Simba: Tutapigana dakika zote 90

Wakati Simba ikiikabili TP Mazembe kwenye mchezo wa pili wa hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika, kocha wake, Patrick Aussems amesema watapambana dakika zote 90. Mchezo huo umepangwa kufanyika Stade TP Mazembe, Lubumbashi DR Congo.
Awali kwenye mchezo wa kwanza wa robo fainali uliopigwa Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam wiki moja iliyopita, Simba ambao ni wawakilishi wa Tanzania kwenye mashindano hayo walibanwa mbavu na kwenda suluhu.
Kikosi kamili cha Simba kikiongozwa na nahodha wao, John Bocco kiliondoka jana asubuhi kwa ndege ya kukodi kikiwa na wachezaji 18 tayari kwa mchezo huo wa marudiano.
Kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Kimataifa wa Julius Nyerere (Terminal 1) Aussems alisema wamejiandaa kwa wiki moja kwenda kutafuta matokeo ya ushindi Lumbambashi ili kutinga nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Katika wiki hiyo Simba walianza maandalizi yao kwa kujikita na mazoezi ya kujenga utimamu kwa wachezaji hiyo huku siku chache kabla ya kuondoka wakijinoa pia kwenye upigaji wa mikwaju ya penati.
“Ninaiheshimu TP Mazembe kwa sababu ni timu kubwa yenye rekodi nzuri kwenye mashindano haya lakini hatuiogopi.Tumejiandaa kama tulivyopanga na nina imani kuwa tunakwenda kukitekeleza kile ambacho tumekifanyia kazi kwenye mazoezi.
“Natambua umuhimu wa mashabiki wetu ambao walikuwa wakitupa nguvu kwenye michezo yetu ya nyumbani tunaenda ugenini ambako mazingira yatakuwa tofauti ila niwatoe woga kwa kusema tutapambana kusonga mbele.

“Inawezekana kuingia hatua ya nusu fainali. Tulitengeneza nafasi kwenye mchezo wa kwanza ila tulishindwa kuzitumia hivyo naamini kuwa hata kwenye mchezo huu wa ugenini tunaweza kutengeneza nafasi,” alisema Aussems
Ili Simba isonge mbele kwenye hatua ya nusu fainali, inahitaji ushindi kwenye mchezo huo au sare ya aina yoyote ya mabao.

Kama mchezo huo ukimalizika kwa suluhu kama ilivyokuwa mchezo wa kwanza jijini Dar es Salaam, Simba na TP Mazembe basi mshindi ataamuliwa kwa mikwaju ya penalti.

Aussems alisema mchezaji pekee ambaye atakosekana kwenye kikosi chake ni beki wa kati, Pascal Wawa ambaye ni majeruhi baada ya kuumia kwenye mchezo wa kwanza uliofanyika jijini Dar es Salaam.
“Nina wachezaji 24 kwenye kikosi changu hivyo ni rahisi pindi anapoumia mmoja nafasi yake kuzibwa na mwingine, nadhani mliona namna Juuko alivyoziba pengo lake kwenye mchezo wa kwanza,” alisema kocha huyo wa Mbelgiji.

Nahodha wa kikosi hicho, John Bocco alisema wapo kwenye hali nzuri na akatoa ahadi kwa wapenzi na mashabiki wa Simba kuwa lengo lao ni kutinga nusu fainali na sio kitu kingine.
“Tunaenda kupambana. Kushikamana kwetu kwenye mchezo uliopita kama wachezaji kutaendelea ili tuweke historia nyingine ya kutinga hatua ya nusu fainali.
“Kuna mashabiki wetu ambao walitamani kuwa nasi DR Congo lakini kutokana na sababu za kiuchumi pengine wamekwama niwaombe kitu kimoja watuombee ili kila kitu kiende kama tulivyopanga,” alisema Bocco.

