Yanga ilitarajiwa kurejea jijini Dar es Salaam jana Jumatatu kutoka Bukoba baada ya kumaliza mechi zake za Kanda ya Ziwa kibabe kwa kuvuna alama zote sita ilizozifuata, lakini Kocha Mkuu, Mwinyi Zahera ameamua kutoa masharti mazito.
Kocha huyo kutoka DR Congo, ameamua kuwarahisishia kazi Kamati ya Usajili ya klabu hiyo kwa kulegeza masharti ya kuwaacha wachezaji wa kigeni dirisha dogo ili kuhakikisha inawanasa wachezaji wazawa ambao anaamini wataibeba timu.
Lakini katikati ya masharti hayo kwa mabosi wake, Zahera ametoa tahadhari mapema kwa nyota wapya wanaotamani kuichezea Yanga ama watakaosajiliwa, ni lazima wawe watu wa mazoezi kwelikweli kwani hataki wavivu.
Zahera alisema usajili wa nyota wazawa utasaidia pia kuipunguzia klabu gharama, lakini amebaini ni vijana wenye vipaji vya soka isipokuwa wanaangushwa na tabia za uvivu hasa wa mazoezi.
Kocha huyo aliyeiongoza Yanga katika mechi 12 za msimu huu ikishinda 10 na kutoka sare mbili, alimtolea mfano Ibrahim Ajib ‘Kadabra’ kwa kusema awali alikuwa anampa nafasi kwa kuwa alikuwa anaonyesha jitihada kuanzia mazoezini, lakini baada ya kuanza kutegea ameamua kumkalisha benchi.
“Yanga kwa sasa imeyumba, lazima mchezaji anayekuja atambue hali ya klabu na awe tayari kustahimili, isije ikawa kama alivyofanya Obrey Chirwa kutukimbia tukiwa na uhitaji na huduma yake kisa Yanga haina pesa,” alisema Zahera.
Kauli ya Zahera imekuja huku kukiwa na taarifa, mabosi wa klabu hiyo wamekuwa katika mchakato wa kuwanasa mastraika wakali, Eliud Ambokile anayekipiga Mbeya City, Sixtus Sabilo na Bigirimana Blaise wa Stand United.
Kama kweli wachezaji hao wanahamu ya kutua Jangwani, lazima wajiandae kutii masharti ya Zahera, kwani amesisitiza anataka wapambanaji atakaowapa nafasi.
Zahera alisema amesikia nyota wengi wakihusishwa kutua Yanga katika dirisha hili la usajili, ila kwake analowaambia ni kuhakikisha wanafuata kile anachokitaka ili wapate nafasi ya kucheza katika kikosi chake akiamini mchezaji yeyote wa timu ya Ligi Kuu ana uwezo wa kukipiga Jangwani.
“Mchezaji hadi asajiliwe kikosi kinachoshiriki ligi basi huyo ni mchezaji haswa na anayejitambua, hivyo kwa upande wangu yeyote anayejituma hasa mazoezini ndiye anayepata nafasi ya kucheza siangalii majina,” alisema Zahera.
“Kuna muda watu wananiletea mapenzi, sijui kwa nini fulani sijampanga katika kikosi cha kwanza. Huwa siwasikilizi naangalia mchezaji anayefanya vizuri mazoezini, nategemea kile alichokionyesha ndicho kitakachozaa matokeo mazuri hata kwenye mchezo huwezi ukampanga mvivu wa mazoezi ukategemea katika mapambano atacheza kwa nguvu, sio kweli, huo ndio msimamo wangu,” alisema.
Mwanaspoti