Mabadiliko makubwa ya kikosi yanakuja Yanga

Kocha Mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera amepania hasa kutengeneza kikosi imara ili msimu ujao kuwa na timu itakayotoa ushindani wa kweli kwenye ligi na kwa wapinzani wake Simba ambao kwa msimu wa pili sasa wanaonekana kukosa changamoto

Baada ya kuhakikishiwa ‘fungu la uhakika’ kwa ajili ya kufanya usajili, Zahera amepanga kutengeneza Yanga mpya mapema tu ili wakati anaondoka kwenda Congo kwa ajili ya michuano ya AFCON 2019, aache masuala ya usajili yawe yamemalizika

Mcongomani huyo ana mwezi mmoja tu wa kukamilisha michakato hiyo ambayo tayari imeshaanza kukamilishwa kwa usiri mkubwa

Zahera amepania kufanya mabadiliko makubwa kwenye baadhi ya maeneo ambayo mwenyewe aliyaanisha kuwa na mapungufu

Golikipa

Baada ya ‘kumtosa’ Beno Kakolanya aliyeingia kwenye mgogoro na uongozi, Yanga itasajili mlinda lango mwingine kuziba nafasi yake ambaye atasaidiana na Klaus Kindoki na Ramadhani Kabwili.

Hata hivyo Kabwili nae anawaniwa na timu kutoka Saudi Arabia

Mlindalango wa Bandari Fc Farouq Shikalo anatajwa kuwa kwenye mazungumzo na Yanga

Walinzi wa pembeni

Yanga huenda ikasajili walinzi wawili wa pembeni, mmoja wa kulia mwingine wa kushoto ili kuwaongezea nguvu waliopo

Kwa sasa Yanga inawategemea zaidi Gadiel Michael na Paulo Godfrey huku hatma ya Juma Abdul na Haji Mwinyi ikibaki mikononi mwa Zahera

Mikataba ya wakongwe hao katika kikosi cha Yanga inamalizika mwishoni mwa msimu

Mlinzi wa kati

Eneo la safu ya ulinzi wa kati linatarajiwa kuboreshwa kwa kuongeza mlinzi mwingine licha ya eneo hilo kuwa na walinzi watatu wa kutegemewa Kelvin Yondani, Andrew Vicent na Abdallah Shaibu ‘Ninja’

Mlinzi wa AS Vita Yanick Bangala ambaye yuko kwenye kikosi cha timu ya Taifa ya DR Congo anatajwa kuwaniwa ili kuongeza nguvu kwenye safu hiyo

Kiungo Mkabaji

Papi Tshishimbi alisajiliwa na Yanga kucheza nafasi ya kiungo mkabaji.

Hata hivyo alipokuja Zahera alimbadilishia majukumu kwa kumchezesha namba 10 au 8 nafasi ambazo amekuwa akifanya vizuri

Feisal Salum ‘Fei Toto’ amekuwa akitumika nafasi ya kiungo mkabaji lakini Zahera alisema analazimika kumtumia kinda huyo kwa kuwa ndiye anayemudu zaidi nafasi hiyo kuliko viungo wengine

Lakini Fei Toto alipaswa kucheza namba nane, na ndio nafasi ambayo kocha wa timu ya Taifa Emmanuel Amunike amekuwa akimtumia kwenye kikosi cha Stars

Yanga huenda ikasajili kiungo mkabaji ‘wa asili’ ambaye pia atakuwa na uwezo wa kucheza nafasi ya ulinzi wa kati

Washambuliaji wa pembeni

Zahera ni muumini wa soka la kushambulia kwa kasi kupitia pembeni na mara kwa mara amelalamika kuwa Yanga haina wachezaji wa nafasi hiyo wanaoendana na mfumo wake na hivyo ndio sababu inayomfanya afanye mabadiliko ya mara kwa mara pembeni

Ni Mrisho Ngasa pekee ambaye kwa sasa amejihakikishia namba kwenye kikosi cha Zahera miongoni mwa washambuliaji wanaotokea pembeni

Yanga huenda ikaongeza viungo washambuliaji wawili wa pembeni kwa kila upande

Safu ya ushambuliaji

Yanga ina washambuliaji wa asili wawili tu, Amissi Tambwe na Heritier Makambo.

