Yanga yasaka alama tatu dhidi ya Azam Fc leo

Vinara wa ligi kuu ya Tanzania Bara Yanga leo wanashuka kwenye uwanja wa Uhuru kuikabili Azam Fc katika mchezo wa ligi hiyo

Mchezo unatarajiwa kuanza saa kumi kamili jioni

Yanga iliyojikusanyia alama 74, iko mbele ya Azam Fc kwa tofauti ya alama nane, inahitaji ushindi katika mchezo huo ili kuendelea kuweka hai mbio za kuwania ubingwa msimu huu

Hata hivyo, mchezo hautakuwa mwepesi kutokana na uimara wa kikosi cha Azam ambacho tangu kimtimue kocha Hans van Pluijm kimepoteza mchezo mmoja tu

Kocha Mwinyi Zahera amesema amewaandaa wachezaji wake kikamilifu lengo lao likiwa kushinda

Amesema ni mchezo ambao wanahitaji kupambana na kuwa makini zaidi, hawapaswi kufanya makosa mengi na lazima watumie nafasi

Timu zote zitawakosa wachezaji wake waandamizi Kelvin Yondani na Aggrey Morris wanaotumikia adhabu ya kukosa michezo mitatu

Yanga yataka sapoti ya mashabiki mchezo dhidi ya Azam Fc

Mashabiki wa Yanga wameaswa kujitokeza kwa wingi uwanja wa Uhuru kesho kuiunga mkono timu yao ikichuana na Azam Fc

Mratibu wa Yanga Hafidh Saleh amesema wamefanya maandalizi ya kutosha na wana matumaini makubwa ya kupata matokeo mazuri kwenye mchezo huo

“Tunawaomba mashabiki wetu wajitokeze kwa wingi kutuunga mkono. Timu iko tayari kwa ajili ya mchezo huo na lengo letu ni kupata ushindi ambao utaendelea kutuimarisha kileleni mwa msimamo wa ligi”

Azam Fc itakuwa mwenyeji wa mchezo huo wa kwanza kwa timu hizo kukutana msimu huu

Viingilio kwa majukwaa ya VIP A ni Tsh 15,000/- na VIP B ni Tsh 10,000/- wakati Mzunguuko ikiwa Tsh 5,000/-

Mchezo huo pia utakuwa mbashara kupitia Azam Sport 2 ambapo mtangazaji Baraka Mpenja ndiye atakayeongoza matangazo hayo

Viongozi hakikisheni Yanga inamaliza msimu salama

Mpaka hapa ilipofika Yanga hata kama haitatwaa ubingwa wa ligi kuu, msimu huu utabaki kuwa wa mafanikio kwa mabingwa hao wa kihistoria

Licha ya kukabiliwa na changamoto za kiuchumi, wachezaji wa timu hiyo wamepambana na kuweza kufanya vizuri kwenye ligi huku wakitinga nusu fainali ya michuano ya kombe la Azam (ASFC)

Mwanzoni mwa msimu hakuna aliyeipa Yanga nafasi ya kufanya vizuri kutokana na kushindwa kufanya usajili ‘mkubwa’ ukilinganisha na wapinzani wake Simba na Azam Fc

Bila shaka mgomo waliofanya wachezaji juzi umewasikitisha wengi, ni faraja kusikia uongozi wa timu hiyo umechukua hatua haraka kuirejesha timu katika hali ya kawaida

Wachezaji na benchi la ufundi wamefanya kazi kubwa katika mazingira magumu, litakuwa jambo la kusikitisha kama walichokifanya wakati wa shida kitaharibiwa dakika hizi za majeruhi

Naamini viongozi wameyasikia malalamiko ya wachezaji, wayapatie ufumbuzi mapema ili wamalize msimu kwa moyo mmoja

Yanga bado inawania mataji mawili, wakati huu inapaswa fikra za wachezaji ziwe katika kumaliza msimu kwa nguvu ili washinde angalau taji moja kuliko kufikiria mambo mengine

