Yanga kusaka alama tatu mchezo dhidi ya Prisons leo

Ligi Kuu ya Tanzania Bara inaendelea leo kwa mchezo mmoja kupigwa ambapo vinara wa ligi hiyo Yanga watakuwa uwanja wa Uhuru kuikabili Tanzania Prisons

Yanga inahitaji kushinda mchezo huo ili kuendelea kuipa ‘presha’ Simba kwenye mbio za kuwania ubingwa msimu

Aidha, itakuwa ikisaka rekodi ya kuwa timu kwanza kufikisha alama 80 msimu huu

Wapinzani wao katika mbio za upingwa Simba wao wanaelekea mkoani Mbeya ambapo kesho May 03 watacheza na Mbeya City kisha May 05 watacheza na Tanzania Prisons

Mratibu wa Yanga Hafidh Saleh amesema wachezaji wote wako katika hali nzuri, tayari kwa mchezo huo utakaopigwa kuanzia saa kumi kamili jioni

Dk Msolla azindua kampeni Yanga

Mgombea wa nafasi ya Mwenyekiti katika uchaguzi wa Yanga utakaofanyika May 05, Dk Mshindo Msolla amezindua kampeni zake leo Makao Makuu ya klabu ya Yanga, jijini Dar es salaam

Dk Msolla ambaye kitaalamu ni Mwalimu wa mpira wa miguu (kocha) aliyewahi kuinoa Taifa Stars, ametaja vipaumbele vyake ambavyo atavitekeleza kama atachaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Yanga

Baadhi ya vipaumbele hivyo ni pamoja na Kujenga umoja na ushirikiano, Kuendeleza mchakato wa mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji, Kuendeleza miradi yote ya klabu iliyopo pia kuanzisha mipya, Kuweka na kusimamia misingi ya utawala bora pia kuweka misingi ya Yanga kuwa na timu imara

Dk Msolla amesema anataka kuona ushirikiano baina ya timu na mashabiki na wanachama wake unaimarika zaidi na ameunga mkono zoezi la kuichangia Yanga linaloendeshwa

“Nataka kujenga umoja ndani ya klabu kwa maana ya kuirudisha timu kwa wanachi hivyo sio vibaya wenye timu kuichangia klabu yao”

Aidha DK Msolla amesema atabadili mfumo wa uchaguzi wa Yanga unaotoa fursa pekee kwa wanachama wa Dar es salaam kushiriki michakato ya uchaguzi

“Natambua kuwa wanachama wengi wa Yanga ambao hushiriki uchaguzi ni wale ambao wapo Dar, ndani ya uongozi wangu kama nikipewa nafasi basi wa mkoani nao watapata haki hiyo.

“Tutakuwa na mfumo ambao utawawezesha kupiga kura wakiwa kwenye matawi yao”

Kuhusu utawala bora Dk Msolla amesema uongozi wake hautaingilia majukumu ya kocha Mwinyi Zahera

Amesema kocha huyo ni mtu muhimu kwa klabu ya Yanga, ni bahati kuwa nae hasa ikizingatiwa timu inapita katika kipindi kigumu sana

“Mimi ni kocha wengi wananifahamu, akihitaji ushauri wa kiufundi nitampatia lakini nitaingia Yanga kama mwenyekiti hivyo niseme wazi kuwa nitamwacha awe huru kutekeleza majukumu yake.

“Uongozi wangu hautakuwa na mipango ya kuachana naye, mara kadhaa nimekuwa nikisema wazi kuwa Yanga tunabahati ya kupata kocha wa namna hii”

Pia Dk Msolla amesema atahakikisha Yanga inakuwa na misingi mizuri ya kuendeleza vijana wa kikosi B kwa lengo la kuja kuwatumia kikosi cha kwanza

Wagombea wa nafasi mbalimbali za uongozi Yanga wameendelea kuzindua kampeni ambazo zitadumu hadi Jumamosi, May 04 siku moja kabla ya uchaguzi

BREAKING NEWS: REGINALD MENGI AFARIKI DUNIA

Mwenyekiti Mtendaji wa Makampuni ya IPP , Dkt Reginald Abraham Mengi (75) amefariki dunia usiku wa kuamkia leo.

Dk Mengi amefariki dunia akiwa jijini Dubai, Falme za Kiarabu (UAE).

Dk Mengi alikuwa ni mfanyabiashara mkubwa barani Afrika, ambapo sehemu ya utajir wake aliuelekeza kwa jamii kwa kutoa misaada mbalimbali.

