Yanga yatua Iringa kibabe, yaipania Lipuli Fc

Vinara wa ligi kuu Tanzania Bara Yanga waliwasili mkoani Iringa jana jioni tayari kwa mchezo wa nusu fainali kombe la FA dhidi ya Lipuli fc

Mchezo huo utapigwa Jumatatu, May 06 uwanja wa Samora

Yanga inayosaka nafasi ya kurejea kwenye michuano ya Kimataifa msimu ujao, imepania kushinda mchezo huo ili kutinga fainali ambapo kama ikifanikiwa, itachuana na Azam Fc

Msafara wa Yanga umejumuisha wachezaji 24 ambao leo wataanza maandalizi ya mchezo huo mkoani Iringa

Yanga yaomboleza kifo cha Mwanachama wake Dk Mengi

TAARIFA

Uongozi wa Yanga, wanachama na mashabiki wamepokea kwa masikitiko makubwa sana kifo cha aliekuwa Mwenyekiti mtendaji wa makampuni ya IPP Dkt Reginald A Mengi kilichotokea jana uko falme za kiarabu

Mzee Mengi alikuwa mwanachama na pia mwanafamilia wa Yanga na tunatambua sana mchango wake kwenye klabu yetu

Tunaungana na Familia pamoja na wa Tanzania wote kwenye kipindi hiki kigumu cha Maombolezo

Bwana ametoa na bwana ametwaa jina lake lihimidiwe

Kesi ya kupinga uchaguzi Yanga yafutwa, kadi zote kutumika

Mwenyekiti wa Kamati ya uchaguzi ya TFF Malangwe Mchungahella ambaye Kamati yake inashirikiana na kamati Maalum ya Uchaguzi ya Yanga, amesema kesi iliyokuwa imefunguliwa na Wanachama wawili ya kupinga uchaguzi wa Yanga, imefutwa.

Mchungahella amesema baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kufuta shauri hilo, uchaguzi utafanyika May 05 kama ulivyopangwa

Aidha amesema mpaka sasa zoezi la kampeni linaendelea vizuri na hakuna malalamiko yoyote ya uvunjwaji wa sheria

Mchungahella amesema wanachama wote wenye kadi za zamani (kitabu) na za ki-elektroniki (posta) wataruhusiwa kushiriki katika mchakato huo

Muhimu ni Mwanachama lazima awe amelipia ada ya mwaka

Yondani aongeza nguvu Yanga

Beki kisiki wa Yanga Kelvin Yondani amejumuishwa kwenye kikosi cha timu hiyo kilichoondoka leo kuelekea mkoani Iringa kwa ajili ya mchezo wa nusu fainali kombe la FA dhidi ya Lipuli Fc

Mchezo huo utapigwa Jumatatu, May 06 katika uwanja wa Samora

Yondani amemaliza kutumikia adhabu ya kukosa michezo mitatu baada ya kuonyeshwa kadi nyekundu katika mchezo dhidi ya Kagera Sugar uliopigwa jijini Mwanza

Amekosa michezo dhidi ya Mtibwa Sugar, Azam Fc na Tanzania Prisons

Wachezaji waliojumuishwa kwenye msafara huo ni pamoja na Klaus Kindoki, Ramadhan Kabwili, Kelvin Yondan, Haji Mwinyi, Juma Abdul, Paul Godfrey, Abdallah Shaibu, Endrew Vicent, Said Makapu, Feisal Salum, Mohammed Issa, Papy Tshishimbi, Thaban Kamusoko, Deus Kaseke, Mrisho Ngasa, Ibrahim Ajib, Raphael Daud, Herieter Makambo, Amiss Tambwe, Haruna Moshi, Jaffar Mohamed, Ibrahim Hamid na Pius Buswita

Mchezo wa kwanza wa nusu fainali kombe la FA unapigwa leo kati ya Azam Fc dhidi ya KMC, saa moja jioni uwanja wa Azam Complex

Mastaa kibao waalikwa ‘Gala Dinner’ May 11

Siku ya Jumamosi ya May 11 2019 Yanga imepanga kuandika historia jijini Dar es salaam katika hafla maalum ya chakula cha jioni iliyoandaliwa Kamati ya Uhamishaji wa michango inayoongozwa na Mh Anthony Mavunde

Hafla hiyo ambayo itatumika ‘kuijaza Yanga mapesa’, itawashirikisha wadau wake mbalimbali ambao kwa umoja wao wamedhamiria kuirejesha heshima ya timu hiyo

Mwanamuziki Ali Kiba ni miongoni mwa watu maarufu watakaohudhuria hafla hiyo itakayofanyika Hoteli ya Serena kuanzia saa 12 jioni

Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe Mh Jokate Mwegelo, Wema Sepetu, Jackline Wolper, Batuli, Vicent Kigosi na Steve Nyerere nao watakuwepo

FT : Yanga 2-1 Prisons

Yanga imeendelea kujiimarisha kileleni mwa msimamo wa ligi baada ya kuichapa Tanzania Prisons mabao 2-1 katika mchezo uliopigwa uwanja wa Uhuru jijini Dar es salaam

