Esperance yatinga fainali ligi ya mabingwa, kucheza na Wydad Casablanca

Esperance imetinga fainali ligi ya mabingwa Barani Afrika baada ya kuiondosha TP Mazembe kwa ushindi wa bao 1-0

Esperance leo imeilazimisha TP Mazembe suluhu ya bila kufungana katika mchezo uliopigwa dimba la Mazembe, Lubumbashi huku ikitoka kushinda bao 1-0 kwenye mchezo wa kwanza

Mamelodi Sundowns pia imeshindwa kupindua matokeo ya 2-1 iliyofungwa na Wydad Casablanca kwenye mchezo wa kwanza baada ya kulazimishwa suluhu ya bila kufungana

Esperance imetinga fainali kwa msimu wa pili mfululizo sasa itachuana na Wydad Casablanca michezo miwili ya fainali itakayopigwa mwishoni mwa mwsi huu

Yanga yasogeza mbele Gala Dinner

Uongozi wa Yanga umeahirisha hafla ya chakula cha jioni (Gala Dinner) iliyokuwa limepangwa kufanyika Jumamosi ijayo, May 11 2019 ili kuwapa nafasi wadau wa klabu hiyo kushiriki katika mazishi ya Mwanachama wao marehemu Dk Reginald Mengi ambaye aliwahi kuifadhili Yanga miaka ya nyuma

Hafla hiyo sasa itafanyika May 18 Hoteli ya Serena jijini Dar es salaam

Mwili wa Dk Mengi unatarajiwa kuwasili Jumatatu ambapo utahifadhiwa kwenye nyumba yake ya milele Jumamosi ya May 11, Machame mkoani Kilimanjaro

Igangula ajitoa uchaguzi Yanga

Mgombea mwingine wa nafasi ya Mwenyekiti Baraka Igangula amejiondoa katika kinyan’ganyiro cha nafasi hiyo katika uchaguzi wa Yanga utakaofanyika kesho Jumapili

Inaelezwa Igangula ameamua kumuunga mkono Dk Mshindo Msolla ambaye sasa atachuana na Dk Jonas Tiboroha aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa Yanga

Dk Msolla amepata uungwaji mkono mkubwa na anapewa nafasi kubwa ya kuibuka kidedea kwenye uchaguzi huo wa kesho

Yanga kupata viongozi wapya kesho

Wagombea wa nafasi mbalimbali za uongozi katika klabu ya Yanga leo wanahitimisha zoezi la kampeni kuelekea uchaguzi Mkuu wa klabu hiyo utakaofanyika kesho Jumapili ukumbi wa Bwalo la Polisi, Osterbay jijini Dar es salaam

Wagombea walianza kunadi sera zao kwa Wanachama Jumanne iliyopita

Nafasi ya Mwenyekiti wa Yanga inawaniwa na wagombea watatu Barak Igangula, Dk Jonas Tiboroha na Dk Mshindo Msolla wakati nafasi ya Makamu Mwenyekiti inawaniwa na wagombea wanne ambao ni Fredrick Mwakalebela, Janeth Mbene, Titus Osoro na Yono Kevela

Aidha wagombea 21 wanawania nafasi nane za wajumbe wa Kamati ya Utendaji

Wanachama wa Yanga wametakiwa kutofanya makosa kwenye uchaguzi wa kesho kwa kuwachagua viongozi ambao wataweza kuipeleka Yanga mbele

Suala la Mabadiliko limekuwa kilio cha Wanayanga. Wagombea wote wameahidi kufanya mabadiliko, ni jukumu la Wanachama kujiridhisha na uwezo wao na ahadi walizotoa katika kutatua changamoto zinazoikabili Yanga

Wanachama wameaswa kutochagua viongozi kwa mazoea badala yake wachague viongozi ambao wana upeo mkubwa

Ni vyema kiongozi atakayechaguliwa awe na uwezo wa kutengeneza mikakati ya kuipeleka Yanga kule ambako kila mdau anahitaji kuona klabu ikielekea

Huu sio wakati wa kujaribu viongozi, Wanachama wawaweke madarakani ‘watu wa kazi’

Wanachama wasichague viongozi kwa papara, mihemko na makundi, kila mmoja afanye uamuzi kwa maslahi ya klabu kwa kuchagua viongozi wenye tija

Yanga ikipata viongozi wazuri, utakuwa mwanzo wa kutengeneza Yanga imara ambayo itagombewa na wawekezaji na kuifanya timu hiyo kongwe zaidi Tanzania kuondokana na dimbwi la ‘umasikini’

Pointi 18 kuipa Simba ubingwa

Licha ya Yanga kuongoza ligi kwa tofauti ya alama tano dhidi ya Simba, haitakuwa na ubavu wa kuipoka Simba taji walilotwaa msimu uliopita kama mabingwa hao watetezi watashinda michezo sita tu kati ya tisa ilyobaki

Yanga ina alama 80 na imebakiwa na michezo minne ambayo hata kama wakishinda yote watafikisha alama 92

