Full Time: Yanga 1-0 African Lyon

Mabingwa wa kihistoria Tanzania, Yanga wameendelea kujichimbia kileleni mwa msimamo wa ligi kuu ya Tanzania Bara baada ya kuichapa African Lyon bao 1-0 katika mchezo uliopigwa dimba la Sheikh AMri Abeid mkoani Arusha.

Bao pekee la Yanga lilipatikana kwenye dakika ya 64 likiwekwa kimiani na beki ‘mbishi’ Abdallah Shaibu ‘Ninja’ aliyeunganisha kwa kichwa mpira wa adhabu uliopigwa na Ibrahim Ajib ‘Miguu ya dhahabu’

Hilo lilikuwa bao la pili kwa Shaibu msimu huu huku Ajib akiendelea kujiongezea ‘assists’ sasa zikifika 12

Licha ya kukabiliwa na changamoto ya uwanja, Yanga ilicheza vizuri hasa katika kipindi cha pili.

Mabingwa hao wa kihistoria walipata pigo katika mchezo huo baada ya kuwapoteza wachezaji wake wawili kutokana na majeruhi.

Jaffard Mohammed alishindwa kuendelea na mchezo baada ya kuumia katika dakika ya 14 na nafasi yake kuchukuliwa na Deus Kaseke.

Mlinda lango tegemeo Ramadhani Kabwili nae aliumia nyonga na kushindwa kuendelea na mchezo katika dakika ya 38 na nafasi yake kuchukuliwa na Klaus Kindoki

Kabwili alikimbizwa Hospitalini kupatiwa matibabu zaidi

Ushindi huo umeikita Yanga kileleni mwa msimamo wa ligi kwa tofauti ya alama saba baada ya kufikisha alama 47

Yanga itazidi kukimbiza na wachezaji Hawahawa

Yanga haikufanya usajili wa maana katika dirisha dogo la lililofungwa wiki iliyopita na kuacha malalamiko mengi kwa viongozi wa timu hiyo.

Kiungo Haruna Moshi ‘Boban’ ndio mchezaji pekee ambaye alipendekezwa na Kocha Mwinyi Zahera aliyefanikiwa kusajiliwa.

Zahera aliutupia lawama uongozi wa Yanga kwa kushindwa kukamilisha usajili wa wachezaji wengine wanne huku akikerwa na kitendo cha uongozi wa timu hiyo kumdanganya kuwa usajili wa wachezaji hao ungekamilika

Lakini Mcongomani huyo amesema atatumia wachezaji waliopo ingawa hawezi kutoa ahadi ya kutwaa ubingwa.

Hata hivyo kushindwa kwa usajili wa wachezaji wapya kunaweza kuwa chachu ya kuwafanya wachezaji waliopo waongeze bidii zaidi ili kumshawishi kocha juu ya uwezo wao.

Ujio wa wachezaji wapya pengine ungeweza kuwaondoa baadhi ya wachezaji kikosini lakini sasa watakuwa na nafasi nyingine ya kumshawishi Zahera

Wachezaji hawa waliopo katika kikosi cha Yanga hawapaswi kukatishwa tamaa kwa kuhofia kuwa timu haitafanya vizuri eti kwa kuwa usajili uliopendekezwa haukufanikiwa

Hakuna ubishi kama wachezaji waliotakiwa na Zahera wangesajiliwa, Yanga ingekuwa moto zaidi lakini hata sasa ikiwa na hawa wachezaji waliopo Yanga haikamatiki

Wachezaji waliopo wameiwezesha Yanga kukaa kileleni mwa msimamo wa ligi wakiongoza kwa tofauti ya alama nne dhidi ya Azam FC na alama 17 dhidi ya Simba inayojinasibu kuwa na kikosi cha zaidi ya Bil 1

Kama ilivyowashangaza wale ambao mwanzoni mwa msimu walikuwa wakiamini na wengine kudiriki kusema ‘Msimu huu Yanga inapigania isishuke daraja’, basi mwishoni mwa msimu pia Yanga itawashangaza wale wanaoamini kushindikana kwa usajili wa wachezaji wapya kutaigharimu timu hiyo.

Kitu pekee kinachoweza kuigharimu Yanga sasa ni labda akiondoka kocha Mwinyi Zahera ambaye amekuwa akifanya kazi ya ziada kuhakikisha timu inafanya vizuri.

