Kikosi cha Simba tayari kimerejea jijini Dar es salaam baada ya kumaliza ratiba ya michezo ya kanda ya ziwa
Simba kesho Jumanne itashuka uwanja wa Uhuru kuikabili JKT Tanzania katika mchezo mwingine wa ligi kuu ya Tanzania Bara
Kocha Mkuu wa mabingwa hao watetezi Patrick Aussems amesema licha ya timu yake kukusanya alama tisa kutoka kanda ya ziwa, bado kazi haijamalizika na wanahitaji kushinda michezo yote iliyobaki waweze kutetea ubingwa wao
Aidha Aussem amesema ushindani kwenye ligi umeongezeka katika kipindi hiki cha lala salama hivyo wanahitaji kupambana kila mara wanaposhuka dimbani
“Bado tuna kazi ya kufanya, mechi zote ni ngumu, ligi bado ina ushindani, hakuna mechi rahisi, kila timu inahitaji ushindi ndio maana hakuna anayekata tamaa mpaka filimbi ya mwisho inapopigwa, tunataka kushinda kila mechi iliyopo mbele, ” amesema
Baada ya mchezo dhidi ya JKT Tanzania kesho, kikosi cha Simba kitaelekea mkoani Mbeya ambako kitacheza michezo miwili dhidi ya Mbeya City na Tanzania Prisons
Kimahesabu, Simba inahitaji kushinda michezo nane kati ya 11 iliyobaki ili kujihakikishia ubingwa bila ya kujali matokeo ya mpinzani wake Yanga ambaye leo huenda akadondosha pointi zaidi dhidi ya Azam Fc