Mgombea wa nafasi ya Mwenyekiti katika uchaguzi wa Yanga utakaofanyika May 05, Dk Mshindo Msolla amezindua kampeni zake leo Makao Makuu ya klabu ya Yanga, jijini Dar es salaam
Dk Msolla ambaye kitaalamu ni Mwalimu wa mpira wa miguu (kocha) aliyewahi kuinoa Taifa Stars, ametaja vipaumbele vyake ambavyo atavitekeleza kama atachaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Yanga
Baadhi ya vipaumbele hivyo ni pamoja na Kujenga umoja na ushirikiano, Kuendeleza mchakato wa mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji, Kuendeleza miradi yote ya klabu iliyopo pia kuanzisha mipya, Kuweka na kusimamia misingi ya utawala bora pia kuweka misingi ya Yanga kuwa na timu imara

Dk Msolla amesema anataka kuona ushirikiano baina ya timu na mashabiki na wanachama wake unaimarika zaidi na ameunga mkono zoezi la kuichangia Yanga linaloendeshwa
“Nataka kujenga umoja ndani ya klabu kwa maana ya kuirudisha timu kwa wanachi hivyo sio vibaya wenye timu kuichangia klabu yao”
Aidha DK Msolla amesema atabadili mfumo wa uchaguzi wa Yanga unaotoa fursa pekee kwa wanachama wa Dar es salaam kushiriki michakato ya uchaguzi
“Natambua kuwa wanachama wengi wa Yanga ambao hushiriki uchaguzi ni wale ambao wapo Dar, ndani ya uongozi wangu kama nikipewa nafasi basi wa mkoani nao watapata haki hiyo.
“Tutakuwa na mfumo ambao utawawezesha kupiga kura wakiwa kwenye matawi yao”
Kuhusu utawala bora Dk Msolla amesema uongozi wake hautaingilia majukumu ya kocha Mwinyi Zahera
Amesema kocha huyo ni mtu muhimu kwa klabu ya Yanga, ni bahati kuwa nae hasa ikizingatiwa timu inapita katika kipindi kigumu sana
“Mimi ni kocha wengi wananifahamu, akihitaji ushauri wa kiufundi nitampatia lakini nitaingia Yanga kama mwenyekiti hivyo niseme wazi kuwa nitamwacha awe huru kutekeleza majukumu yake.
“Uongozi wangu hautakuwa na mipango ya kuachana naye, mara kadhaa nimekuwa nikisema wazi kuwa Yanga tunabahati ya kupata kocha wa namna hii”
Pia Dk Msolla amesema atahakikisha Yanga inakuwa na misingi mizuri ya kuendeleza vijana wa kikosi B kwa lengo la kuja kuwatumia kikosi cha kwanza
Wagombea wa nafasi mbalimbali za uongozi Yanga wameendelea kuzindua kampeni ambazo zitadumu hadi Jumamosi, May 04 siku moja kabla ya uchaguzi