Nimepata maumivu ya kawaida – Gadiel

Beki wa kushoto wa Yanga Gadiel Michael Mbaga amewatoa hofu mashabiki wa timu hiyo kuwa hali yake inaendelea vizuri

Gadiel alishindwa kuendelea na mchezo leo dhidi ya Azam Fc baada ya kuumia kwenye kipindi cha kwanza na nafasi yake kuchukuliwa na Jaffar Mohammed

Gadiel amesema alipata mshtuko uliosababisha maumivu ya misuli. Amesema akipata mapumziko ya siku tatu hadi nne atakuwa sawa

“Nimepata maumivu ya kawaida ya misuli, mapumziko ya siku tatu hadi nne yatanisaidia kurejea katika hali yangu ya kawaida,” amesema

Yanga inakabiliwa na mchezo mwingine wa ligi kuu ya Tanzania Bara dhidi ya Tanzania Prisons ambao utapigwa Alhamisi, May 02 kwenye uwanja wa Taifa

Ninja, Chikupe wawatuliza Chirwa na Ngoma

Washambuliaji wa zamani wa Yanga Obrey Chirwa na Donald Ngoma ambao wanakipiga katika klabu ya Azam Fc leo wameshindwa kufurukuta mbele ya waajiri wao wa zamani wakikubali kipigo cha bao 1-0

Walinzi wawili wa kati wa Yanga Abdallah Shaibu ‘Ninja’ na Andrew Vicent ‘Dante’ leo walikuwa na kazi maalum ya kuhakikisha washambuliaji hao hawasababishi madhara

Hakika kazi hiyo wameifanya kwa ustadi mkubwa kwani walifanikiwa ‘kuwaweka mifukoni’ washambuliaji hao

Wakati Ngoma alipata mwanya wa kufunga bao lililokataliwa na mwamuzi baada ya kumfanyia madhambi Chikupe, nafasi pekee aliyopata Chirwa kwenye kipindi cha kwanza iliokolewa kwa ustadi mkubwa na kipa Klaus Kindoki

Ushindi wa Yanga leo umechangiwa kwa kiasi kikubwa na umakini wa walinzi hao na wachezaji wote kwa ujumla ambao walikuwa na nidhamu ya hali ya juu katika ulinzi

Licha ya kumiliki mpira kwa muda mwingi, Azam Fc ilikosa mbinu ya kuipenya ngome ya Yanga

FT : Azam Fc 0-1 Yanga

Mabingwa wa kihistoria wa Tanzania Yanga wameendelea kujiimarisha kileleni mwa msimamo wa ligi kuu baada ya kuichapa Azam Fc bao 1-0 katika mchezo uliopigwa uwanja wa Uhuru jijini Dar es salaam

Ikicheza kwa nidhamu na tahadhari kubwa, Yanga ilifunga bao lake pekee kwenye dakika ya 13 kupitia kwa winga Mrisho Ngasa aliyeunganisha mpira wa krosi uliochongwa na Ibrahim Ajib kutoka winga ya kulia

Krosi hiyo ya Ajib ilikuwa zao la shambulizi la kushitukizwa lililofanywa na Yanga

Ngasa sasa amefikisha mabao 5 msimu huu wakati Ajib ametengeneza bao la 16

Azam Fc ilitawala mchezo huo kwa muda mwingi hata hivyo mbinu ya mahiri ya kujilinda ya kocha Zahera iliwapa wakati mgumu wana ‘rambaramba’ hao kuipenya ngome ngumu ya Yanga iliyokuwa chini ya Abdallah Shaibu ‘Ninja’ na Andrew Vicent ‘Dante’

Azam ilipoteza nafasi pekee adimu kwenye dakika ya 84 baada ya Dani Lyanga kushindwa kuutumbukiza mpira kimiani akiwa amebaki na kipa Klaus Kindoki

Ushindi huo umeendelea kuiweka Yanga kileleni mwa msimamo wa ligi ikiwa imefikisha alama 77, ikiongoza kwa tofauti ya alama 8 dhidi ya Simba na alama 11 dhidi ya Azam Fc

