Waziri Mkuu mgeni rasmi mchezo wa Stars vs Uganda

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh Kassim Majaliwa keshokutwa Jumapili, March 24 2019 atawaongoza Watanzania kuiunga mkono timu ya Taifa ya Tanzania katika mchezo wa kusaka tiketi ya kutinga fainali za AFCON 2019 akiwa mgeni rasmi katika mcheoz huo dhidi ya Uganda

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam Mh Paul Makonda ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati Maalum ya Uhamasishaji, amesema Waziri Mkuu amekubali kuwa mgeni rasmi wa mchezo huo na hivyo kuwataka wakazi wa jiji la Dar es salaam na maeneo ya jirani kujitokeza kwa wingi kwenye uwanja wa Taifa kuungana na Waziri Mkuu katika kuipa sapoti Stars inayohitaji matokeo ya ushindi dhidi ya Uganda

Kikosi cha Stars kimeendelea kujifua katika dimba la Taifa kujiandaa na mchezo huo utakaopigwa saa kumi na mbili jioni

Stars imedhamiria kuvunja rekodi ya miaka 39 ya kukosa nafasi ya kushiriki fainali za michuano ya AFCON. Inaweza kufikia malengo hayo kama itaifunga Uganda huku ikiomba Lesotho ambayo itakuwa ugenini ikichuana na Cape Verde itashindwa kupata ushindi

Uganda tayari imefuzu ikiongoza kundi L ikiwa na alama 13, Lesotho inafuatia nafasi ya pili ikiwa na alama tano sawa na Stars lakini Lesotho imeipiku Stars kutokana na faida ya kupata alama nne katika michezo miwili ambayo timu hizo zilikutana

Cape Verde inashika mkia ikiwa na alama nne lakini pia inaweza kufuzu kama Stars itashindwa kupata ushindi dhidi ya Uganda huku yenyewe ikiichapa Lesotho

Ngasa ashikiria rekodi ya michezo, mabao Stars

Wakati Watanzania wakiusubiri kwa hamu mchezo wa Stars dhidi ya Uganda utakaopigwa keshokutwa Jumapili katika uwanja wa Taifa, winga wa Yanga Mrisho Ngasa ‘Uncle’ ni miongoni mwa wachezaji wenye historia ya kipekee katika kikosi cha timu ya Taifa ya Tanzania

Ngasa ameichezea Stars michezo 100 na kufanikiwa kufunga mabao 25. Bado rekodi yake hiyo ya michezo na mabao haijavunjwa

Ngasa mwenye umri wa miaka 29 anasema bado hajastaafu kuichezea timu ya Taifa na yuko tayari kuitumikia iwapo ataitwa siku zijazo

“Bado sijatangaza kustaafu kuichezea Stars, bado naamini ninayo nafasi ya kucheza na kuonyesha uwezo kama ilivyokuwa mwanzo,” amesema Ngasa

“Sijakata tamaa nitapambana kuhakikisha wakati wmingine napata nafasi ya kulitumikia taifa langu muda bado ninao na kipaji kipo kwanini nisiitwe hakuna raha kama kucheza katika timu ya taifa”

Ngasa amekuwa na msimu mzuri katika kikosi cha Yanga akijihakikishia namba kwenye kikosi cha kwanza cha kocha Mwinyi Zahera

Ngasa ameifungia Yanga mabao manne katika ligi kuu ya Tanzania Bara

Samatta aipongeza Simba, aiombea ushindi dhidi ya TP Mazembe

Nahodha wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ Mbwana Samatta ameipongeza klabu ya Simba kwa kufanikiwa kutinga hatua ya robo fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika

Simba imepangwa kuchuana na TP Mazembe katika mchezo wa robo fainali

Samatta ambaye kwa sasa ni kinara wa upachikaji mabao ligi kuu ya Ubelgiji akiwa na klabu ya KRC Genk, amewahi kuzitumikia Simba na TP Mazembe

Samatta aliitumikia Simba kwa muda mfupi kabla ya mabingwa hao wa Tanzania Bara kumuuza TP Mazembe ambako aliweza kupata mafanikio zaidi

Akiwa na TP Mazembe, mwaka 2015 aliweza kuisaidia timu hiyo kutwaa taji la ligi ya mabingwa Afrika yeye akiibuka kuwa mfungaji bora akipachika mabao saba

Mafanikio hayo yalimpa tuzo ya Mwanasoka bora wa Afrika kwa wachezaji wanaocheza ndani

