Samatta aunga mkono zawadi kwa Kapombe

Nahodha wa Taifa Stars Mbwana Samatta ameungana na wadau wanaoamini beki Shomari Kapombe ambaye aliumia nchini Afrika Kusini wakati akiwa kambini na kikosi cha Stars, anastahili kupewa zawadi kama walivyopewa wachezaji wote waliyoipeleka Stars fainali za AFCON 2019

Samatta ambaye tayari amerudi Ubelgiji kuungana na KRC Genk, amesema TFF inapaswa kumjumuisha mchezaji huyo kwenye zawadi zinazotolewa kwa kuwa aliumia wakati akitimiza majukumu ya timu ya Taifa

Aidha Samatta amesema kama hilo haliwezekani basi atawashawishi wachezaji wote wagawane na Kapombe kile walichozawadiwa

Samatta amekwenda mbali zaidi kwa kusema kama hilo haliwezekani nalo basi yeye atagawana na Kapombe nusu kwa nusu zawadi alizozawadiwa kama mchezaji wa timu ya Taifa

Nae Kapombe amesema amefurahi uiona Stars inakata tiketi ya kushiriki fainali za AFCON mwaka huu

“Nimefurahi sana kama mtanzania ambaye pia nilikuwa kwenye kikosi huko nyuma licha ya kutolewa baadaye kwakuwa nisingeweza kucheza.

“Natoa pongezi kubwa kwa wachezaji wenzangu, na wale waliosaidia kufika hatua hii.

“Kwakweli ni jambo kubwa sana kutokea kwasababu ni miaka 39 nafasi hii ilikuwa haijatokea kwetu, nina furaha kubwa kwakweli”.

Kapombe amesema hali yake inaendelea vizuri na tayari ameanza mazoezi mepesi akitarajiwa kujiunga na kikosi cha Simba baada ya wiki tatu hadi nne

Serikali kutoa Sh. Bilioni moja kwa timu ya Serengeti Boys

Serikali kutoa Sh. Bilioni moja kwa timu ya Serengeti Boys

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli amesema kuwa serikali itatoa shilingi bilioni moja kwaajili ya kuiwezesha Serengeti Boys.

Rais Magufuli amesema kuwa atatoa fedha hizo ili kuiwezesha timu hiyo kufanya vizuri kwenye mashindano ya Afrika kwa vijana AfconU17 yatakayofanyika nchini Tanzania mwezi Aprili mwaka huu.

Rais Magufuli amesema kuwa ataendelea kushirikiana na Wizara ya Michezo kwa kuwa Timu ya Taifa Stars imemfurahisha sana baada ya kuipiga timu ya Uganda 3 bila.

Rais Magufuli awaita wachezaji Stars Ikulu

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk John Magufuli amewaalika Ikulu wachezaji wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ pamoja na Bondia Hassani Mwakinyo aliyemtwanga Muargentina Sergio Eduardo katika pambano lililofanyika juzi nchini Kenya

Kulingana na taarifa iliyotolewa mapema leo na msemaji wa Ikulu Gerson Msigwa, Rais Magufuli atatoa pongezi kwao na kula nao chakula cha mchana

Jana Stars ilifanikiwa kufuzu fainali za AFCON 2019 baada ya kusubiri kwa miaka 39 ikiibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Uganda katika mchezo uliopigwa uwanja wa Taifa

Stars yakata tiketi AFCON 2019 baada ya kuichapa Uganda 3-0

Historia imeandikwa leo katika dimba la Taifa baada ya timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ kufuzu kwa fainali za AFCON 2019 kufuatia ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Uganda

Stars imefuzu kwa fainali hizo baada ya kusubiri kwa miaka 39

Matokeo ya suluhu ya bila kufungana kati ya Cape Verde dhidi ya Lesotho yameinufaisha Tanzania kuweza kuwa miongoni mwa timu 24 zitakazochuana nchini Misri mwezi Juni

Stars iliyokuwa katika kiwango bora, iliandika bao la kuongoza kwenye dakika ya 21 kupitia kwa Saimon Msuva aliyemalizia pasi murua ya John Bocco

Erasto Nyoni akaifungia Stars bao la pili kupitia mkwaju wa penati kwenye dakika ya 50 baada ya Samatta kumnawisha mlinzi wa Uganda ndani ya eneo la hatari

Bao lililoizamisha Uganda liliwekwa kimiani na Aggrey Morisi kwenye dakika ya 56 akimalizia krosi iliyochongwa na John Bocco

Ushindi wa Stars ulinogeshwa na idadi kubwa ya mashabiki waliofurika kuujaza uwanja wa Taifa

Kikosi cha Stars kilichoandika historia leo;

Manula, Hassan Kessy, Gadiel Michael, Agrey Morris, Kelvin Yondani, Erasto Nyoni , Saimon Msuva, Mudathir Yahya, John Bocco, Mbwana Samatta, Farid Mussa

AKIBA
Metacha Munata, Aron Kalambo, Ally Sonso, Kennedy Juma, Jonas Mkude, Himid Mao, Feisal Salum Fei Toto, Shiza Kichuya, Yahya Zaydi, Thomas Ulimwengu, Rashid Mandawa, ShabaanIddi Chilunda

KAPOMBE: Kurejea Kikosini SIMBA SC

Beki wa pembeni wa Simba Shomari Kapombe ameruhusiwa kuanza mazoezi mepesi tayari kurejea dimbani baada ya kupona majeraha ya goti