Simba yenye alama 75 ikishinda michezo sita itafikisha alama 93 ambazo hazitafikiwa na timu nyingine yoyote

kesho Simba itarejea uwanja wa Sokoine kusaka alama nyingine tatu kati ya 18 zinazohitajika ili kutetea ubingwa katika mchezo dhidi ya Tanzania Prisons

Habari njema ni kwamba baada ya mchezo huo, Simba itarejea jijini Dar es salaam ambako itacheza michezo sita

Ushindi katika michezo hiyo itakayopigwa uwanja wa Taifa/Uhuru, utawahakikishia mabingwa hao kuubakisha ubingwa Msimbazi mapema tu hata kabla ya tarehe ya mwisho ya kufunga msimu

Nyoni aahidi pointi tatu dhidi ya Tanzania Prisons

Beki kiraka wa Simba Erasto Nyoni amesema wamefuata alama sita mkoani Mbeya, alama tatu walizipata jana na kesho watapambana kuhakikisha wanapata alama nyingine tatu dhidi ya Tanzania Prisons

Licha ya changamoto ya ukaribu wa michezo yake, Nyoni amesema wataendelea kujituma ili kupata matokeo yatakayo-wahakikishia kutetea ubingwa waliotwaa msimu uliopita

Baada ya ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Mbeya City jana, kesho Jumapili Simba itarudi tena uwanja wa Sokoine kuikabili Tanzania Prisons

Simba itahitaji kuwa katika ubora wake ili kuondoka na ushindi dhidi ya Prisons iliyoimarisha kiwango chake tangu ilipoanza kunolewa na kocha Adolph Richard

Aidha mazingira ya uwanja wa Sokoine yanaweza kuchangia kuharibu burudani kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha mkoani humo

Hata hivyo Nyoni amesema kama walifanikiwa kupata ushindi dhidi ya Mbeya City kwenye uwanja huo, basi watahakikisha wanashinda mchezo dhidi ya Prisons

“Hali ya uwanja hatuwezi kuikwepa lakini jambo la msingi kwetu tutahakikisha tunapambana. Tunawaahidi mashabiki wetu kuwa tumedhamiria kushinda mchezo huo,” amesema

Simba iheshimiwe – Manara

Msemaji wa Simba Haji Manara ameeleza kushangazwa na kauli zinazotolewa na baadhi ya makocha wa timu zinazoshiriki ligi kuu kuwa timu hiyo inabebwa

Akizungumza na waandishi wa habari mkoani Mbeya leo, Manara amesema uongozi wa timu hiyo uliamua kukaa kimya kwa kuwa haukuona umuhimu wa kuwajibu wanaoropoka

Hata hivyo amesema ukimya huo haumaanishi kuwa wanazifurahia kauli hizo

Amesema Simba ni taasisi kubwa na ametaka taasisi hiyo iheshimiwe, isiingizwe katika tuhuma ambazo hazina ukweli wowote

“Tunawataka wote wanaotuhusisha na masuala ya rushwa waache mara moja na kama wana usahidi wapeleke kwa vyombo husika,” amesema

“Simba sio klabu dhaifu, Simba sio klabu nyonge isifike mahali Simba ikafanywa kuwa ni timu dhaifu. Simba ni taasisi kubwa, tunaomba iheshimiwe”

“Mafanikio tunayopata yanatokana na ubora wa timu yetu. Msimu huu tumefika robo fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa, mtu anasemaje kuwa kiwango cha soka Tanzania hakijapanda?”

“Huku ni kuikosea heshima nchi yetu”

Azam Fc yaichapa KMC 1-0, yatangulia fainali kombe la FA

Azam Fc imefanikiwa kutinga fainali ya michuano ya kombe la FA (ASFC) baada ya kupata ushindi wa bao 1-0 dhidi ya KMC katika mchezo wa kwanza wa nusu fainali ambao umechezwa uwanja wa Azam Complex

Bao pekee la Azam lilifungwa na Donald Ngoma katika dakika ya 75

Mchezo wa pili wa nusu fainali kati ya Lipuli Fc dhidi ya Yanga utachezwa Jumatatu, May 06 uwanja wa Samora mkoani Iringa

Mshindi wa mchezo huo atachuana na Azam Fc katika mchezo wa fainali utakaopigwa Juni 02 2019 uwanja wa Ilulu mkoani Lindi

Yanga yatua Iringa kibabe, yaipania Lipuli Fc

Vinara wa ligi kuu Tanzania Bara Yanga waliwasili mkoani Iringa jana jioni tayari kwa mchezo wa nusu fainali kombe la FA dhidi ya Lipuli fc

Mchezo huo utapigwa Jumatatu, May 06 uwanja wa Samora

Yanga inayosaka nafasi ya kurejea kwenye michuano ya Kimataifa msimu ujao, imepania kushinda mchezo huo ili kutinga fainali ambapo kama ikifanikiwa, itachuana na Azam Fc

Msafara wa Yanga umejumuisha wachezaji 24 ambao leo wataanza maandalizi ya mchezo huo mkoani Iringa