Simba ilivyoizidi ujanja AS Vita kwa Tuyisenge

Uongozi wa klabu ya Simba tayari umemalizana na mshambuliaji wa Gor Mahia Jacques Tuyisenge ambaye pia alikuwa akiwaniwa na AS Vita Club ya DR Congo

Baada ya kumpoteza mshambuliaji wake Jean Mark Makusu aliyetimkia nchini Morocco, Vita ilikuwa mbioni kumsajili Tuyisenge kuchukua nafasi yake

Hata hivyo Meddie Kagere aliyekuwa ‘pacha’ wa Tuyisenge katika klabu ya Gor Mahia ambaye pia ni pacha wake katika kikosi cha timu ya Taifa ya Rwanda, amechangia kwa kiasi kikubwa kumshawishi Tuyisenge kutua Simba

Simba imempa Tuyisenge mkataba wa awali wa miaka miwili akitarajiwa kuanza kazi mwishoni mwa msimu

Tuyisenge alikutana na mabosi wa Simba juzi usiku katika kikao ambacho kilikuwa na mafanikio kwa pande zote mbili kufikia makubaliano

Tetesi za soka barani Ulaya Alhamisi hii, Hudson-Odoi, Sanchez, Rashford, Maguire, Chilwell

Barcelona wapo tayari kuwapa Manchester United kiungo Philippe Coutinho, 26, ama Malcom, 22, kama sehemu ya ofa ya kumnasa mshambuliaji Marcus Rashford, 21. (Mundo Deportivo, via Mail)
Klabu ya Borussia Dortmund inasisitiza kuwa haina mpango wa kumuuza mchezaji wao raia wa Uingereza Jadon Sancho, 19, ambaye amekuwa akihusishwa na Manchester United. (Mirror)
Chelsea wanaweza wakasikiliza ofa za usajili za zaidi ya Pauni milioni 43 ili kumuachia mshambuliaji kinda wa Uingereza Callum Hudson-Odoi, 18. (Sport Bild, via Metro)

Leicester hawapo tayari kuwatoa mabeki wake Harry Maguire, 26, na Ben Chilwell, 22, ambao wamekuwa wakinyemelewa na vilabu vikubwa vya Manchester United na Manchester City. (Mirror)
Manchester United hawana mpango wa kumuuza mchezaji wao anayepokea mshahara mkubwa zaidi, Alexis Sanchez, 30, licha ya kutoonesha makali uwanjani na ripoti kuwa suala la mshahara wake linatatiza mapatano ya mkataba mpya na kipa David De Gea. (London Evening Standard)

Beki wa Liverpool Dejan Lovren ananyemelewa na vilabu vikongwe vya Italia, Roma, Napoli na AC Milan ili wamsajili mwishoni mwa msimu. (Mirror)
Manchester City ni miongoni mwa vilabu ambavyo vinamfuatilia kwa karibu winga wa Swansea na Wales Dan James, 21. (Sun)

Mshambuliaji kinara wa klabu ya Tottenham Harry Kane, 25, amesema anataka kucheza kwenye ligi ya Marekani NFL “ndani ya miaka 10 au 12 ijayo”. (ESPN)

Kiungo wa Liverpool na Serbia Marko Grujic, 22, ambaye yupo kwa mkopo katika klabu ya Hertha Berlin, anataka kusalia kwenye klabu hiyo ya Ujerumani walau kwa mwaka mmoja zaidi. (Liverpool Echo)
Mshambualiaji wa raia wa Paraguay Sergio Diaz, 21, atasalia Real Madrid baada ya klabu ya Corinthians ya Brazil, ambako amekuwa kwa mkopo msimu huu kuamua kuwa hawatamnunua. (Marca)

Wengine wawili waingia anga za Simba Today

Simba imepania kwelikweli kuboresha kikosi chake kwa ajili ya msimu ujao! Hilo limedhihirika kutokana na michakato ya usajili kuanza mapema

Juzi Jacques Tuyisenge alikuwa nchini kumalizana na mabingwa hao wa Tanzania Bara akitarajiwa kujiunga nao mwishoni mwa msimu wakati huo huo nahodha wa Yanga Ibrahim Ajib nae akiwa njiani kurejea nyumbani

Anayefuatia ni beki kisiki wa Azam Fc Yakubu Mohammed. Inaelezwa Yakubu tayari amefikia makubaliano ya awali na uongozi wa Simba na atamwaga wino mwishoni mwa msimu

Kakolanya nae safi

Mlinda lango wa Yanga Beno Kakolanya aliyegoma kuitumikia timu hiyo kutokana na ‘ukata’, nae anasubiri kumalizwa kwa mgogoro baina yake na uongozi wa timu hiyo

Kakolanya ameitaka Yanga ivunje mkataba wake na tayari ameliwasilisha suala hilo kwa TFF

Kakolanya anatarajiwa kujiunga na Simba akiwa mchezaji huru

Wakati huo huo Simba inaendelea kumjaribu kiungo mkabaji Jean Vital Ourega aliyetokea nchini Ivory Coast

