Okwi, Kagere waweka rekodi ya ‘hat-trik’ ligi kuu

Washambuliaji Emmanuel Okwi na Meddie Kagere wameweka rekodi ya kufunga hat-trik mbili kwenye mchezo mmoja wa ligi kuu

Washambuliaji hao hatari wa Simba wamefunga mabao matatu kila mmoja katika mchezo dhidi ya Coastal Union uliomalizika kwa Simba kuibuka na ushindi wa mabao 8-1

Mwamuzi wa mchezo huo Jonesia Rikiyaa aliwakabidhi mpira kila mmoja baada ya mchezo kumalizika

Hizo zilikuwa hat-trik za sita kufungwa kwenye ligi msimu huu

Kagere amefikisha mabao 20 na kujiimarisha kileleni katika mbio za kuwania kiatu cha dhahabu akiwaacha Heritier Makambo na Salim Aiyee wakibaki na mabao 16

Okwi mfungaji bora wa ligi msimu uliopita, amerejea katika mbio za kuwania kiatu hicho baada ya leo kufikisha mabao 14 akimfikisha mshambuliaji mwingine wa Simba John Bocco

Kagere, Okwi na Bocco wameifungia Simba mabao 48 kwa pamoja

FT : Simba 8-1 Coastal Union

Mabingwa watetezi ligi kuu ya Tanzania Bara Simba wamerejea kileleni mwa msimamo wa ligi kibabe baada ya kuifumua Coastal Union mabao 8-1 kwenye mchezo uliopigwa uwanja wa Uhuru

Leo ilikuwa siku ya sherehe ya mabao kwa washambuliaji wawili wa Simba Emmanuel Okwi na Meddie Kagere ambao wamefunga ‘hat-trik’ kila mmoja

Alianza Okwi kupiga hat-trik kabla ya Kagere kupata ya kwake kwenye kipindi cha pili

Mabao mengine mawili yalifungwa na viungo Hassani Dilunga na Clatous Chama aliyefunga bao lake kwenye dakika za majeruhi

Kagere amejichimbia kileleni katika mbio za kuwania kiatu cha dhahabu akiwa amefikisha mabao 201 wakati Okwi amemfikia John Bocco baada ya kufikisha mabao 14

Simba ni kama imezianza sherehe za ubingwa leo na itahitaji kushinda michezo minne tu ili kutawazwa mabingwa kwa msimu wa pili mfululizo

Aussems afichua usajili atakaofanya

Kocha Mkuu wa Simba Patrick Aussems amesema atakiongezea nguvu kikosi chake mwishoni mwa msimu kwa kusajili wachezaji wanne

Simba inayoelekea kutetea taji lake la ligi kuu kwa msimu wa pili mfululizo, inatarajiwa kurejea jijini Dar es salaam leo wakitokea mkoani Mbeya ambako wameshinda michezo yote miwili dhidi ya Mbeya City na Tanzania Prisons

Akizungumza baada ya mchezo jana, Aussems amesema ushindi wa bao 1-0 waliopata dhidi ya Tanzania Prisons umewaweka katika nafasi nzuri zaidi ya kutetea ubingwa na kujihakikishia nafasi ya kushiriki michuano ya ligi ya mabingwa msimu ujao

Amesema atakiboresha kikosi chake ili wafike mbali zaidi ya mafanikio waliyopata kwenye michuano hiyo msimu huu

Aussems ametaja maeneo ambayo atayaboresha kwa kusajili wachezaji wapya ni eneo la ulinzi (mabeki wawili), kiungo mmoja na mshambuliaji mmoja

Aidha, Aussems amesema timu yake inakabiliwa na changamoto ya kufanya vizuri Kimataifa kutokana na ukweli kuwa haipati ushindani mkubwa kutoka timu za ndani

Kagera Sugar yawahi Dar, Simba kurejea leo kutoka Mbeya

Kagera Sugar ndio timu pekee iliyopata ushindi dhidi ya Simba katika michezo minne ya kanda ya ziwa waliyocheza mabingwa hao watetezi kwenye duru ya pili

Kagera Sugar inayonolewa na kocha Mecky Mexime tayari kimewasili jijini Dar es salaam kusubiri mchezo dhidi ya Simba utakaopigwa Ijumaa, May 10

Simba wao watarejea jijini Dar es salaam leo wakitokea mkoani Mbeya ambako walifanikiwa kuchukua alama zote sita dhidi ya Mbeya City na Tanzania Prisons

Hata hivyo kabla ya kucheza na Kagera Sugar Ijumaa, siku ya Jumatano Simba itachuana na Coastal Union katika mchezo utakaopigwa uwanja wa Taifa/Uhuru