Mchezo unaofuata ni dhidi ya Tanzania Prisons na utapigwa May 02 kwenye uwanja wa Taifa/Uhuru

KIkosi : Azam Fc vs Yanga, TPL April 29

1. Klaus Kindoki

2. Paulo Godfrey

3. Gadiel Michael

4. Abdallah Shaibu

5. Andrew Vicent

6. Feisal Salum

7. Mrisho Ngasa

8. Mohammed Issa

9. Heritier Makambo

10. Ibrahim Ajib (C)

11. Raphael Daudi

SUB

Ramadhani Kabwili

Juma Abdul

Said Juma

Jaffar Mohammed

Papi Tshishimbi

Amissi Tambwe

Haruna Moshi

Misimu miwili, mabao 35 huyu ndio John Bocco

Nahodha wa Simba John Bocco amefikisha mabao 35 katika misimu miwili aliyoitumikia Simba kwenye mashindano yote

Bocco aliyetua Simba akitokea klabu ya Azam Fc ambayo aliitumikia kwa takribani miaka 10, nidye kinara wa muda wote wa upachikaji mabao katika ligi ya Tanzania akiwa amefunga mabao zaidi ya 100

Licha ya umri kusonga, Bocco ‘hachuji’, ameendelea kuwa katika ubora uleule wa kupachika mabao

Msimu huu ameifungia Simba mabao 14 kwenye ligi akishika nafasi ya nne katika orodha ya vinara wa upachikaji mabao nyuma ya Meddie Kagere (16), Salim Aiyee (16) na Heritier Makambo (15)

Msimu uliopita Bocco aliifungia Simba mabao 14 na kushika nafasi ya pili nyuma ya Emmanuel Okwi ambaye msimu huu kasi yake ya kuzifumania nyavu imepungua akiwa amefunga mabao 10

Bocco kwa kushirikiana na Kagere na Okwi, wamefungia Simba jumla ya mabao 40 kwenye ligi msimu huu na kuifanya Simba kuwa moto wa kuotea mbali katika kuzifumania nyavu ikiwa imefunga jumla ya mabao 57

Aussems anataka ushindi mechi zote zilizobaki

Kikosi cha Simba tayari kimerejea jijini Dar es salaam baada ya kumaliza ratiba ya michezo ya kanda ya ziwa

Simba kesho Jumanne itashuka uwanja wa Uhuru kuikabili JKT Tanzania katika mchezo mwingine wa ligi kuu ya Tanzania Bara

Kocha Mkuu wa mabingwa hao watetezi Patrick Aussems amesema licha ya timu yake kukusanya alama tisa kutoka kanda ya ziwa, bado kazi haijamalizika na wanahitaji kushinda michezo yote iliyobaki waweze kutetea ubingwa wao

Aidha Aussem amesema ushindani kwenye ligi umeongezeka katika kipindi hiki cha lala salama hivyo wanahitaji kupambana kila mara wanaposhuka dimbani

“Bado tuna kazi ya kufanya, mechi zote ni ngumu, ligi bado ina ushindani, hakuna mechi rahisi, kila timu inahitaji ushindi ndio maana hakuna anayekata tamaa mpaka filimbi ya mwisho inapopigwa, tunataka kushinda kila mechi iliyopo mbele, ” amesema

Baada ya mchezo dhidi ya JKT Tanzania kesho, kikosi cha Simba kitaelekea mkoani Mbeya ambako kitacheza michezo miwili dhidi ya Mbeya City na Tanzania Prisons

Kimahesabu, Simba inahitaji kushinda michezo nane kati ya 11 iliyobaki ili kujihakikishia ubingwa bila ya kujali matokeo ya mpinzani wake Yanga ambaye leo huenda akadondosha pointi zaidi dhidi ya Azam Fc

Kapombe anakaribia kurejea kisosini Simba

Uongozi wa Simba umethibitisha kuwa beki wake kiraka Shomari Kapombe anakaribia kurejea kikosini baada ya kuanza mazoezi mepesi

Msemaji wa Simba Haji Manara amesema Kapombe amepona majeraha ya goti na tayari ameanza mazoezi ya gym ikiwa ni hatua ya mwanzo kabla ya kurejea dimbani