Ajib, Tuyisenge watajwa Msimbazi

Nahodha wa Yanga Ibrahim Ajib huenda akarejea katika klabu ya Simba, mahali alipokuza jina lake kwenye soka

Inaelezwa Ajib ambaye mkataba wake na Yanga unamalizika mwishoni mwa msimu, tayari amesaini mkataba wa awali kurudi Msimbazi

Ajib alisajiliwa na Yanga mwaka juzi akipishana na Haruna Niyonzima aliyetua Msimbazi

Simba tayari imeanza mkakati wa kukiboresha kikosi chake kwa ajili ya msimu ujao ambapo mbali na Ajib, mabingwa hao wa Tanzania Bara inaelezwa tayari wametua nchini Kenya kumnyakua mshambuliaji wa Gor Mahia, Jacques Tuyisenge

Tuyisenge aliyeisaidia Gor Mahia kutinga robo fainali ya kombe la Shirikisho Barani Afrika, ataondoka Gor Mahia mwishoni mwa msimu mkataba wake utakapokuwa umemalizika

Msimu uliopita Tuyisenge alikuwa pacha wa Meddie Kagere katika kikosi cha Gor Mahia kilichokuwa kikinolewa na Dylan Kerr

DORTMUND: na Callum Hudson Odo

Klabu ya Borussia Dortmund inajipanga kuanza mazungumzo na klabu Chelsea ili kuona uwezekano wa kumpata mshambuliaji wake Callum Hudson Odoi ili kuwa mbadala wa Jadon Sancho endapo atatimkia Man United.
.

Licha ya kusisitiza kuwa hawatamuuza nyota huyo BVB wanahofia huenda wakalazimika kumpiga bei ifikapo mwishoni mwa msimu huu ikiwa kama Sancho atahitaji kuondoka.

DISMAS TEN: Afunguka kuhusu Usajili wa NDEMLA

Kwa siku za karibuni kupitia kurasa zake za mitandao ya kijamii, Msemaji wa klabu ya Yanga Dismas Ten amekuwa akimposti kiungo wa Simba Said Khamis Ndemla huku akiweka jumbe zinazoashiria kuwa huenda mabingwa hao wa kihistoria wanaiwania sahihi ya kiungo huyo kwa ajili ya msimu ujao

Ndemla nusura asajiliwe na Yanga katika usajili wa mwanzoni mwa msimu huu kabla hajaamua kubaki Simba kwa kuongeza mkataba wa mwaka mmoja

Jana Ten alifunguka kuhusu tetesi za Yanga kumuwania Ndemla ambapo amekiri kuwa kiungo huyo ana uwezo mkubwa lakini ana bahati mbaya hapati nafasi katika klabu yake ya Simba

“Ndemla ni mchezaji mzuri sana. Mtu yeyote ukimuuliza katika wachezaji wa Tanzania wenye vipaji hawezi kukosa kumtaja Ndemla,” amesema Ten

“Ndemla mimi ni rafiki yangu, suala la kusajili au kutosajiliwa na Yanga hilo linahusu benchi la ufundi na Kamati yetu ya usajili. “

“Yote yanaweza kusemwa mwisho wa msimu lakini kwa sasa hivi huwezi kuzungumza lolote lakini anabaki kuwa ni mchezaji mwenye kipaji na kila mtu anaona”

“Amekuwa ni mchezaji mwenye mwenendo mzuri licha ya kuwa sasa hapati nafasi kwenye timu yake”

Wakati msimu ukielekea ukingoni tayari timu zimeanza ‘kupigana vikumbo’ kuwania wachezajia ambao mikataba yao inaelekea ukingoni

MAN UNITED Yamfuatilia Kiungi Huyu

Klabu ya Manchester United ya Uingereza inamfuatilia kiungo wa kati wa Barcelona na timu ya Taifa Croatia Ivan Rakitic, 30 ifikapo mwishoni mwa msimu huu (Mail)Hata hivyo huenda wakamkosa kutokana na yeye kusema kamwe kwasasa hawezi kuondoka klabuni hapo bado anatamani kuendelea kukipiga kwenye miamba hiyo ya Hispania

USAJILI: Yanga wakamilisha usajili wa BOBAN

Imebainika kocha Mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera ndiye aliyependekeza kusajiliwa kwa kiungo wa African Lyon, Haruna Moshi ‘Boban’.

Tayari Yanga imeshamalizana na Boban ambaye amesaini mkataba wa miezi sita.

Zahera amebainisha kuvutiwa na Boban alipomuona kwenye mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara kati ya African Lyon dhidi ya JKT Tanzania

Baada ya kuvutiwa na uwezo wake, Mcongomani huyo aliwaagiza viongozi wa Yanga kumfuatilia na kukamilisha usajili wake.

Boban ana uzoefu wa soka la Tanzania, na ni miongoni mwa wachezaji walion’gara kwenye kikosi cha African Lyon msimu huu.