Mwishoni mwa wiki hii Yanga inakabiliwa na mchezo muhimu wa robo fainali kombe la Azam (ASFC) dhidi ya Alliance Fc utakaopigwa March 30 kwenye uwanja wa CCM Kirumba
Kocha Msaidizi wa Yanga Noel Mwandila amesema ni lazima wajiandae kikamilifu kuhakikisha wanapata matokeo yatakayo-wapeleka hatua ya nusu fainali
Kocha huyo anayekaimu nafasi ya Zahera, amesema wanaufahamu ubora wa Alliance Fc, kupitia michezo miwili ambayo wamekutana nao kwenye ligi, wanafahamu nini wafanye ili waweze kupata matokeo
“Hatuna cha kupoteza kuelekea mchezo huo tupo makini kila idara tunapambana kuhakikisha tunapata matokeo uwanja wa Kirumba, sio kazi rahisi kwetu kwani tunakutana na wapinzani ambao ni bora kila idara,” Mwadila amenukuliwa na Mwanaspoti
“Wana nguvu, wachezaji vijana na wana kasi tunatarajia kukutana na changamoto kubwa kutoka kwao lakini tumejipanga kukabiliana nazo kwasababu tunatambua umuhimu wa mchezo huo, Ngassa na Makambo wanakasi ya kukimbia na mipira Tambwe atakaa tayari kwaajili ya kumalizia mipira mirefu itakayokuwa inapigwa”
Mwandila ameongeza kuwa hawawezi kucheza mchezo sawa na wapinzani wao wanatarajia kutumia mbinu mbadala ambayo itawasaidia wao kupata matokeo kama ilivyokuwa michezo iliyopita na kuweka wazi kuwa lengo lao ni kupata matokeo mapema ili kuwatoa mchezoni wapinzani wao.
Yanga imekutana mara mbili na Alliance Fc katika michezo ya ligi na Yanga kushinda yote
Kwenye mchezo wa kwanza uliopigwa uwanja wa Taifa Yanga ilishinda mabao 3-0 kabla ya kushinda 1-0 katika mchezo wa marudiano uliopigwa dimba la CCM Kirumba
Itarejea mkoani Mwanza tena katika uwanja wa CCM Kirumba dhidi ya vijana hao machachari kuwania tiketi muhimu ya kutinga nusu fainali kombe la FA (ASFC)
Baada ya mchezo huo, Yanga itaendelea kutumia dimba la CCM Kirumba kwa michezo yake yote ya nyumbani wakati uwanja wa Taifa utakapokuwa umefungwa kupisha michuano ya kombe la AFCON ya vijana