“Tunashukuru beki wetu Shomari Kapombe amepona majeraha ya goti yaliyomuweka nje kwa muda mrefu. Hivi sasa anafanya mazoezi ya Gym ili kuurejesha mwili katika hali yake kabla ya kuanza mazoezi ya mpira,” amesema

Kapombe amekuwa nje kwa zaidi ya miezi mitano akiuguza majeraha ya goti aliyopata nchini Afrika Kusini wakati akiitumikia timu ya Taifa

Licha ya beki huyo kuanza kujifua, kuna uwezekano mdogo kwake kucheza mechi zilizobaki

Wagombea Yanga kuanza kampeni Jumanne

Wagombea waliopitishwa kuwania nafasi mbalimbali za uongozi katika klabu ya Yanga, wanatarajiwa kuanza rasmi kampeni kesho Jumanne, April 30 2019

Kampeni zitaanza baada ya muda wa rufaa kwa wagombea walioenguliwa kupita huku mgombea mmoja kati ya 15 ambao majina yao yalienguliwa, amekata rufaa

Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF Malangwe Mchungahella amesema rufaa ya mgombea huyo wa nafasi ya Ujumbe, Rodgers Gumbo itasikilizwa kesho

Uchaguzi Mkuu wa Yanga kuwapata viongozi wapya watakoiongoza timu hiyo kwa kipindi cha miaka minne utafanyika Jumapili, May 05 2019

Hii hapa orodha ya wagombea wote waliopitishwa;

Mwenyekiti

1. Baraka Igagungula (ME)
2. Dr. Jonas Tiboroha (ME)
3. Elias Mwanjala (ME)
4. Dr. Mbette Mshindo Msola (ME)

Makamu Manyekiti

1. Fredrick Mwakalebela (ME)
2.Jannet Mbene (KE)
3. Titus Osoro (ME)
4. Yono Kevela (ME)

Wajumbe

1. Saady Mohamed Khimji (ME)
2. Hassan H. Yahaya (ME)
3. Arafat Hajji (ME)
4. Suma Mwaitenda (KE)
5. Hamad Islam (ME)
6. Dominick Albinus (ME)
7. Sharifu Amour Makosa (ME)
8. Eng. Bahati F. Mwaseba (ME)
9. Eng. Leonard Marango (ME)
10. Haruna H. Batenga (ME)
11. Athanas Kazinghe (ME)
12. Ramadhan Said (ME)
13. Salim Rupia (ME)
14. Dominick Francis (ME)
15. Sharifu Amir (ME)
16. Benjamin Mwakasendo (ME)
17. Christopha Kashiririka (ME)
18. Ally Msigwa (ME)
19. Frank K. Kamugisha (ME)
20. Said Kambi (ME)
21. Silvester Haule (ME)

NB : Rufaa ya mgombea mmoja wa nafasi ya Ujumbe Rodgers Gumbo itasikilizwa kesho Jumanne April 30 2019

Yanga yasaka alama tatu dhidi ya Azam Fc leo

Vinara wa ligi kuu ya Tanzania Bara Yanga leo wanashuka kwenye uwanja wa Uhuru kuikabili Azam Fc katika mchezo wa ligi hiyo

Mchezo unatarajiwa kuanza saa kumi kamili jioni

Yanga iliyojikusanyia alama 74, iko mbele ya Azam Fc kwa tofauti ya alama nane, inahitaji ushindi katika mchezo huo ili kuendelea kuweka hai mbio za kuwania ubingwa msimu huu

Hata hivyo, mchezo hautakuwa mwepesi kutokana na uimara wa kikosi cha Azam ambacho tangu kimtimue kocha Hans van Pluijm kimepoteza mchezo mmoja tu

Kocha Mwinyi Zahera amesema amewaandaa wachezaji wake kikamilifu lengo lao likiwa kushinda

Amesema ni mchezo ambao wanahitaji kupambana na kuwa makini zaidi, hawapaswi kufanya makosa mengi na lazima watumie nafasi

Timu zote zitawakosa wachezaji wake waandamizi Kelvin Yondani na Aggrey Morris wanaotumikia adhabu ya kukosa michezo mitatu