Kwa mujibu wa jarida la Forbes mwaka 2014, utajiri wa bilione huyo ulitajwa kuwa ni TZS trilioni 1.3 ($560 milioni).

Enzi za uwahi wake na katika shughuli zake aliweza kushinda tuzo mbalimbali za kitaifa na kimataifa, pamoa na kuandika kitabu chake cha I Can, I Must, I will.

Mungu Ailaze Roho yake Mahali Pema Peponi. Amina

Yanga kuikabili Tanzania Prisons uwanja wa Uhuru kesho

Ligi Kuu ya Tanzania Bara inaendelea kesho ambapo vinara wa ligi hiyo Yanga watakuwa uwanja wa Uhuru kupepetana na Tanzania Prisons

Baada ya juzi kuichapa Azam Fc bao 1-0, Yanga itakuwa na nafasi ya kuzidi kujiimarisha kileleni mwa msimamo wa ligi kama itaibuka na ushindi kwenye mchezo huo

Mabingwa hao wa kihistoria wamesalia na michezo mitano kabla ya kumalizika kwa ligi, kama watashinda yote watafikisha alama 92

Bado Yanga haiwezi kuondolewa katika mbio za ubingwa kwani wapinzani wao Simba bado watahitaji kupata matokeo katika michezo yao10 iliyobaki ili waweze kutete ubingwa

Baada ya mchezo wa kesho Yanga itaelekea mkoani Iringa tayari kwa mchezo wa nusu fainali kombe la FA dhidi ya Lipuli Fc utakaopigwa May 06 2019

Ajib ajumuishwa kikosi cha Stars

Hatimaye kocha Mkuu wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ Emmanuel Amunike amemjumuisha nahodha wa Yanga Ibrahim Ajib kwenye kikosi cha timu ya Taifa kitakachoshiriki michuano ya AFCON itakayofanyika mwezi ujao nchini Misri pamoja na michuano ya CHAN inayohusisha wachezaji wa ndani

Kikosi hicho chenye wachezaji 39 pia kimewajumuisha Gadiel Michael, Kelvin Yondani na Feisal Salum kutoka klabu ya Yanga

Nimepata maumivu ya kawaida – Gadiel

Beki wa kushoto wa Yanga Gadiel Michael Mbaga amewatoa hofu mashabiki wa timu hiyo kuwa hali yake inaendelea vizuri

Gadiel alishindwa kuendelea na mchezo leo dhidi ya Azam Fc baada ya kuumia kwenye kipindi cha kwanza na nafasi yake kuchukuliwa na Jaffar Mohammed

Gadiel amesema alipata mshtuko uliosababisha maumivu ya misuli. Amesema akipata mapumziko ya siku tatu hadi nne atakuwa sawa

“Nimepata maumivu ya kawaida ya misuli, mapumziko ya siku tatu hadi nne yatanisaidia kurejea katika hali yangu ya kawaida,” amesema

Yanga inakabiliwa na mchezo mwingine wa ligi kuu ya Tanzania Bara dhidi ya Tanzania Prisons ambao utapigwa Alhamisi, May 02 kwenye uwanja wa Taifa

Ninja, Chikupe wawatuliza Chirwa na Ngoma

Washambuliaji wa zamani wa Yanga Obrey Chirwa na Donald Ngoma ambao wanakipiga katika klabu ya Azam Fc leo wameshindwa kufurukuta mbele ya waajiri wao wa zamani wakikubali kipigo cha bao 1-0

Walinzi wawili wa kati wa Yanga Abdallah Shaibu ‘Ninja’ na Andrew Vicent ‘Dante’ leo walikuwa na kazi maalum ya kuhakikisha washambuliaji hao hawasababishi madhara

Hakika kazi hiyo wameifanya kwa ustadi mkubwa kwani walifanikiwa ‘kuwaweka mifukoni’ washambuliaji hao

Wakati Ngoma alipata mwanya wa kufunga bao lililokataliwa na mwamuzi baada ya kumfanyia madhambi Chikupe, nafasi pekee aliyopata Chirwa kwenye kipindi cha kwanza iliokolewa kwa ustadi mkubwa na kipa Klaus Kindoki

Ushindi wa Yanga leo umechangiwa kwa kiasi kikubwa na umakini wa walinzi hao na wachezaji wote kwa ujumla ambao walikuwa na nidhamu ya hali ya juu katika ulinzi

Licha ya kumiliki mpira kwa muda mwingi, Azam Fc ilikosa mbinu ya kuipenya ngome ya Yanga