Majanga ya msimu uliopita yaikumba tena Yanga

Wakati kikosi cha Yanga kikitarajiwa kuchuana na Azam Fc Jumatatu, April 29 katika mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara, kocha Mwinyi Zahera huenda akalazimika kutumia wachezaji wa kikosi cha pili kufuatia mgomo unaofanywa na wachezaji wa kikosi cha kwanza

Leo Zahera aliamua kutumia wachezaji wa Yanga B kujiandaa na mchezo dhidi ya Azam FC baada ya wachezaji wa kikosi cha kwanza kugoma tena kufanya mazoezi licha ya kufika mapema uwanja wa chuo cha Polisi Kurasini

Mwishoni mwa msimu uliopita Yanga ilikumbana na changamoto kama hii ya wachezaji kugoma wakishinikiza walipwe hali iliyopelekea kumalizia michezo ya mikaoni ikiwa na kikosi cha wachezaji 14

Huenda hali hiyo ikajirudia tena kwa michezo sita iliyobaki kama viongozi wa muda wa Yanga hawatachukua hatua za haraka kutatua mgogoro uliopo

Wachezaji wafika mazoezini kuendelea na maandalizi ya kuikabili Azam Fc

Wachezaji wote leo wamefika mazoezini kuendelea na maandalizi ya mchezo dhidi ya Azam Fc utakaopigwa Jumatatu, April 29 kwenye uwanja wa Uhuru

Jana wachezaji hao waligoma kufanya mazoezi wakishinikiza waonane na uongozi wa Yanga ili kujua hatma ya madai yao ya mishahara na fedha za usajili

Wagoma tena

Licha ya kufika mapema mazoezini, wachezaji wa kikosi cha kwanza, waligoma kufanya mazoezi wakiwasubiri viongozi wafanye nao kikao

Kocha Zahera alilazimika kutumia Yanga B kuendelea na program ya mazoezi kujiandaa na mchezo dhidi ya Azam

Azam Fc vs Yanga kupigwa uwanja wa Uhuru

Mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara kati ya Azam Fc dhidi ya Yanga ambao awali ulipangwa kupigwa uwanja wa Taifa, sasa umehamishiwa uwanja wa Uhuru

Mratibu wa Yanga Hafidh Saleh amesema wamepokea barua kutoka TFF inayowaelekeza sababu ya mchezo huo kuhamishiwa uwanja wa Uhuru ni kutoa nafasi kwa uwanja wa Taifa kufanyiwa ukarabati baada ya kumalizika mchezo wa fainali AFCON U17 utakaopigwa April 28 2019

Kikosi cha Yanga kinaendelea kujifua kwenye uwanja wa Chuo cha Polisi Kurasini jijini Dar es salaam kujiandaa na mchezo huo utakaopigwa Jumatatu, April 29 2019 saa kumi kamili jioni

Uwanja wa Uhuru ulifanyiwa ukarabati kabla ya kuanza kwa michuano ya vijana ya AFCON ambapo nyasi bandia za uwanja huo zilibadilishwa

Waliochangia Milioni moja kualikwa tukio kubwa May 11 Dar

TAARIFA MUHIMU

Kutokana na umuhimu wa Kila Mwanayanga ambae anatoa pesa yake kwa ajili ya timu yetu TUIPENDAYO na yenye Thamani kubwa sana kwetu sote, Kamati imefikia uamuzi ufuatao ili kujenga wigo mpana wa kila mtu kuwa sehemu ya tukio hili muhimu linalohusu uchangiaji wa Klabu yetu.

Tukio Maalum la chakula cha jioni jijini Dar es salaam litafanyika siku ya Jumamosi tarehe 11/05/2019 Hotel ya Serena kuanzia saa kumi na mbili jioni.

Makundi ambayo yatakuwa yameshachangia shilingi milioni moja au zaidi yatapewa kadi ya mualiko na kumteua mtu mmoja ambaye ataliwakilisha kwa niaba na hatimaye aweze kushiriki kwenye Chakula Cha Jioni pamoja na kupokea CHETI MAALUMU cha Shukurani kwa niaba ya kundi lake.

