Kadi za njano zamuumiza Fei Toto

Kiungo wa Yanga Feisal Salum ‘Fei Toto’ ni miongoni mwa wachezaji wanaoongoza kwa kupewa kadi za njano msimu huu

Fei Toto tayari amekosa michezo mitatu ya ligi inayotokana na adhabu za kadi za njano

Kiungo huyo aliyesajiliwa na Yanga akitokea JKU ya Zanzibar, hafurahii kadi hizo kwani zinamharibia jina na kumpa sifa mbaya

Fei Toto amesema anachokifanya uwanjani ni kutimiza wajibu na maelekezo anayopewa na Mwalimu.

Anaamini baadhi ya kadi anastahili lakini yapo matukio ambao anadhani hatendewi haki na waamuzi

Aidha kiungo huyo amesema amekuwa akikamiwa na wachezaji wa timu pinzani hali inayomfanya acheze kwa presha kubwa

“Baadhi ya mechi huwa nakamiwa, na kunifanya nicheze kwa presha kubwa. Siwezi kusema uwezo wangu ndio chanzo cha kukamiwa kwani naamini kila timu inaingia uwanjani ikiwa na lengo la kupata alama tatu,” amesema

Zahera aenda Congo, kuiwahi Mbeya City

Kocha Mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera ameondoka jana kwenda DR Congo ambako inaelezwa amekwenda kushughulikia masuala binafsi

Zahera anatarajiwa kurudi May 19 siku tatu kabla ya mchezo wa raundi ya 37 ligi kuu ya Tanzania Bara dhidi ya Mbeya City

Mcongomani huyo amemuachia majukumu kocha Msaidizi Noel Mwandila

Yanga kuunda Kamati ya Usajili

Uongozi wa klabu ya Yanga uko katika mchakato wa kuunda Kamati ya usajili ambayo itashirikiana na Kocha Mwinyi Zahera kusimamia usajili wa timu hiyo

Akizungumza na waandishi wa habari leo katika Mkutano uliofanyika Makao Makuu ya Yanga jijini Dar es salaam, Mwenyekiti wa timu hiyo Dk Mshindo Msolla amesema tayari uteuzi umeshafanyika kwa sasa wanafanya majadiliano na wajumbe walioteuliwa kabla ya kuwaweka hadharani

“Wajumbe wa Kamati hiyo tumeshawateua lakini hatuwezi kuwatangaza kabla nao hawajaridhia,” amesema Dk Msolla

“Wiki ijayo tutakuwa na kikao na benchi la Ufundi, pengine katika kikao hicho tutaitangaza Kamati”

“Msimu huu tumedhamiria kufanya usajili makini wenye tija”

Aidha Dk Msolla amesema hata hivyo jukumu la kutafuta wachezaji litabaki kwa kocha Zahera na benchi lake la ufundi, Kamati hiyo itakuwa na jukumu la kumsaidia kukamilisha michakato ya usajili baada ya makubaliano kufikiwa

Dk Msolla amesema kuanzia msimu ujao watawatumia wachezaji waliocheza Yanga zamani kutafuta wachezaji

“Msimu ujao kazi kubwa itafanywa na wachezaji wetu wa zamani kwani tutawapa jukumu la kutembea mikoani kutafuta wachezaji wenye vipaji”

Yanga yatenga Bilioni Mbili kwa ajili ya usajili

Uongozi wa Yanga umetenga kati ya Tsh Bilioni 1.5 hadi Bilioni mbili kwa ajili ya usajili wa msimu ujao

Katika Mkutano na Waandishi wa Habari uliofanyika Makao Makuu ya Yanga jijini Dar es salaam leo, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Hamasa Lucas Mashauri amesema walikutana na kocha Mwinyi Zahera ambapo aliwapa mchanganuo wa mahitaji yake kwa ajili ya usajili

“Bajeti ya usajili mara nyingi inatolewa baada ya kukamisha zoezi la usajili”

“Lakini kwa sasa tunakuwa na makisio ya Bajeti tunayohitaji ambapo Kamati yetu ilipewa kazi ya kutafuta kati Bilioni 1.5 na Bilioni mbili,” amesema

“lengo letu kubwa ni kuwa na Yanga imara msimu ujao. Kazi tumemuachia kocha Mwinyi Zahera ili atuambie wachezaji anaowahitaji”

“Bajeti halisi itafahamika baada ya kocha kujadiliana na wachezaji anaotaka waje”

“Lakini tumemuhakikishia, hakuna mchezaji ambaye atamuhitaji tutashindwa kumsajili. Awe Tanzania, nje ya Tanzania hata Ulaya akipatikana mchezaji tutamsajili. Yanga imeshawahi kusajili wachezaji kutoka Ulaya”

“Kamati yetu inaendelea na zoezi la kutafuta fedha ili tuweze kutimiza lengo la kusajili timu bora kadiri kocha atavyopendekeza”

Katika hatua nyingine, Mashauri amewataka Wanayanga waendelee kuichangia timu yao waepuke upotoshaji unaosambazwa kwenye mitandao ya kijamii

“Tunawataka wapenzi, wanachama na mashabiki wetu waendelee kuichangia timu wasipotoshwe na taarifa zinazosambazwa kwenye mitandao”

“Taarifa nyingi zinazosambazwa kuwa tumepokea Bilioni mbili hazina ukweli wowote. Wanaoanzisha taarifa hizo wana lengo la kupunguza kasi ya kuichangia timu yetu”

