Simba haina shida wachezaji kuwatoa kwa mkopo wale ambao hawapati nafasi kwenye kikosi chao lakini timu ambayo inahitaji huduma ya wachezaji hao basi wanapaswa kujipanga kupangua masharti mawili magumu ukiachana na yale madogo madogo.
Sharti la kwanza ambalo limewekwa ni kuhakikisha huko watakakokwenda wanacheza kikosi cha kwanza na sio kukaa benchi ama jukwaani.
Sharti la pili ni kuhakikisha wanawapa huduma zote kwa jinsi watakavyokubaliana ikiwemo, mshahara, posho kuishi maisha mazuri yasiyokuwa ya mawazo hasa suala la kukosa mshahara kwa zaidi ya mwezi.
Kwasasa viongozi wa Simba wanasubiri ripoti ya kocha mkuu Patrick Aussems ili kuona ni wachezaji gani amependekeza waondolewe kwa mkopo na kama atahitaji kuongeza wachezaji na kwa nafasi gani.
Kuna taarifa kwmaba nyota watatu wa Simba Mohamed Rashid ‘Mo Rashid’, Marcel Kaheza na kipa Mohamed Said ‘Nduda’ watatolewa kwa mkopo katika timu ambazo zitahitaji huduma zao na kukubali masharti hayo huku kipa Emmanuel Mseja yeye anasubiri barua pekee ingawa yupo kwenye mazungumzo ya chini chini na Caostal Union ya Tanga.
Aliyekuwa Kaimu Rais wa Simba ambaye sasa ni mmoja wa wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi, Salim Abdallah ‘Try Again’ ambaye ameombwa kuendelea na majukumu yake hadi hapo baadaye Bodi itakapoanza majukumu yake rasmi alisema wamepokea maombi ya timu nyingi zikomba huduma za wachezaji wao.
Try Again amesema kuwa wana maombi mengi lakini hadi sasa hakuna maombi yaliyofanyiwa kazi kwani wanasubiri kocha wao atoe mapendekezo kupitia ripoti yao ila tayari wameweka masharti yao ambapo atakayevuka hayo atapewa mchezaji kama itatokea amependekezwa na kocha.
Simba imepokea maombi mengi ya mshambuliaji wao Mo Rashid ambapo timu tano zimetuma barua ambazo ni Singida United, Lipuli FC, Prisons, Coastal Union na KMC huku Kaheza anasakwa na timu mbili KMC na Alliance upande wa Nduda bado hakuna timu iliyojitokeza hadi sasa.
Try Again alisema, “Mo Rashid anatafutwa na timu nyingi sana na huenda tukaendelea kupokea maombi, ila hatuwezi kuamua lolote hadi hapo tutakapopata ripoti kutoka kwa kocha mkuu maana kila kitu tumemwachia akifanye yeye.
“Pia hizi timu zinazohitaji wachezaji wetu kiukweli wakubaliane na baadhi ya haya mammbo, apate nafasi ya kucheza kwani hiyo ndiyo maana halisi ya kupelekwa kwa mkopo kwani mchezaji akitolewa kwa mkopo matarajio ni kumrejesha tena kikosi kwetu wakati yupo kwenye kiwango kizuri zaidi.
“Timu hizo zitambue kwamba mchezaji tutakayewapa basi apate huduma zote, asiwe na njaa kabisa ya mshahara na mambo mengine ambayo yanaweza kuchangia kiwango chake kishuke, wamlee kama tunavyowalea sisi wachezaji wetu, vinginevyo itakuwa vigumu kuwapata wachezaji hao kutoka kwetu,” alisema Try Again.
Try Again alifafanua pia kuwa masuala yote ya ufundi yameachwa kwa Aussems ikiwemo kocha msaidizi na mapendekezo mengine ya usajili na mashindano yote ya ndani na nje ya nchi kwamba mahitaji atakayohitaji viongozi watakuwa watekelezaji.
“Kila kitu kipo chini ya kocha mkuu, hatutaki kumwingilia, hivyo akisema anahitaji kocha msaidizi na akimpendekeza basi sisi tutafanya utekelezaji ikiwemo mambo mengine, hivyo kwasasa tunamsubiri yeye tu,” alisema Try Again.
Aussems yeye alisema ataandaa majina ya wachezaji watano hadi sita atakaowasajili ila kati ya hao mchezaji mmoja tu ndiye atapendekeza asajiliwe wakati huu wa dirisha dogo na kufafanua kwamba, “Kati ya hao napendekeza straika mmoja tu mwenye uwezo wa kufunga na kutengeneza nafasi kwa wenzake,”.
Mpaka sasa kuna majina ya wachezaji wanaotajwa kwenye usajili wa Mabingwa hao watetezi wa ligi kuu Bara akiwemo Francis Kahata kutoka Gor Mahia ingawa ana mkataba na timu yake, Epharaim Guikan na Philomeno Otieno wote wa Gor Mahia pamoja na Sadam Juma wa KCCA ya Uganda.