Kikosi cha Yanga vs Ruvu Shooting

1. Ramadhani Kabwili
2. Paulo Godfrey
3. Haji Mwinyi
4. Andrew Vicent
5. Abdallah Shaibu
6. Feisal Salum
7. Ibrahim Ajib
8. Papi Tshishimbi
9. Heritier Makambo
10. Amissi Tambwe
11. Jaffar Mohammed

SUB
Klaus Kindoki
Juma Abdul
Gadiel Michael
Cleofas Sospeter
Maka Edward
Pius Buswita
Deus Kaseke

USAJILI: Yanga wakamilisha usajili wa BOBAN

Imebainika kocha Mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera ndiye aliyependekeza kusajiliwa kwa kiungo wa African Lyon, Haruna Moshi ‘Boban’.

Tayari Yanga imeshamalizana na Boban ambaye amesaini mkataba wa miezi sita.

Zahera amebainisha kuvutiwa na Boban alipomuona kwenye mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara kati ya African Lyon dhidi ya JKT Tanzania

Baada ya kuvutiwa na uwezo wake, Mcongomani huyo aliwaagiza viongozi wa Yanga kumfuatilia na kukamilisha usajili wake.

Boban ana uzoefu wa soka la Tanzania, na ni miongoni mwa wachezaji walion’gara kwenye kikosi cha African Lyon msimu huu.

Full Time : Yanga 2-1 Biashara United

Mabingwa wa kihistoria wa Tanzania Yanga wameendeleza ubabe kwenye ligi kuu ya Tanzania Bara baada ya kuilaza Biashara United mabao 2-1 katika mchezo uliopigwa uwanja wa Taifa leo.

Huo ulikuwa ushindi wa 13 kwa Yanga katika michezo 15 waliyocheza, wakitoka sare michezo miwili tu

Biashara United iliandika bao la kuongoza kwenye dakika ya 38 baada ya kufanya shambulizi la kushitukiza lililomaliziwa vyema na Mangalo

Yanga imedhihirisha kuwa ni timu isiyofungika kwa urahisi kwani katika kipindi cha pili ilipeleka mashambulizi mengi langoni kwa Biashara United waliokuwa wakicheza kwa kujihami

Bao la kusawazisha la Yanga liliwekwa kambani na Abdallah Shaibu ‘Ninja’ ambaye kwenye mchezo wa leo kocha Mwinyi Zahera alimchezesha kama kiungo

Shaibu alimalizia vyema pasi murua ya Amisi Tambwe aliyeingia katika kipindi cha pili.

Aliyeipa Yanga matokeo muhimu sio mwingine zaidi ya Heritier Makambo aliyefunga bao safi kwenye dakika ya 80 na kuihakikishia Yanga alama tatu muhimu

Makambo aliyechaguliwa kuwa mchezaji bora wa mwezi uliopita, amefikisha mabao nane sasa akiwa nyuma ya Eliud Ambokile wa Mbeya City kwa tofaurti ya bao moja tu.

Yanga imerudi kileleni mwa msimamo wa ligi baada ya kufikisha alama 41, alama mbili zaidi ya Azam Fc iliyo nafasi ya pili

Aidha matokeo hayo yanaifanya Yanga izidi kuitimulia vumbi Simba sasa ikiachwa kwa tofauti ya alama 14 licha ya kuwa na michezo mitatu ya kiporo

Tshishimbi, Yondani kuongeza Nguvu kikosini Yanga

Nahodha wa Yanga Kelvin Yondani amerejea kikosini baada ya kuwa nje kwa zaidi ya wiki tatu akisumbuliwa na majeraha ya enka.

Hivi karibuni Yondani na mlinda lango Beno Kakolanya waliviteka vyombo vya habari za michezo baada ya kudaiwa wamegoma kucheza wakishinikiza walipwe madai yao.

Hata hivyo beki huyo mkongwe alikanusha taarifa hizo na kusisitiza alikuwa akisumbuliwa na majeraha ya enka na uongozi wa Yanga ulikuwa na taarifa zake

Naye kiungo Mcongomani Papi Tshishimbi amerejea kikosini baada ya kupona majeraha.

Tshishimbi, Yondani na winga mpya Reuben Bomba walihudhuria mazoezi ya jana ya kikosi cha Yanga yanayofanyika Chuo cha Polisi, Kurasini jijini Dar es salaam.

Yanga 1-2 Sumbawanga Fc | Mechi ya kirafiki

Kikosi cha Yanga kimepoteza mchezo wa kirafiki leo baada ya kuchapwa mabao 2-1 na Sumbawanga United kwenye mchezo uliopigwa dimba la Mandela

Bao pekee la Yanga lilifungwa na Thabani Kamusoko kwenye dakika ya 40.