Katika mchezo huo Simba itawategemea zaidi wachezaji wake wanne ambao wana mabao mengi katika mashindano hayo wakiongozwa na Meddie Kagere mwenye mabao sita, Clatous Chama(5),John Bocco (3) na Emmanuel Okwi mwenye mabao mawili katika safu ya ushambuliaji.
Wapinzani woa TP Mazembe wanawategemea Tressor Mputu mwenye mabao manne sawa na Jackosn Muleka, Kelvin Mondeko mwenye mabao matatu na Meshack Elia aliyefunga mawili.
Kikosi kamili cha wachezaji wa Simba ambacho kimekwenda DR Congo ni Aishi Manula, Deogratius Munishi ‘Dida’, Zana Coulibaly, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Juuko Murshid, Erasto Nyoni, Paul Bukaba, James Kotei, Jonas Mkude.
Nyota wengine ni Mzamiru Yassin, Said Ndemla, Haruna Niyonzima, Hassan Dilunga, Clatous Chama, John Bocco, Meddie Kagere, Emmanuel Okwi na Rashid Juma.

Kila kheri Simba, kila la kheri wawakilishi wa nchi

Mabingwa wa soka Tanzania Bara Simba leo wanashuka katika dimba la Stade De Mazembe huko Lubumbashi DR Congo kuikabili TP Mazembe kwenye mchezo wa pili wa robo fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika

Simba ina nafasi ya kutinga nusu fainali ya michuano hiyo kama itaibuka na ushindi au kutoka sare yoyote ya mabao

Simba ilitua Lubumbashi mapema jana Ijumaa na jioni kupata nafasi ya kufanya mazoezi katika uwanja wa Mazembe ambao utatumika baadae

Kocha Patrick Aussems amesema kikosi chake kiko tayari kuelekea mchezo huo na amewataka wapenzi, mashabiki wa Simba na Watanzania wote kwa ujumla kuwaombea dua ili waweze kuibuka na ushindi

Ushindi wa Simba leo ni faida kwa Tanzania kwani matokeo hayo yataisaidia Tanzania kuongezewa timu za kushiriki michuano ya CAF kuanzia msimu ujao

Simba tayari imedhihirisha kuwa inaweza kupambana na timu yoyote barani Afrika, mchezo wa leo utadhihirisha mara dufu uimara wa Simba

Kila la kheri Simba, kila la kheri mabingwa wa nchi, kila la kheri wawakilishi wa Tanzania..

MAKUNDI AFCON 2019

MAKUNDI YOTE SITA: #AFCON2019

Kundi A
Misri
DR Congo
Uganda
Zimbabwe

Kundi B
Nigeria
Guinea
Madagascar
Burundi

Kundi C
Senegal
Algeria
Kenya
Tanzania

Kundi D
Morocco
Ivory Coast
South Africa,
Namibia

Kundi E
Tunisia
Mali
Mauritania,
Angola

Kundi F
Cameroon
Ghana
Benin,
Guinea-Bissau

Simba yawasili Lubumbashi

Msafara wa kikosi cha Simba uliondoka mapema leo jijini Dar es salaam kuelekea DR Congo, umewasili salama katika mji wa Lubumbashi yalipo makazi ya klabu ya TP Mazembe

Kesho Jumamosi Simba itashuka dimba la Mazembe kuwakabili wenyeji wao katika mchezo wa pili wa robo fainali michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika

Simba imetumia usafiri wa Ndege Maalum ya kukodi na wataitumia Ndege hiyo kurejea nchini kesho baada ya mchezo

Mabingwa hao wa Tanzania leo jioni wanatarajia kujifua katika uwanja wa Mazembe ambao utatumika kwenye mchezo wa kesho

Aussems aahidi Simba tofauti Lubumbashi

Kikosi cha Simba tayari kimeondoka nchini kuelekea Lubumbashi DR Congo kwa ajili ya mchezo wa marudiano robo fainali ligi ya mabingwa barani Afrika dhidi ya TP Mazembe


Simba itashuka katika dimba la Mazembe kesho kuumana na wenyeji wao hao ambao mchezo wa raundi ya kwanza uliopigwa uwanja wa Taifa waliwalazimisha suluhu ya bila kufungana
Huo ulikuwa mchezo wa kwanza kwa Simba kushindwa kupata ushindi katika dimba la Taifa kwenye michuano ya ligi ya mabingwa msimu huu
Hata hivyo licha ya matokeo hayo kocha Mkuu wa mabingwa hao wa Tanzania Patrick Aussems amesema wana nafasi kubwa ya kupata matokeo yatakayowapeleka nusu fainali huko Lubumbashi

Aussems amesema mchezo waliocheza Dar umemsaidia kutambua udhaifu wa wapinzani wao na amerekebisha makosa yaliyosababisha wakose ushindi nyumbani
Amewataka mashabiki wa Simba na Watanzania wote kuwaombea huku akiahidi kuwa wataishuhudia Simba tofauti kabisa na ile ambayo ilipoteza michezo yote ya ugenini katika hatua ya makundi
Aussems amesema mbinu atakazotumia kwenye mchezo huo wa marudiano zitawashangaza Wakongo nyumbani kwao, licha ya kukiri ni pambano gumu.