FT : Azam Fc 0-1 Yanga

Mabingwa wa kihistoria wa Tanzania Yanga wameendelea kujiimarisha kileleni mwa msimamo wa ligi kuu baada ya kuichapa Azam Fc bao 1-0 katika mchezo uliopigwa uwanja wa Uhuru jijini Dar es salaam

Ikicheza kwa nidhamu na tahadhari kubwa, Yanga ilifunga bao lake pekee kwenye dakika ya 13 kupitia kwa winga Mrisho Ngasa aliyeunganisha mpira wa krosi uliochongwa na Ibrahim Ajib kutoka winga ya kulia

Krosi hiyo ya Ajib ilikuwa zao la shambulizi la kushitukizwa lililofanywa na Yanga

Ngasa sasa amefikisha mabao 5 msimu huu wakati Ajib ametengeneza bao la 16

Azam Fc ilitawala mchezo huo kwa muda mwingi hata hivyo mbinu ya mahiri ya kujilinda ya kocha Zahera iliwapa wakati mgumu wana ‘rambaramba’ hao kuipenya ngome ngumu ya Yanga iliyokuwa chini ya Abdallah Shaibu ‘Ninja’ na Andrew Vicent ‘Dante’

Azam ilipoteza nafasi pekee adimu kwenye dakika ya 84 baada ya Dani Lyanga kushindwa kuutumbukiza mpira kimiani akiwa amebaki na kipa Klaus Kindoki

Ushindi huo umeendelea kuiweka Yanga kileleni mwa msimamo wa ligi ikiwa imefikisha alama 77, ikiongoza kwa tofauti ya alama 8 dhidi ya Simba na alama 11 dhidi ya Azam Fc

Mchezo unaofuata ni dhidi ya Tanzania Prisons na utapigwa May 02 kwenye uwanja wa Taifa/Uhuru

KIkosi : Azam Fc vs Yanga, TPL April 29

1. Klaus Kindoki

2. Paulo Godfrey

3. Gadiel Michael

4. Abdallah Shaibu

5. Andrew Vicent

6. Feisal Salum

7. Mrisho Ngasa

8. Mohammed Issa

9. Heritier Makambo

10. Ibrahim Ajib (C)

11. Raphael Daudi

SUB

Ramadhani Kabwili

Juma Abdul

Said Juma

Jaffar Mohammed

Papi Tshishimbi

Amissi Tambwe

Haruna Moshi

Wagombea Yanga kuanza kampeni Jumanne

Wagombea waliopitishwa kuwania nafasi mbalimbali za uongozi katika klabu ya Yanga, wanatarajiwa kuanza rasmi kampeni kesho Jumanne, April 30 2019

Kampeni zitaanza baada ya muda wa rufaa kwa wagombea walioenguliwa kupita huku mgombea mmoja kati ya 15 ambao majina yao yalienguliwa, amekata rufaa

Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF Malangwe Mchungahella amesema rufaa ya mgombea huyo wa nafasi ya Ujumbe, Rodgers Gumbo itasikilizwa kesho

Uchaguzi Mkuu wa Yanga kuwapata viongozi wapya watakoiongoza timu hiyo kwa kipindi cha miaka minne utafanyika Jumapili, May 05 2019

Hii hapa orodha ya wagombea wote waliopitishwa;

Mwenyekiti

1. Baraka Igagungula (ME)
2. Dr. Jonas Tiboroha (ME)
3. Elias Mwanjala (ME)
4. Dr. Mbette Mshindo Msola (ME)

Makamu Manyekiti

1. Fredrick Mwakalebela (ME)
2.Jannet Mbene (KE)
3. Titus Osoro (ME)
4. Yono Kevela (ME)

Wajumbe

1. Saady Mohamed Khimji (ME)
2. Hassan H. Yahaya (ME)
3. Arafat Hajji (ME)
4. Suma Mwaitenda (KE)
5. Hamad Islam (ME)
6. Dominick Albinus (ME)
7. Sharifu Amour Makosa (ME)
8. Eng. Bahati F. Mwaseba (ME)
9. Eng. Leonard Marango (ME)
10. Haruna H. Batenga (ME)
11. Athanas Kazinghe (ME)
12. Ramadhan Said (ME)
13. Salim Rupia (ME)
14. Dominick Francis (ME)
15. Sharifu Amir (ME)
16. Benjamin Mwakasendo (ME)
17. Christopha Kashiririka (ME)
18. Ally Msigwa (ME)
19. Frank K. Kamugisha (ME)
20. Said Kambi (ME)
21. Silvester Haule (ME)

NB : Rufaa ya mgombea mmoja wa nafasi ya Ujumbe Rodgers Gumbo itasikilizwa kesho Jumanne April 30 2019