Esperance yatinga fainali ligi ya mabingwa, kucheza na Wydad Casablanca

Esperance imetinga fainali ligi ya mabingwa Barani Afrika baada ya kuiondosha TP Mazembe kwa ushindi wa bao 1-0

Esperance leo imeilazimisha TP Mazembe suluhu ya bila kufungana katika mchezo uliopigwa dimba la Mazembe, Lubumbashi huku ikitoka kushinda bao 1-0 kwenye mchezo wa kwanza

Mamelodi Sundowns pia imeshindwa kupindua matokeo ya 2-1 iliyofungwa na Wydad Casablanca kwenye mchezo wa kwanza baada ya kulazimishwa suluhu ya bila kufungana

Esperance imetinga fainali kwa msimu wa pili mfululizo sasa itachuana na Wydad Casablanca michezo miwili ya fainali itakayopigwa mwishoni mwa mwsi huu

Pointi 18 kuipa Simba ubingwa

Licha ya Yanga kuongoza ligi kwa tofauti ya alama tano dhidi ya Simba, haitakuwa na ubavu wa kuipoka Simba taji walilotwaa msimu uliopita kama mabingwa hao watetezi watashinda michezo sita tu kati ya tisa ilyobaki

Yanga ina alama 80 na imebakiwa na michezo minne ambayo hata kama wakishinda yote watafikisha alama 92

Simba yenye alama 75 ikishinda michezo sita itafikisha alama 93 ambazo hazitafikiwa na timu nyingine yoyote

kesho Simba itarejea uwanja wa Sokoine kusaka alama nyingine tatu kati ya 18 zinazohitajika ili kutetea ubingwa katika mchezo dhidi ya Tanzania Prisons

Habari njema ni kwamba baada ya mchezo huo, Simba itarejea jijini Dar es salaam ambako itacheza michezo sita

Ushindi katika michezo hiyo itakayopigwa uwanja wa Taifa/Uhuru, utawahakikishia mabingwa hao kuubakisha ubingwa Msimbazi mapema tu hata kabla ya tarehe ya mwisho ya kufunga msimu

Nyoni aahidi pointi tatu dhidi ya Tanzania Prisons

Beki kiraka wa Simba Erasto Nyoni amesema wamefuata alama sita mkoani Mbeya, alama tatu walizipata jana na kesho watapambana kuhakikisha wanapata alama nyingine tatu dhidi ya Tanzania Prisons

Licha ya changamoto ya ukaribu wa michezo yake, Nyoni amesema wataendelea kujituma ili kupata matokeo yatakayo-wahakikishia kutetea ubingwa waliotwaa msimu uliopita

Baada ya ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Mbeya City jana, kesho Jumapili Simba itarudi tena uwanja wa Sokoine kuikabili Tanzania Prisons

Simba itahitaji kuwa katika ubora wake ili kuondoka na ushindi dhidi ya Prisons iliyoimarisha kiwango chake tangu ilipoanza kunolewa na kocha Adolph Richard

Aidha mazingira ya uwanja wa Sokoine yanaweza kuchangia kuharibu burudani kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha mkoani humo

Hata hivyo Nyoni amesema kama walifanikiwa kupata ushindi dhidi ya Mbeya City kwenye uwanja huo, basi watahakikisha wanashinda mchezo dhidi ya Prisons

“Hali ya uwanja hatuwezi kuikwepa lakini jambo la msingi kwetu tutahakikisha tunapambana. Tunawaahidi mashabiki wetu kuwa tumedhamiria kushinda mchezo huo,” amesema

Simba iheshimiwe – Manara

Msemaji wa Simba Haji Manara ameeleza kushangazwa na kauli zinazotolewa na baadhi ya makocha wa timu zinazoshiriki ligi kuu kuwa timu hiyo inabebwa

Akizungumza na waandishi wa habari mkoani Mbeya leo, Manara amesema uongozi wa timu hiyo uliamua kukaa kimya kwa kuwa haukuona umuhimu wa kuwajibu wanaoropoka

Hata hivyo amesema ukimya huo haumaanishi kuwa wanazifurahia kauli hizo

Amesema Simba ni taasisi kubwa na ametaka taasisi hiyo iheshimiwe, isiingizwe katika tuhuma ambazo hazina ukweli wowote