Wakati hatma ya Tambwe ambaye mkataba wake unamalizika mwishoni mwa msimu ikibaki mikononi mwa Zahera, hakuna shaka, safu ya ushambuliaji itaongezewa nguvu

Miongoni mwa washambuliaji wanaotajwa kuwaniwa na Yanga ni Jackues Tuyisenge ambaye mkataba wake na Gor Mahia uko ukiongoni huku ‘mtukutu’ Obrey Chirwa akitajwa kuwa tayari kurejea Yanga baada ya kugoma kuongeza mkataba na Azam Fc. Makataba wake wa miezi sita unamalizika mwishoni mwa msimu

Juzi Zahera alinukuliwa na chombo kimoja cha habari akisema kikosi chake cha msimu ujao kitakuwa na mabadiliko makubwa sana, wachezaji wa zamani ambao wataendelea kubaki Yanga hawatazidi 10

HAJI MANARA vs ZAHERA

MICHEZO || Afisa Habari wa klabu ya Simba Sc Haji Manara alitaka shirikisho la soka nchini Tanzania TFF kumchukulia hatua kocha Mkuu wa klabu ya Yanga Sc Mwinyi Zahera kwa makosa ya kuituhumu Simba Sc na TFF kuwa wanaihujumu klabu yake ya Yanga Sc kwa kuiibia point zao la Ligi kuu Tanzania bara bila kutaja kuwa hizo point wanaiba vipi.

Zahera akerwa na waamuzi ligi kuu

Kocha Mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera amesema kumekuwa na makosa mengi yanafanywa na waamuzi hasa kuionea Yanga lakini anasikitishwa kuona wanaondesha mpira nchini hawachukui hatua yoyote

Zahera aliyazungumza hayo jana baada ya mchezo kati ya Mtibwa Sugar dhidi ya Yanga, mchezo ambao wenyeji waliondoka na ushindi wa bao 1-0

Zahera amesema kwa mfumo huu wa kuzibeba dhahiri baadhi ya timu, ana mashaka na hatma ya mpira wa Tanzania kuwa utaendelea kubaki chini

Marefa wa Tanzania watoswa AFCON 2019

Shirikisho la Soka Afrika (CAF) limetoa orodha ya marefa 27 na marefa wasaidizi 29 kwa ajili ya Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) mwaka huu nchini Misri, lakini hakuna Mtanzania hata mmoja.

Waamuzi hao wameteuliwa kushiriki kozi maalum kuanzia Aprili 28 hadi Mei 5 mwaka huu mjini Rabat, Morocco kunolewa kwa ajili ya Fainali za Misri mwezi Juni.

Marefa hao wanatoka nchi 33 na wataingia kwenye kambi maalum ya mafunzo itakayosaidia uteuzi wa orodha ya mwisho ya marefa watakaochezesha fainali za mwaka huu zitakazoanza Juni 21 hadi Julai 19 katika miji ya Alexandria, Cairo, Ismailia na Suez

Kabwili kutimkia Arabuni

Mlinda lango wa Yanga Ramadhani Kabwili huenda akatimkia Saudi Arabia mwishoni mwa msimu baada ya timu ya Aladalah Fc inayoshiriki ligi kuu nchini humo kumuhitaji

Kabwili aliyejiunga na Yanga mwaka juzi baada ya kufanya vizuri kwenye michuano ya AFCON U17 iliyofanyika Gabon, mkataba wake na Yanga uko ukingoni na atakuwa huru ifikapo mwezi Juni

Kabwili amepata nafasi ya kucheza zaidi msimu huu baada ya aliyekuwa mlinda lango namba moja Beno Kakolanya kuingia kwenye mgogoro na kocha Mwinyi Zahera

Kwa sasa hapati nafasi mara kwa mara baada ya mlinda lango aliyeimarisha kiwango chake Klaus Kindoki kumpiku

Kocha Mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera amepania kukijenga upya kikosi cha Yanga kwa ajili ya msimu ujao na inaelezwa amewaruhusu wachezaji wote wanaotaka kuondoka, waondoke