Hivi karibuni Kapombe alikwenda Afrika Kusini kufanyiwa uchunguzi wa jeraha alilopata wakati akiitumikia timu ya Taifa mwishoni mwa mwaka jana

Habari njema ni kwamba madaktari wameridhishwa na uponaji wa jeraha hilo hivyo kumruhusu Kapombe kuanza mazoezi mepesi

Kiraka huyo aliyekuwa nje ya dimba kwa takribani miezi mitano, anatarajiwa kuanza mazoezi mepesi wiki ijayo na huenda akarejea kikosini mapema kuwahi mchezo wa marudiano wa robo fainali ligi ya mabingwa dhidi ya TP Mazembe utakaopigwa April 12 au 13 huko DR Congo

Uganda kumpaisha au kumponza Amunike

Kikosi cha Stars leo kitakuwa katika dimba la Taifa kuikabili Uganda Cranes katika mchezo wa kusaka tiketi ya kutinga fainali za AFCON 2019

Mchezo huo ambao ushindi ni lazima kwa Stars, utapigwa saa 12 jioni

Kocha Mkuu wa Stars Emmanuel Amunike amesema wamefanya maandalizi ya kutosha na anaamini vijana wake watafuata maelekezo na hatimaye kuibuka na ushindi

Ni mchezo ambao umeshikilia hatma ya Amunike kuendelea kuinoa Stars au kurejea kwao Nigeria kama atashindwa kuiongoza Stars kupata matokeo leo

Katika michezo iliyopita Amunike alikumbana na ukosoaji mkubwa kutoka kwa wadau wa soka nchini kutokana kutofurahishwa na uteuzi wa wachezaji, mbinu pamoja na upangaji wa kikosi chake

Stars ilikuwa na nafasi ya kufuzu mapema kama ingeweza kushinda mchezo uliopita dhidi ya Lesotho. Hata hivyo Amunike alipanga kikosi cha kujihami zaidi katika mchezo huo na kupelekea Stars kuchapwa bao 1-0 ugenini

Wengi wanasubiri kwa hamu kikosi atakachopanga leo dhidi ya Uganda ambapo Stars haihitaji matokeo mengine tofauti na ushindi

Lakini ni dhahiri hatma yake itakuwa mikononi mwake mwenyewe, kwani kama Stars haitashinda nae safari ya kurejea Nigeria itakuwa imewadia

Uganda, Kenya, Burundi zatangulia AFCON 2019, Stars zamu yetu leo

Timu ya Taifa ya Burundi jana iliandika historia ya kukata tiketi ya kushiriki fainali za AFCON 2019 kwa mara ya kwanza baada ya kutoka sare ya ao 1-1 dhidi ya Togo matokeo ambayo yamewapa nafasi ya kwenda Misri

Burundi imeungana na Uganda na Kenya kuwa timu kutoka Afrika Mashariki ambazo zimefuzu kwa fainali hizo zitakazopigwa mwezi Juni mwaka huu

Leo Tanzania inaweza kuwa timu ya nne kutoka ukanda wa Afrika Mashariki kufuzu kwa fainali za michuano hiyo kama itapata ushindi dhidi ya Uganda huku ikiomba matokeo mabaya kwa Lesotho

Ni mchezo wa ‘kufa au kupona’ kwa Stars ambayo inajaribu kurudia kile ilichokifanya miaka 39 iliyopita kwa kutinga fainali za michuano hiyo zilizofanyika Nigeria mwaka 1980

Mchezo dhidi ya Uganda utapigwa saa 12 jioni sambamba na mchezo mwingine wa kundi L kati ya Cape Verde dhidi ya Lesotho

Kila la kheri Stars…!

SAMATTA : Aahidi kuibeba TAIFA STARS

Nahodha wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ Mbwana Samatta amesema wachezaji wa timu hiyo leo wana kazi moja tu ya kuhakikisha wanapata ushindi dhidi ya Uganda kuwania nafasi ya kufuzu kwa fainali za michuano ya AFCON 2019

Akizungumza kwa niaba ya wachezaji baada ya kutembelewa na Waziri Mkuu katika kambi ya kikosi cha Stars, Samatta amesema wanajiona kuwa na deni kubwa kwa Watanzania na watahakikisha wanawapa furaha kwa kupata ushindi leo

“Naona naenda kuiongoza nchi siku ya kesho (leo), sitakuwa nahodha kwa ajili ya wachezaji peke yake bali nitakuwa nahodha kwa ajili ya wananchi wote wa Tanzania,” amesema Samatta

“Wachezaji wote wako tayari kwa ajili ya kuitetea nchi yao, lengo kubwa ni kuhakikisha bendera yetu ya Tanzania inasimama, Dunia itambue na Afrika yote ifahamu”

Jana Waziri Mkuu Mh Kassim Majaliwa alitembelea kambi ya wachezaji wa timu ya Taifa na kuwaeleza kwamba Serikali na wananchi wanamatumaini makubwa kwa timu yao, hivyo wahakikishe wanapata ushindi katika mechi yao dhidi ya timu ya Taifa ya Uganda leo

“Macho yote ya Watanzania yameelekezwa katika mechi ya kesho (leo) na Serikali inamatumaini makubwa na timu ya Taifa, hivyo muelewe kwamba kesho (leo) ni siku muhimu sana. Lengo letu ni kufikia hatua ambayo mataifa mengine yamefikia”