“Tunawataka wote wanaotuhusisha na masuala ya rushwa waache mara moja na kama wana usahidi wapeleke kwa vyombo husika,” amesema

“Simba sio klabu dhaifu, Simba sio klabu nyonge isifike mahali Simba ikafanywa kuwa ni timu dhaifu. Simba ni taasisi kubwa, tunaomba iheshimiwe”

“Mafanikio tunayopata yanatokana na ubora wa timu yetu. Msimu huu tumefika robo fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa, mtu anasemaje kuwa kiwango cha soka Tanzania hakijapanda?”

“Huku ni kuikosea heshima nchi yetu”

MATOKEO MECHI ZA LEO LIGI KUU

MATOKEO YA MECHI ZA LEO

FT: Mbeya City 1-2 Simba SC (Naldo 22’ : Mkude 68’, Kagere 85’)
.
.
FT: Singida United 1-1 Mtibwa Sugar (Habib Kyombo 32’ : Ismail Aidan 45’+1)
.
.
FT: Ruvu Shooting 3-1 JKT Tanzania (Musa Said 48’, Emmanuel Martin 59’, Fully Maganga 79’: Ally Bilaly 44’)
.
.
FT: Alliance FC 2-2 Kagera Sugar (Birimana Blaise 39’, Dickson Ambundo 90’+5 : Ramadhan Kapera 53’, Peter Mwalyanzi 71’)
.
.
#TanzaniaPremierLeague

Rekodi ya mabao Simba inatisha

Simba imeendelea ‘kuzikimbiza’ timu nyingine zinazoshiriki ligi kuu ya Tanzania Bara, ikiongoza kwa kufunga mabao

Mabao mawili yaliyoiwezesha Simba kupata ushindi wa 2-1 dhidi ya Mbeya City leo, yameifanya timu hiyo iwe imefunga mabao 60

Meddie Kagere sasa ndiye kinara wa kuzifumania nyavu akiwa ametupia kambani mabao 17 akiwaacha washindani wake Salum Aiyee (16) na Heritier Makambo (16)

Katika mabao 60 yaliyofungwa mpaka sasa, Kagere, Okwi na Bocco wamechangia mabao 41

Kagere (17), Okwi (10) na Bocco (14)

Lakini pia Simba ndio timu iliyoruhusu mabao machache zaidi mpaka sasa ikiwa imefungwa mabao 12 tu. Azam Fc inafuatia ikiwa imeruhusu mabao 19

Simba inakaribia kutetea ubingwa wake ikihitaji kushinda michezo sita kati ya tisa iliyobaki

Baada ya mchezo dhidi ya Tanzania Prisons keshokutwa, Simba itarejea jijini Dar es salaam ambako itacheza michezo sita katika dimba la Taifa/Uhuru

Huenda ikatangaza ubingwa kupitia michezo hiyo

FT : Mbeya City 1-2 Simba

Mabingwa watetezi ligi kuu ya Tanzania Bara Simba wameendelea kuukaribia ubingwa wa pili mfululizo baada ya leo kuichapa Mbeya City mabao 2-1 katika mchezo uliopigwa uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya

Mchezo huo uliathiriwa na mazingira ya uwanja uliojaa maji baada ya mvua kunyesha muda mchache kabla ya mchezo kuanza

Mbeya City ilitangulia kufunga bao katika dakika ya 22 kupitia kwa Iddi Selemani Naddo

Hata hivyo Simba ilirejea ikiwa imara kwenye kipindi cha pili na kusawazisha bao hilo kupitia kwa Jonas Mkude kwenye dakika ya 68 kabla Meddie Kagere hajaihakikishia Simba alama tatu muhimu kwa kufunga bao la ushindi kwenye dakika ya 85

Ushindi huo umeifanya Simba ifikishe alama 75, ikiendelea kushika nafasi ya pili kwa tofauti ya alama tano dhidi ya Yanga

Itacheza mchezo mwingine dhidi ya Tanzania Prisons keshokutwa Jumapili hapohapo dimba la Sokoine