Yanga huenda ikamsajili mlinda lango wa Bandari Fc, Farouk Shikalo ambaye usajili wake ulipaswa kukamilishwa mwezi Disemba wakati wa dirisha dogo la usajili kabla ya aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya usajili ya Yanga Hussein Nyika kushindwa kwenye dakika za majeruhi

Shikalo ni miongoni mwa wachezaji wanne ambao Zahera alisikitika kuwakosa katika usajili huo

Zahera azipigia hesabu Azam Fc, Lipuli Fc

Kocha Mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera amesema licha ya changamoto za waamuzi wanazokabiliana nazo kwenye ligi, hawatakata tamaa na watafanya maandalizi ya kutosha kuelekea mchezo unaofuata dhidi ya Azam Fc utakaopigwa uwanja wa Taifa April 29 2019

Yanga imesalia na michezo sita kumaliza msimu huku imchezo mmoja dhidi ya Biashara United ukitarajiwa kupigwa nje ya Dar

Yanga itarejea jijini Dar es salaam kutumia uwanja wa Taifa baada ya kumalizika fainali za AFCON U17 April 28 2019

Zahera amesema watahakikisha wanashinda michezo yote iliyobaki pamoja na kuweka msisitizo zaidi kwenye michuano ya kombe la FA (ASFC) wakitarajia kucheza na Lipuli Fc mwanzoni mwa mwezi wa tano katika mchezo wa nusu fainali

“Unajua mimi nimezunguka nchi nyingi sana Afrika lakini sijawahi kuona maamuzi ya hovyo kama ya waamuzi wa Ligi ya Tanzania, Hakuna haki na kungekuwa na haki nina uhakika sasaivi tungekuwa tushajihakikishia ubingwa”

“Kwa sasa tumesahau yote, tunajipanga kuelekea michezo inayofuata ukiwemo wa Azam Fc ili kuhakikisha tunashinda mechi zote zilizosalia huku tukihakikisha tunatwaa ubingwa wa Kombe la ASFC ili kujihakikishia nafasi ya kushiriki michuano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika mwakani”

Simba au Yanga kuchuana na Sevilla May 23

Wadhamini wa vilabu vya Simba na Yanga kampuni ya SportPesa, imetangaza kuileta nchini Sevilla Fc inayoshiriki ligi kuu ya Hispania, La Liga

Mkurugenzi wa Utawala na Utekelezaji wa kampuni ya SportPesa Abbas Tarimba amesema Sevilla itakuja nchini May 23 kuchuana na kati ya Simba au Yanga kwenye mchezo utakaopigwa uwanja wa Taifa

SportPesa pia inadhamini ligi kuu ya Hispania, La Liga

Zahera kukamilisha usajili kabla ya ligi kumalizika

Kocha Mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera tayari ameanza michakato ya kuwania sahihi za wachezaji anaowataka kuitumikia Yanga msimu ujao

Zahera ambaye aliasisi zoezi la uchangiaji linaloendelea sasa, ametaka kukamilisha michakato ya usajili kabla hajatimkia kwao DR Congo anakokabiliwa na majukumu ya timu ya Taifa kuelekea fainali za AFCON 2019 zitakazofanyika mwezi Juni nchini Misri

Zahera ataondoka mwanzoni mwa mwezi wa sita hivyo ametaka masuala yote ya usajili yakamilishwe mapema

Yanga inaendelea na mchakato wa kukusanya michango ya wadau wake kupitia Kamati Maalum ya uhamasishaji ambayo imemuhakikishia kocha huyo kuwa atapatiwa kiasi cha fedha alichohitaji ili kukamilisha michakato yote ya usajili

Wakati wa uzinduzi wa zoezi la kuichangia Yanga mkoani Dodoma mwanzoni mwa mwezi huu, Zahera alibainisha kuwa ana orodha ya wachezaji nane ambao wako tayari kutua Yanga

Mwenyekiti wa Kamati ya Uhamasishaji Mh Athony Mavunde amewataka, Wapenzi, mashabiki na wanachama wa Yanga waendelee kuwasilisha michango yao ili kukamilisha michakato yote kwa wakati

Kadi maalum za kuichangia Yanga ambazo zina thamani ya Tsh Milioni moja kwa kila kadi zinaendelea kutolewa, ambapo michango yote imetakiwa kuwasilishwa kabla ya April 25 2019