisha mabao 201 wakati Okwi amemfikia John Bocco baada ya kufikisha mabao 14

Simba ni kama imezianza sherehe za ubingwa leo na itahitaji kushinda michezo minne tu ili kutawazwa mabingwa kwa msimu wa pili mfululizo

Tumetolewa FA, tutaendelea kupambana kwenye ligi – Zahera

Kocha Mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera amesema baada ya kupoteza mchezo wa nusu fainali kombe la FA kwa kufungwa mabao 2-0 na Lipuli Fc leo, wanahamishia nguvu zao kwenye ligi kuhakikisha wanashinda michezo minne iliyobaki

Zahera amesema licha ya kutofanikiwa kutinga fainali, msimu huu wamevuka malengo na matarajio ya awali

“Hakuna kitu kitabadilika juu ya mipango yetu, tunahitaji kushinda mechi nne zilizobakia ligi kuu,” amesema Zahera

“Ukiangalia mpaka hapa tumefanikiwa kuliko matarajio. Mwaka huu tulianza ligi tukiomba mungu atusaidie japo tumalize nafasi ya sita au ya saba”

“Tulipaswa kumaliza nafasi ya sita au saba kutokana na changamoto tulizopitia msimu huu. Tulikubaliana tufanye nguvu tusimalize chini ya nafasi ya kumi”

“Mkiangalia tunaongoza ligi tokea mwanzo wa msimu mpaka leo. Malengo ya kutwaa ubingwa wa ligi na hata kombe la FA yalikuja baada ya kuona tumeweza kufanya vizuri licha ya changamoto zilizokuwa zinatukabili”

“Kazi waliyofanya wachezaji wangu ni nzuri sana. Tutaendelea kupambana kwenye ligi ili tuweze kushinda michezo yote minne iliyobaki”

Aidha akizungumzia mabadiliko aliyofanya kwenye kipindi cha pili amesema ilikuwa ni kazima kuwatoa Ajib na Mohammed Issa na kuwaingiza Tambwe na Juma Abdul ili kwendana na aina ya uchezaji wa Lipuli Fc

“Lipuli walikuwa wengi katikati hivyo nililazimika kumuingiza Tambwe na Abdul ili kutumia mipira ya krosi kupitia pembeni kujaribu kusaka mabao ya kusawazisha”

“Mfumo huo ulitusaidia kwani tulipata karibu nafasi tatu za kuweza kufunga lakini tulikosa bahati”

Aussems afichua usajili atakaofanya

Kocha Mkuu wa Simba Patrick Aussems amesema atakiongezea nguvu kikosi chake mwishoni mwa msimu kwa kusajili wachezaji wanne

Simba inayoelekea kutetea taji lake la ligi kuu kwa msimu wa pili mfululizo, inatarajiwa kurejea jijini Dar es salaam leo wakitokea mkoani Mbeya ambako wameshinda michezo yote miwili dhidi ya Mbeya City na Tanzania Prisons

Akizungumza baada ya mchezo jana, Aussems amesema ushindi wa bao 1-0 waliopata dhidi ya Tanzania Prisons umewaweka katika nafasi nzuri zaidi ya kutetea ubingwa na kujihakikishia nafasi ya kushiriki michuano ya ligi ya mabingwa msimu ujao

Amesema atakiboresha kikosi chake ili wafike mbali zaidi ya mafanikio waliyopata kwenye michuano hiyo msimu huu

Aussems ametaja maeneo ambayo atayaboresha kwa kusajili wachezaji wapya ni eneo la ulinzi (mabeki wawili), kiungo mmoja na mshambuliaji mmoja

Aidha, Aussems amesema timu yake inakabiliwa na changamoto ya kufanya vizuri Kimataifa kutokana na ukweli kuwa haipati ushindani mkubwa kutoka timu za ndani

Kagera Sugar yawahi Dar, Simba kurejea leo kutoka Mbeya

Kagera Sugar ndio timu pekee iliyopata ushindi dhidi ya Simba katika michezo minne ya kanda ya ziwa waliyocheza mabingwa hao watetezi kwenye duru ya pili

Kagera Sugar inayonolewa na kocha Mecky Mexime tayari kimewasili jijini Dar es salaam kusubiri mchezo dhidi ya Simba utakaopigwa Ijumaa, May 10

Simba wao watarejea jijini Dar es salaam leo wakitokea mkoani Mbeya ambako walifanikiwa kuchukua alama zote sita dhidi ya Mbeya City na Tanzania Prisons

Hata hivyo kabla ya kucheza na Kagera Sugar Ijumaa, siku ya Jumatano Simba itachuana na Coastal Union katika mchezo utakaopigwa uwanja wa Taifa/Uhuru

Simba inahitaji kushinda michezo mitano tu kuweza kutetea ubingwa wake bila ya kujali matokeo ya Yanga ambayo imebakiwa na michezo minne ambayo kama wakishinda yote watafikisha alama 92

Ushindi katika michezo mitano utaifanya Simba ifikishe alama 93

TFF yapongeza uongozi mpya Yanga

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Wallace Karia amewapongeza Viongozi wapya wa Klabu ya Young Africans kwa kuchaguliwa kuiongoza klabu hiyo kwa kipindi cha miaka minne (4)

Karia amesema TFF itashirikiana na Viongozi hao katika maendeleo ya Mpira wa Miguu nchini

Wanachama wa Yanga jana walikamilisha salama mchakato wa uchaguzi wa klabu hiyo kwa kuwachagua Dk Mbette Mshindo Msolla kuwa Mwenyekiti na Fredrick Mwakalebela kuwa Makamu Mwenyekiti pamoja na kuchaguliwa kwa wajumbe wengine nane wa Kamati ya Utendaji

Mchezo wa Lipuli vs Yanga kuanza saa tisa na nusu

TAARIFA

Mchezo wa Nusu fainali ya ASFC uwanja wa Samora Utachezwa leo Kati ya Lipuli na Yanga utaanza saa 9:30 Alasiri (sio saa kumi) kama ilivyopangwa awali.

Hii ni kutokana na kwamba kama kutakuwa na suluhu (sare) baada ya dk 90 kutakuwa na Extra Time na baadaye penalty.

Na viingilio vya mchezo wa leo ni kama ifuatavyo

V.I.P – 20,000
MZUNGUKO 5,000
WATOTO – 2,500

Upatapo taarifa hii usisite kumjulisha na Mwenzio ili kuepusha usumbufu unaoweza kujitokeza

Imetolewa

ALLY NGALA
Katibu Mkuu IRFA

Viongozi Yanga watua Iringa kuongeza nguvu

Viongozi wapya wa klabu ya Yanga wametimiza ahadi baada ya kuwasili mkoani Iringa kuiunga mkono timu yao inayoshuka uwanja wa Samora kuikabili Lipuli Fc katika mchezo wa nusu fainali kombe la FA

Msafara wa viongozi hao umeongozwa na Mwenyekiti Dk Mbette Mshindo Msolla na Makamu Mwenyekiti Fredrick Mwakalebela pamoja na Wajumbe wa Kamati ya Utendaji

Yanga imeweka mkazo katika kuhakikisha wanatinga fainali na baadae kutwaa taji la kombe la FA ili kupata nafasi ya kushiriki michuano ya CAF msimu ujao