Simba inahitaji kushinda michezo mitano tu kuweza kutetea ubingwa wake bila ya kujali matokeo ya Yanga ambayo imebakiwa na michezo minne ambayo kama wakishinda yote watafikisha alama 92

Ushindi katika michezo mitano utaifanya Simba ifikishe alama 93

Simba mwendo mdundo, ubingwa huoooo

Ni suala la muda tu kabla ya mabingwa wa nchi, Simba kutangazwa tena kuwa wameuhifadhi ubingwa wao kwa msimu wa pili mfululizo baada ya ushindi wa leo wa bao 1-0 dhidi ya Tanzania Prisons

Simba imejiweka katika mazingira mzuri ya kutetea ubingwa wake baada ya kuondoka na alama zote sita mkoani Mbeya

Mbeya City na Tanzania Prisons zilikuwa zikiangaliwa kuwa na uwezo wa ‘kuitibulia’ Simba hesabu zake kuelekea ubingwa

Simba imesalia na michezo nane, michezo sita itapigwa jijini Dar es salaam kunako uwanja wa Taifa au Uhuru

Simba itatoka nje ya jiji kuzifuata Singida United na Mtibwa Sugar (mchezo wa pili) wakati Coastal Union, Kagera Sugar, Azam Fc, Mtibwa Sugar(mchezo wa kwanza), Ndanda na Biashara United zote zitaifuata Simba ‘majinjioni’ uwanja wa Taifa

Simba huenda ikarejea rasmi kileleni mwa msimamo wa ligi Jumatano May 08 itakapocheza na Coastal Union mchezo utakaopigwa uwanja wa Taifa/Uhuru

FT : Prisons 0-1 Simba

Simba imeendelea kuukaribia ubingwa wa pili mfululizo baada ya leo kuichapa Tanzania Prisons bao 1-0 katika mchezo uliopigwa uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya

Bao pekee la Simba lilipatikana kwenye kipindi cha kwanza likiwekwa kambani na Emmanuel Okwi katika dakika ya 11 baada ya shambulizi la kushitukiza

Ushindi huo umeendelea kuisogeza Simba kileleni baada ya kufikisha alama 78 sasa ikihitaji alama mbili tu kuweza kuifikia Yanga

Yanga ina alama 80 ikiwa imecheza michezo minne zaidi ya Simba pia

Okwi ameendelea kuwasogelea vinara wa mabao leo akifikisha mabao 11

Mchezo unaofuata ni dhidi ya Coastal Union na utapigwa May 08 kwenye uwanja wa Taifa

Mashabiki Mbeya kama kawaida uwanja wa Sokoine leo

Simba leo iko ugenini mkoani Mbeya ikiikabili Tanzania Prisons katika mchezo wa pili utakaopigwa uwanja wa Sokoine katika kipinci cha siku tatu

Lakini asikwambie mtu, mzuka wa mashabiki wa timu hiyo mkoani Mbeya, unawafanya mabingwa hao wa Tanzania Bara kutojihisi kabisa kama wako ugenini

Katika mchezo dhidi ya Mbeya City ambao Simba iliibuka na ushindi wa mabao 2-1, mashabiki wa ‘Mnyama’ walifunika dimba la Sokoine.

Leo tena wameahidi kuwa sambamba na timu yao kuhakikisha alama zote tatu zinakwenda Msimbazi

Mchezo unatarajiwa kuanza saa kumi kamili jioni na tayari mashabiki wameanza kujisogeza uwanja wa Sokoine

Simba yasaka alama nyingine tatu Mbeya

Baada ya ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Mbeya City juzi, leo Simba inarejea tena uwanja wa Sokoine kuikabili Tanzania Prisons

Mchezo ambayo kama Simba itaibuka na ushindi, itasogea zaidi kileleni mwa msimamo wa kwani itabakisha alama mbili tu kuifikia Yanga

Meneja wa Simba Patrick Rweyemamu amesema wachezaji wa timu yake wako katika hali nzuri, wamejiandaa vyema kuweza kupata alama nyingine tatu leo

Tanzania Prisons ilitua mkoani Mbeya juzi ikitokea Dar es salaam ambako ilifungwa na Yanga mabao 2-1

Kocha Mkuu wa timu hiyo Adolph Richard amesema wanatarajia mchezo hautakuwa mwepesi lakini wamepania kupata matokeo ili kujiweka salama na hatari ya kuteremka daraja

Baada ya mchezo huo Simba itarejea jijini Dar es salaam ambako itakuwa na nafasi ya kutwaa ubingwa katika michezo sita itakayocheza uwanja wa Taifa/Uhuru