Kamati imeona ni busara kupata uwakilishi huo wa mtu mmoja mmoja kutokana na eneo husika kubeba idadi isiyozidi watu mia tano.

Kwa mantiki hiyo tunaamini tutakuwa tumeweza kushirikisha kila kundi au mtu kwenye matukio haya muhimu kwa Klabu yetu.

TUENDELEE KUICHANGIA TIMU YETU ILI TUWE NA KIKOSI SHINDANI MSIMU UJAO

Timu ya Wananchi Wawekezaji ni Wananchi

Deo Mutta
KATIBU – KAMATI YA HAMASA
YANGA 23/04/2019

Yanga yajitathmini faini za kila mara

Uongozi wa Yanga umesema utachukua hatua ili ‘kujisahihisha’ kuepuka faini za Shirikisho la Soka nchini (TFF) kutokana na matukio yanayohusisha imani za kishirikina yanayojiri kwenye baadhi ya michezo yake

Matukio ya kutotumia mlango rasmi wa kuingia uwanjani yameigharimu sana Yanga msimu huu ambapo jana ilipigwa faini ya nne baada ya kufanya kosa hilo mkoani Mtwara ilipokwenda kucheza na Ndanda Fc

Yanga tayari imepigwa faini zilizoigharimu timu hiyo zaidi ya Tsh Milioni 10 kutokana na matukio hayo ya kuingia uwanjani kwa kutumia ‘njia za panya’

Afisa Habari wa Yanga Dismas Ten amesema matukio hayo yanachangiwa zaidi ya Wananchi ambao kimsingi ndio wenye timu na wanahusishwa kuisimamia timu inapokwenda kucheza

“Umefika wakati sasa tunapaswa kuwaelimisha watu wetu wafahamu athari tunazopata kutokana na kuendekeza imani hizi,” amesema

“Lazima ifahamike kila mchezo una kanuni na taratibu zake. Tukiendelea kuvunja kanuni kutokana na imani zetu, tutaendelea kuigharimu timu”

TMA yatoa tahadhari ujio wa kimbunga Keneth

Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini Tanzania (TMA) imetangaza kuwa Kimbunga Kenneth kimeongezeka kasi na kinatarajiwa kufika pwani ya kusini ya Tanzania na kaskazini mwa Msumbiji kuanzia usiku wa leo Alhamisi

Kwa mujibu wa TMA, jana kimbunga hicho kilikuwa kilomita 450 kutoka pwani ya Mtwara na kina kasi ya kilomita 130 kwa saa.

Kimbunga hicho kinatarajiwa kuongeza nguvu zaidi leo Alhamisi mchana ambapo kitakuwa kinasafiri kwa kilomita 170 kwa saa na kitakuwa kilomita 150 kutoka pwani ya Mtwara.

Kwa mujibu wa TMA, eneo husika ambalo kimbunga hicho kitatua litakuwa nchini Msumbiji, kikiwa na kasi ya kilomita 100 kwa saa. Eneo hilo litakuwa kilomita 200 kutoka pwani ya Mtwara.

Hata hivyo, mkoa wa Mtwara na maeneo jirani hususani mikoa ya Lindi na Ruvuma yataathirika pakubwa (athari zinategemewa kufikia umbali mpaka wa kilomita 500 kutoka Mtwara).

TMA imetahadharisha kuwa kimbunga hicho kitaingia nchi kavu na nguvu kubwa (ya upepo na mvua) itakayopelekea madhara makubwa kwa maisha ya watu na mali zao.

“Madhara yanayotarajiwa ni pamoja na mtawanyiko mkubwa wa mafuriko, uharibufu wa mali na makazi, kuezuliwa mapaa kutokana na upepo mkali. Uharibifu wa mazao mashambani na miundombinu kutokana na mafuriko”