“Yanga ni timu ya Wananchi na safari hii tumeamua kuisimamia sisi wenyewe. Na kama alivyosema Mwenyekiti, zoezi hili la uchangiaji litandelea kwa kuwa ni wajibu kwa kila Mwanchama wa Yanga kuichangia timu kila mwezi Tsh 1000/- ambayo ni ada ya uanachama”

TETESI ZA USAJILI YANGA: Kifaa kipya Yanga hiki hapa, ni hatari tupu, kutua nchini mwezi ujao

Kwa mujibu wa mtandao wa michezo wa ‘Kawowo Sports’ kutoka nchini Uganda umeripoti kuwa mshambauliaji wa zamani wa klabu ya Onduparaka FC, Agau Rashid ambaye kwa sasa anaichezea timu ya Maroons FC anatarajiwa kuwasili Tanzania mwezi Juni kwa ajili ya majaribio katika miamba ya soka ya ligi kuu Young Africans SC.
Rashid ni mzuri wa kumiliki mipira na mfumaniaji mzuri wa mabao

Kwa mujibu wa wakala wa mchezaji huyo, amesema kuwa Agau amepata mualiko kwaajili ya kwenda kufanya majaribio kufuatia kufanya vizuri zaidi msimu huu.
Nyota huyo wazamani wa Onduparaka, amejiunga na Maroons msimu wa mwaka 2018/19 akiwa kama mchezaji huru kwa mkataba wa miaka mitatu hata hivyo kama atajiunga na Yanga atakuwa amewatumikia waajiri wake hao mwaka mmoja pekee.

Ndani ya msimu huu mmoja, Agau Rashid amefanikiwa kufunga jumla ya mabao saba na kuwaacha mbali baadhi ya wachezaji wenzake kama Pius Obuya na Seif Batte wenye mabao manne kila mmoja ikiwa pamoja na Isaac Otto, Bronson Nsubuga waliyosajiliwa msimu huu mwezi Januari wakiwa na mabao matatu.

Klabu ya Maroons imetoa baraka zote kwa, Agau endapo atafanikiwa kufuzu majaribio yake ndani ya Yanga, hata hivyo kama atafanikuwa atajiunga na baadhi ya Waganda wenzake kama Emmanuel Arnold Okwi na Murushid Jjuuko wanaotumikia klabu ya Simba.

Zahera ataja sababu ya Ngasa kukosekana mchezo dhidi ya Ruvu Shooting

Kocha Mkuu wa Yanga Mwinyi Zahera amesema winga Mrisho Ngasa hakuweza kucheza jana mchezo dhidi ya Ruvu Shooting baada ya kuugua ghafla

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya mchezo, Zahera alisema Daktari wa timu Dk Bavu alishauri mchezaji huyo asitumike kwenye mchezo huo hivyo kuamua kumtumia Paulo Godfrey ‘Boxer’ wingi ya kulia

“Ngasa alipata matatizo muda mfupi baada ya kuwa tumepata kifungua kinywa. Alianza kutapika mfululizo na baada ya kupatiwa huduma na Daktari wa timu Dk Bavu, alishauri asicheze,” alisema Zahera

Akizungumzia mchezo huo ambao Yanga iliibuka na ushindi wa bao 1-0, Zahera aliwapongeza wachezaji wake kwa ushindi huo huku akifichua hawakuwa wamefanya mazoezi tangu walipocheza na Biashara United May 10

“Tulipata changamoto ya usafiri kutoka Mwanza hali iliyopelekea tuchelewe kurudi jijini Dar es salaam kujiandaa na mchezo. Hata baada ya kurudi tulilazimika kuwapa wachezaji mapumziko kwani walikuwa wamechoka”

“Nilifahamu mchezo wa leo (jana) hautakuwa mwepesi kwetu, lakini nimefurahi tumeweza kutumia moja ya nafasi tulizotengeneza ingawa tulikuwa na uwezo wa kufunga mabao zaidi kwenye kipindi cha kwanza”

TFF yafafanua kutoikabidhi Simba ubingwa mchezo dhidi ya Sevilla

Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), limeamua kumuondoa wasiwasi kocha wa Yanga, Mwinyi Zahera ambaye alikerwa na maneno ya msemaji wa Simba Haji Manara kwamba ubingwa watakabidhiwi wakati wa mechi yao na Sevilla inayoshiriki Ligi Kuu nchini Hispania (La Liga).

Kupitia msemaji wa TFF, Clifford Marion Ndimbo aliliweka sawa jambo hilo kwamba hakuna kanuni ya shirikisho inayoruhusu bingwa akabidhiwa kombe nje na mechi ya Ligi Kuu Bara.

“TFF ina kanuni zake hata Simba wakiandika barua kama alivyosema msemaji wao Manara kwamba endapo wangeshinda mechi zao wakabidhiwe taji la ubingwa kwenye mechi yao na Sevilla hakuna kitu kama hicho na hakitafanyika.

“Kama Zahera ana wasiwasi na hilo basi ajue kabisa kwamba TFF ina kanuni zake hata wakiandika barua hiyo, majibu yao ni rahisi kuwa kanuni haziruhusu mambo hayo”anasema.

Kuna video inayomuonyesha Zahera kwamba Simba watakabidhiwa ubingwa wakati sio mabingwa baada ya kusikia kauli ya msemaji wa Simba, Manara kuwa wataiomba TFF wawakabidhi kombe wakati wa mchezo wao na Sevilla.

Mwanaspoti