Kocha huyo alisema wamegundua kwenye mchezo wa kwanza viungo wao walishindwa kumiliki mpira na washambuliaji kupoteza nafasi nyingi kizembe na kuwapa nafasi Mazembe kuwatawala, lakini wanapoenda kuwafuata kwao viungo wake na washambuliaji watakuwa na kazi maalum Lubumbashi.

“Hatutakiwi kufanya makosa ya kupoteza mpira katika sehemu ya kiungo, pia tukienda mbele tutatakiwa kuwa na malengo makubwa tutawalazimisha wafanye makosa, tuko katika utofauti mkubwa ukilinganisha na mechi za nyuma tulizocheza ugenini,” amesema

Simba imeondoka na kikosi cha wachezaji 18 ikitumia usafiri wa ndege ya kukodi. Itarejea jijini Dar es salaam kesho baada ya mchezo huo

Ni mchezo wa jasho na damu – Manara

Msemaji wa klabu ya Simba Haji Manara amesema kikosi cha timu hiyo kinatarajiwa kuondoka mapema kesho Ijumaa kuelekea DR Congo tayari kwa mchezo wa pili wa robo fainali ligi ya mabingwa barani Afrika dhidi ya TP Mazembe

Manara amesema Simba inakwenda Congo kupambana na watahakikisha wanaiwakilisha vyema nchi kwa kupata matokeo mazuri katika mchezo huo utakaopigwa keshokutwa Jumamosi kwenye uwanja wa TP Mazembe

Amesema wachezaji wa Simba wako tayari kuandika historia nje ya nchi

“Tunakwenda kesho kibingwa tukiwa hatuna cha kupoteza ila tunawaahidi jasho jingi litamwagika kuipigania Simba na nchi Jumamosi,” amesema Manara

“Hatuogopi lolote toka Mazembe pamoja na kuwapa heshima yao kama klabu kubwa”

“Wachezaji wetu wapo tayari kuionyesha Afrika ubora wao na ukubwa wa Simba. Tuombeeni tufike salama na turejee salama kifua mbele”

Simba inakwenda Congo kwa usafiri wa ndege maalum ya kukodi na itarejea nchini Jumamosi jioni baada ya mchezo

Viporo vya Simba kupangiwa ratiba maalum

Mkurugenzi wa Bodi ya Ligi Boniface Wambura amesema watahakikisha ligi inamalizika mwezi ujao kama ilivyopangwa na kuhusu viporo vya Simba vitapangiwa ratiba maalum

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Wambura alisema ratiba ya michezo ya Simba imekuwa na changamoto kutokana na ushiriki wa timu hiyo kwenye michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika

Msimu wa Ligi Kuu 2018/19 unatarajiwa kumalizika May 26 2019 huku Simba, mabingwa watetezi wakiwa bado na michezo 16 ambayo watalazimika kuicheza katika kipindi cha mwezi mmoja na siku kadhaa

“Tutafanyia kazi ratiba ya Simba ili kuhakikisha haiathiri kalenda yetu,” alisema Wambura

“Tutaandaa ratiba maalum kwa klabu ya Simba ili kuhakikisha wanamaliza michezo yao yote bila kuathiri kalenda ya TFF ambapo ligi inapaswa kumalizika mwezi Mei”

Juzi Bodi ya ligi ilisogeza mbele mchezo wa Simba dhidi ya Biashara United ili kuwapa nafasi wawakilishi hao wa nchi wafanye maandalizi ya mchezo wa pili wa robo fainali dhidi ya TP Mazembe

Simba inatarajiwa kuondoka kesho Ijumaa kuelekea DR Congo tayari kwa mchezo huo utakaopigwa uwanja wa TP Mazembe keshokutwa, April 13 2019