Yanga iliyokuwa bora katika mchezo wa leo, ilifunga mabao yake kupitia kwa Wacongomani Papi Tshishimbi na Heritier Makambo wakati bao la kufutia machozi kwa upande wa Prisons lilifungwa na Ismail Kada

Tshishimbi ndiye aliyeanza kuifungia Yanga bao la kuongoza kwenye dakika ya 23 akimalizia mpira wa adhabu uliochongwa na Ibrahim Ajib

Hilo lilikuwa bao la 16 kutengenezwa na Ajib msimu huu

Dakika tisa baadae Kada aliisawazishia Prisons akiujaza mpira wavuni baada ya walinzi wa Yanga kuzembea kuondoa mpira wa kona

Makambo aliihakikishia Yanga ushindi kwenye dakika ya 66 akiunganisha kwa kichwa krosi ya Paulo Godfrey ‘Boxer’

Ushindi huo umeifanya Yanga kuwa timu ya kwanza kufikisha alama 80 msimu huu na kuendelea kujikitia kileleni mwa msimamo wa ligi kwa tofauti ya alama nane dhidi ya Simba inayoshika nafasi ya pili ikiwa na alama 72

Baada ya ushindi huo, Yanga itaelekea mkoani Iringa tayari kwa mchezo wa nusu fainali kombe la FA (ASFC) dhidi ya Lipuli, mchezo ukitarajiwa kupigwa Jumapili, May 05

Makambo awafikia Aiyee, Kagere

Bao alilofunga Heritier Makambo katika mchezo dhidi ya Tanzania Prisons limemfanya mshambuliaji huyo afikishe mabao 16 na kuwafikia Salum Aiyee wa Mwadui Fc na Meddie Kagere wa Simba

Leo Makambo ameiongoza Yanga kuibuka na ushindi muhimu wa mabao 2-1 dhidi ya Tanzania Prisons

Mshambuliaji huyo kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, anayo nafasi ya kuibuka mfungaji bora msimu huu kama ataweza kuitumia vyema michezo minne iliyobaki kujiongezea mabao

Michezo iliyobaki ni dhidi ya Ruvu Shooting, Mbeya City, Biashara United na Azam Fc

Ni mchezo mmoja tu dhidi ya Biashara United ambao utapigwa nje ya jiji la Dar es salaam

Igangula kuanza na uwanja wa Kaunda

Mgombea wa nafasi ya Mwenyekiti wa klabu ya Yanga Baraka Igangula amesema kama atachaguliwa kuwa Mwenyekiti wa klabu hiyo, atahitaji miezi mitatu tu kukamilisha ukarabati wa uwanja wa Kaunda ambao unamilikiwa na Yanga

Aidha Igangula anayechuana na Dk Mshindo Msolla, Dr Jonas Tiboroha na Elias Mwanjala kuwania uwenyekiti wa Yanga, amesema kutokana na uzoefu mkubwa aliyokuwa nao kwenye uongozi wa Yanga, ana lengo la kuifanyia timu hiyo mambo makubwa na kamwe hataweka mbele maslahi binafsi

“Tutakuwa na mpango wa muda mfupi ambao tutaukarabati uwanja wetu pale klabuni, huku tukiwa na mpango wa muda mrefu wa kujenga uwanja nje ya mji, hata ikiwezekana Kibaha, Pwani ambao utakuwa na hosteli, maduka na ofisi mbalimbali,” amesema Igangula

Igangula pia ameunga mkono mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji wa Yanga akiahidi kulikamilisha zoezi hilo haraka

“Nitasimamia mchakato wa mabadiliko na kuhakikisha unakamiliki punde tu nitakapoingia madarakani. Nitaajiri wataalamu wenye ujuzi wa masuala ya kampuni ili tuachane na utaratibu huu wa kuendesha klabu kwa mazoea”

Ahadi nyingine alizotoa Igangula ni kuanzisha bima ya afya itakayowalenga wanachama, saccos, vicoba na mfuko wa kufa na kuzikana, kama sehemu ya kuimarisha umoja, upendo na mshikamano baina ya wanachama na viongozi wa Yanga

Pia atahakikisha wachezaji na benchi la ufundi wanalipwa mishahara kwa wakati, kusimamia mikataba na mapato ili kudhibiti ufisadi

Uchaguzi wa Yanga utafanyika Jumapili, May 05 ukumbi wa bwalo la Polisi, Osterbay jijini Dar es salaam

Watatu kuikosa Tanzania Prisons leo

Leo Alhamisi jioni Yanga itakuwa dimba la Uhuru kuikabili Tanzania Prisons katika mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara

Yanga itamkosa mlinda lango Klaus Kindoki anayetumikia adhabu ya kadi tatu za njano

Pia beki wa kushoto Gadiel Michael alipata majeraha katika mchezo uliopita dhidi ya Azam Fc anatarajiwa kukosekana pamoja na mkongwe Kelvin Yondani ambaye leo anamaliza adhabu ya kukosa michezo mitatu

Yondani atarejea kikosini kwenye mchezo wa nusu fainali kombe la FA (ASFC) dhidi ya Lipuli Fc utakaopigwa mkoani Iringa, May 06 uwanja wa Samora