Dewji aitabiria Simba nusu fainali ligi ya mabingwa

Mfanyabiashara maarufu nchini aliyewahi kuifadhili timu ya soka ya Simba kwa mafanikio makubwa, Azim Dewji ameitabiria makubwa klabu hiyo katika mchezo wa marudiano wa robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) mwishoni mwa wiki hii huko mjini Lumbumbashi.

Dewji amesema Simba ya mwaka huu ni `moto’ na ina uwezo wa kuwang’oa Mazembe kutokana na kuundwa na wachezaji wenye vipaji na ari ya kupata matokeo chanya.

Akizungumza jana mjini Dar es Salaam, Dewji aliyeifikisha Simba fainali za Kombe la Shirikisho Afrika (CAF) mwaka 1993, alisema kitu pekee kinachopaswa kufanywa na wachezaji na viongozi wa Simba ni kuondoa mchecheto wa mchezo na badala yake kuelekeza nguvu katika mchezo wa marudiano

“Ni kweli Mazembe ni timu ngumu na kongwe. Ukiangalia ina historia kubwa Afrika na ndani ya miaka hii kumi tumeshuhudia ikitwaa ubingwa tofauti wa michuano ya CAF mara tano. Ni rekodi bora sana, lakini pamoja na ubora wao, nikiangalia ubora na uthubutu wa wachezaji wa Simba, naona vijana wetu wanaweza kufanya kweli,” Dewji amenukuliwa na Bin Zubeiry

“Wachezaji wa sasa wa Simba nawafananisha na wale wa enzi zile tunafika fainali CAF.

“Walikuwa wanajituma sana uwanjani. Na hawa ukiwaangalia wana kila kitu kinachoweza kuwaduwaza Mazembe kwao.

“Angalia walivyowakimbiza hapa Dar es Salaam, kwa kawaida Mazembe si wa kujiangusha hivyo, lakini uliona katika mchezo wa kwanza, walizidiwa sana ila bahati haikuwa kwa Simba.

“Na hata hao wanaobeza penalti ya John Bocco watambue Simba hii ni moto wa kuotea mbali na usishangae kuona mpira umetangulia Lubumbushi na wachezaji wanakwenda kumalizia kazi ya kuandika historia zaidi kwa soka ya Tanzania,” alisema

Akizungumzia tukio la klabu hiyo kupinga kubadilishiwa mwamuzi wa mchezo wa marudiano dhidi ya Mazembe, alisema jambo hilo litawarejesha mchezoni wachezaji, lakini pia kuongeza umakini wa waamuzi katika mchezo huo.

“Hata kama CAF hawatabadilisha uamuzi huo, mwamuzi aliyepangwa (Janny Sikazwe wa Zambia) atakuwa makini zaidi na kizuri ni kwamba hatataka kuharibu sifa zake zilizomwezesha kuchezesha michuano karibu yote mikubwa duniani.

“Amechezesha Kombe la Dunia mara mbili, Kombe la Mataifa ya Afrika mara mbili, pia fainali za Klabu Bingwa ya Dunia, achilia mbali hii michuano ya klabu Afrika,” alisema Dewji aliyewataka Watanzania kuendelea kuwaunga mkono wawakilishi hao wa taifa.

Katika mchezo wa kwanza mwishoni mwa wiki iliyopita jijini Dar es Salaam, timu hizo hazikufungana, hivyo kuzifanya timu zote kuwa na nafasi ya kusonga mbele hatua ya nusu fainali, matokeo ya mwishoni mwa wiki yakiwa mwamuzi wa mwisho.