Mchezo huo ulikuwa maalum kwa ajili ya wakazi wa Sumbawanga ambao kwa muda mrefu hawajashuhudia timu zinazoshiriki ligi kuu.

Yanga inatarajiwa kurejea mkoani Mbeya tayari kwa safari ya kurudi jijini Dar es salaam.

Jumapili Disemba 09 itacheza na Biashara United kwenye mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara.

KOCHA ZAHERA ANAJUA MPIRA

Kocha Mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera amedhihirisha yeye ni Mwalimu wa mpira baada ya kufanikisha timu yake kuibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Tanzania Prisons leo.

Mabadiliko aliyofanya kwenye dakika ya 72 kwa kumtoa beki Juma Abdul na kumuingiza mshambuliaji Amisi Tambwe yaliwashangaza wengi tena wakati huo Yanga ikiwa nyuma kwa bao 1-0

Lakini baada ya dakika 90 za mchezo kumalizika huku ubao ukisoma Prisons 1-3 Yanga, imedhihirisha Mcongomani huyo alifanya uamuzi sahihi wa kumuingiza Tambwe.

Tambwe alihusika katika mabao yote matatu, akifunga mawili huku pasi yake ikizaa mkwaju wa penati uliowekwa kambani na Ibrahim Ajib.

Zahera aliweza kusoma taswira ya mchezo huo na kubaini kuwa kumuingiza Tambwe kungeipa matokeo Yanga.

Aidha Zahera amefanikiwa kuwajenga wachezaji wake kisaikolojia kiasi kwamba hawapendi kabisa kupoteza mchezo.

Upambanaji walio-onyesha kwenye kipindi cha pili unadhihirisha kuwa wachezaji wa Yanga wameiva na haitakuwa rahisi kwa timu yoyote kuifunga Yanga msimu huu.

Full Time : Yanga 3-1 Tanzania Prisons

Ndio! Mabingwa wa kihistoria wa Tanzania Yanga wameilaza Tanzania Prisons mabao 3-1 katika dimba lao la Sokoine katika mchezo ambao nusura uvurugwe na maamuzi mabovu

Tanzania Prisons ilipewa penati ya utata mwishoni mwa kipindi cha kwanza na Jumanne Elifadhili akaifungia timu hiyo bao la kuongoza.

Penati hiyo ilipingwa vikali na wachezaji wa Yanga kupelekea Ajib, Chikupe na Ngasa kuonyeshwa kadi za njano baada ya kumzonga mwamuzi.

Kabla ya tukio hilo Ibrahim Ajib na Heritier Makambo walifanyiwa madhambi ndani ya eneo la hatari la Prisons lakini mwamuzi hakuchukua hatua yoyote.

Presha ya mchezo ilipelekea Mrisho Ngasa kutolewa nje kwa kadi nyekundu baada ya kumpiga kichwa Laurance Mpalile ambaye naye pia alitolewa nje baada ya kufanya tukio hilo hilo

Kipindi cha pili Yanga iliingia na kasi kubwa ikisaka bao la kusawazisha.

Mabadiliko ya kocha Mwinyi Zahera kwa kumtoa Juma Abdul na kumuingiza Amisi Tambwe yaliinufanisha zaidi Yanga kwani Tambwe aliyecheza kwa dakika 18 ndiye nyota wa mchezo huo.

Kwenye dakika ya 76 Yanga ilipata penati baada ya mlinzi wa Prisons kuunawa mpira uliokuwa umepigwa na Heritier Makambo ndani ya eneo la hatari

Makambo alipokea pasi kutoka kwa Tambwe. Ajib aliisawazishia Yanga kupitia penati hiyo.

Tambwe akaifungia Yanga bao la pili kwenye dakika ya 85 akiunganisha krosi ya Matheo Anthony kisha akafunga la tatu kwenye dakika za majeruhi baada ya kutumia vyema makosa ya mlinzi wa Prisons.

Wachezaji wa Yanga, kocha Mwinyi Zahera na benchi lake la ufundi wanastahili pongezi kwa kazi kubwa waliyoifanya mkoani Mbeya leo.

Yanga imeibuka na ushindi uliopatikana katika mazingira magumu sana, kuanzia hali ya uwanja baada ya mvua kubwa kunyesha na matukio ya ndani ya uwanja.

Ushindi huo umeikita Yanga kileleni mwa msimamo wa ligi baada ya kufikisha alama 38, alama tano mbele ya Azam Fc inayoshuka dimbani kesho.

Aidha Yanga imeiacha Simba kwa alama 11!