Simba kwenda Congo kwa Ndege ya kukodi

Kikosi cha mabingwa wa soka Tanzania Bara, Simba kitaondoka Ijumaa asubuhi kuelekea Lubumbashi Congo kuifuata TP Mazembe kwenye mchezo wa marudiano robo fainali ya ligi ya mabingwa barani Afrika

Msafara wa Simba utajumuisha mashabiki wa timu hiyo ambao wameendelea kukamilisha taratibu za safari hiyo

Msemaji wa Simba Haji Manara amesema wataondoka Ijumaa asubuhi na timu itarejea jijini Dar es salaam Jumamosi jioni baada ya mchezo

“Tutakwenda kibabe DR Congo na tutaondoka na kundi la mashabiki wetu na tutaishangaza Afrika Jumamosi ijayo, Ndege itaondoka asubuhi ya Ijumaa Aprili 12, 2019 na itarejea nchini Jumamosi jioni mara tu baada ya mchezo huo,” amesema Manara

Baada ya kulazimishwa suluhu ya bila kufungana kwenye mchezo uliopigwa uwanja wa Taifa, Simba inahitaji kushinda au hata kupata matokeo ya sare ya mabao ili iweze kusonga mbele

Mkufunzi wa Simba Patrick Aussems amesema wanayo nafasi ya kupata matokeo ugenini na kutinga nusu fainali ya michuano hiyo mikubwa barani Afrika kwa ngazi ya vilabu

Wawa nje wiki moja

Beki kisiki wa Simba Paschal Serge Wawa ataukosa mchezo wa pili wa robo fainali ligi ya mabingwa dhidi ya TP Mazembe utakaopigwa Jumamosi, April 13 huko Lubumbashi DR Congo

Wawa alipata majeraha ya kifundo cha mguu kwenye mchezo wa kwanza uliopigwa uwanja wa Taifa ambao ulimalizika kwa suluhu ya bila kufungana

Uongozi wa Simba umethibitisha kuwa Wawa atakaa nje kwa wiki moja

Wawa hatajumuishwa kwenye kikosi cha Simba kitakachoondoka Alfajiri ya kesho kuelekea Lubumbashi

BIKOSPORTS yakabidhi tuzo kwa Bocco, Aussems

Kampuni ya Bikosports leo imekabidhi tuzo za mchezaji bora na kocha bora wa mwezi March 2019 ambazo zote zilienda kwa klabu ya Simba

Tuzo ya mchezaji bora ilichukuliwa na nahodha John Bocco wakati ya kocha bora ilichukuliwa na Patrick Aussems

Wote wamekabidhiwa kitita cha Tsh Milioni moja pamoja na Ngao Maalum ya utambulisho

Aussems atamba, hajawahi kupoteza robo fainali, aahidi ushindi Congo

Kocha Mkuu wa Simba, Mbelgiji Patrick Aussems, amesema kuwa katika historia yake ya kufundisha soka, hajawahi kushindwa baada ya kutinga robo fainali.

Aussems ambaye msimu huu amevuka malengo kwa kuipeleka Simba robo fainali, amesema baada ya mchezo wa kwanza dhidi ya TP Mazmebe kumalizika kwa suluhu ya bila kufungana, anaamini mchezo wa marudiano utakaopigwa April 13 Simba ina nafasi ya kushinda kama ilivyo kwa wapinzani wao TP Mazembe

“Katika historia yangu ya soka na timu ambazo nimewahi kufundisha, nilizivusha hatua ya robo fainali, ndio maana sina hofu na hili kwa uwezo wa Mungu tutafanikiwa,” amesema.

Aussems amesema anatambua ni makosa madogo waliyoyafanya katika mchezo wa kwanza na kwamba amejipanga kikamilifu kukabiliana na mchezo huo.

“Natambua kuwa Watanzania na mashabiki wa Simba walikuwa na hofu pengine tungefungwa mabao mengi na TP Mazembe katika mchezo uliopita, lakini wameshuhudia namna tulivyopambana, sidhani kama tunaweza kushindwa mchezo wa marudiano.

“Pengine hofu kubwa ni kwa sababu tutakuwa ugenini, mimi naamini kuwa mpira ni dakika 90, hata tuwe wapi ni plani yangu na juhudi za wachezaji ndizo zitakazoleta matokeo mazuri,” alisema Aussems.

Tunaweza kupata ushindi Lubumbashi – Kagere

Mshambuliaji wa Simba, Meddie Kagere, amewaondoa wasiwasi mashabiki wa Simba kuwa waiamini timu yao kwani kupata ushindi Lubumbashi, Congo inawezekana.

Jumamosi, Simba ililazimishwa suluhu ya ila kufungana dhidi ya TP Mazembe, kwenye mchezo wao wa robo fainali uliochezwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar res Salaam.

Matokeo hayo yanailazimu Simba kupata ushindi au sare yoyote ya mabao ugenini ili iweze kutinga nusu fainali

Mchezo wa marudiano utapigwa Aprili 13, nchini Congo kwenye Uwanja wa TP Mazembe.

Kagere alisema anaamini kwa juhudi walizonazo, bado wana nafasi ya kushinda mchezo wao huo.

Alisema kiwango chao si kibaya na hata juzi walicheza vizuri, wakienda ugenini hata kama watatoka sare haitakuwa mbaya.

“Mazembe ni timu kubwa na tulicheza vizuri ila tulikosa bahati ya kupata mabao, tayari tunawajua vizuri hivyo tutacheza zaidi ya tulivyopambana nyumbani, mashabiki wasikate tamaa,” Kagere amenukuliwa na Bingwa

Simba inatarajiwa kuondoka jijini Dar es salaam Alfajiri ya Alhamisi kuelekea nchini Congo tayari kwa mchezo huo

Simba yajipanga kuhuisha mikataba nyota nane

Ligi Kuu ya Tanzania Bara inamalizika mwezi ujao na tayari michakato ya usajili wa wachezaji imeanza kushika kasi

Nyota nane wa kikosi cha Simba mikataba yao inamalizika mwishoni mwa msimu ambapo Mwenyekiti wa Simba Swedy Mkwabi amesema wako mbioni kuanza mazungumzo ya kuhuisha mikataba ya wachezaji hao

Miongoni mwa nyota ambao mikataba yao inamalizika mwishoni mwa msimu ni pamoja na Emmanuel Okwi, John Bocco, Jonas Mkude, Aishi Manula, Erasto Nyoni, James Kotei, Asante Kwasi na Shomari Kapombe

“Tunasubiri ripoti ya Mwalimu Aussems ili tuanze michakato ya usajili. Lakini bila shaka, wachezaji wengi tutaendelea nao” amesema

“Hakuna mchezaji yeyote ambaye mkataba wake wa kuitumikia Simba utakuwa umemalizika na tumempa ruhusa ya kuondoka kwa maana ya kwenda kujiunga na timu nyingine wote tuna mipango nao na tunaimani watasaini mikata mipya ya kubaki hapa.

“Bodi bado haijazungumza na mchezaji yeyote, ambaye mkataba wake unamalizika kutokana na majukumu ya mechi za kimataifa ambazo tunacheza mfululizo, lakini nadhani tutakaa nao na mambo yatakwenda sawa kwa pande zote mbili tutakubaliana”

Bodi ya ligi yaahirisha mchezo wa Simba vs Biashara United

Mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara kati ya Simba dhidi ya Biashara United uliokuwa upigwe leo katika uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro, umeahirishwa ili kuipa nafasi Simba kujiandaa na mchezo dhidi ya TP Mazembe

Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi Boniface Wambura amesema mchezo huo umeahirishwa kutokana na Simba kukabiliwa na mchezo huo muhimu wa marudiano robo fainali ya ligi ya mabingwa

Simba sasa itachuana na Biashara baada ya kumalizana na TP Mazembe April 13 2019

Wekundu wa Msimbazi wameendelea na mazoezi kwenye uwanja wa Boko Veterans kujiandaa na mchezo huo utakaopigwa Lubumbashi, DR Congo