Samatta amesema kwa hatua waliyofikia Simba, wanaweza kusonga mbele zaidi kwani wanaouwezo sawa na timu nyingine wanazoshindana nazo

Licha ya kucheza TP Mazembe kwa muda mrefu, Samatta amesema angependa kuona Simba inapata ushindi katika mchezo baina ya timu hizo ili iweze kutinga nusu fainali

“Simba sio wabaya, ukiangalia wote walioingia nao katika hatua ya robo fainali, kinachowatofautisha ni uzoefu wa kucheza mashindano ya Afrika,” amesema Samatta

“Kinachotakiwa ni maandalizi mazuri na nina imani wanao uwezo wa kufika mbali kwa sababu hata hapa walipofikia ni jitihada walizofanya katika maandalizi”

“Kama Mtanzania ningependa kuona Simba inafika mbali zaidi katika michuano hii”

Aussems apewa mbinu ya kuivusha Simba dhidi ya TP Mazembe

Droo ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika imepangwa juzi usiku, huku Simba wakirudishwa DR Congo kuvaana na TP Mazembe.

Simba wametinga hatua hiyo ya robo fainali baada ya kumaliza nafasi ya pili katika msimamo wa Kundi D, lililoongozwa na Al Ahly, wakiifunga AS Vita ya Congo katika mchezo wa mwisho.

Mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Simba, wataanza kibarua hicho dhidi ya wafalme hao mara tano wa Ligi ya Mabingwa Afrika, TP Mazembe kwa kucheza mchezo wa kwanza Aprili 6, mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.

AS Vita, iliyochapwa na Wekundu hao wa Msimbazi mabao 2-1 mwishoni mwa wiki iliyopita, kama nawaona watakavyowahadithia Mazembe kilichowakuta ndani ya uwanja huo wa Taifa.

Mara ya mwisho Wekundu wa Msimbazi kukutana na Mazembe ilikuwa mwaka 2011, baada ya hapo hawajakutana tena, kutokana na timu hiyo kukosa nafasi ya kushiriki michuano hiyo kwa kushindwa kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara kwa misimu mitano.

Simba ina kila sababu ya kuutumia vyema uwanja huo wa nyumbani kama ilivyofanya kwenye hatua ya makundi ya kuhakikisha hakuna kichwa kinachotoka salama bila kunyolewa.

Basi Simba ifanye hivyo hivyo kwa Mazembe kuhakikisha haitoki na inakufa kwa kipigo cha mabao zaidi ya matatu.

Pamoja na Simba kufungwa mechi zote tatu za ugenini katika hatu ya makundi, lakini hawajafungwa nyumbani wala kutoka sare.

Walianza kuichapa JS Saoura mabao 3-0 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, kisha wakafungwa 5-0 na AS Vita nchini DR Congo na kuchapwa tena kipigo kama hicho cha 5-0 na Al Ahly ya Misri.

Katika mchezo wa marudiano dhidi ya Al Ahly, Simba walishinda 1-0 kabla ya kupoteza 2-0 dhidi ya JS Saoura nchini Algeria na kuichapa AS Vita 2-1 Uwanja wa Taifa.

Kocha Patrick Aussems anapaswa kukumbuka kile kilichomkuta DR Congo na Misri katika mechi za makundi za ugenini.

Simba ilikwenda kucheza mechi za ugenini kama ipo nyumbani, hali iliyosababisha kuruhusu idadi kubwa ya mabao, lakini sasa Aussems anapaswa kujua hatua hii ni ngumu kidogo, maana ukifungwa mabao mengi ugenini ujue umetoka, hivyo Simba inatakiwa ishinde nyumbani kisha iende kupaki basi ugenini.

Aussems asirudie makosa ya hatua ya makundi katika kipindi hiki, bali aje na mbinu nyingine za kujilinda.

Simba haitakuwa ya kwanza kupaki basi, kwani timu kubwa hata Ulaya kama Chelsea na Manchester United ambazo zilikuwa zikinolewa na kocha Jose Mourinho zilikuwa zikifanya hivyo.

Sina wasiwasi na Simba kutumia vyema uwanja wa nyumbani, zaidi iongeze mbinu na maarifa kwa ajili ya mechi za ugenini.

Katika hatua ya makundi, Aussems alinukuliwa na vyombo vya habari kuwa atashambulia mwanzo mwisho ugenini kama anavyofanya akiwa nyumbani.

Lakini lazima akumbuke kuwa nyumbani ni tofauti na ugenini na kila mtu ana mbinu za kutumia vyema uwanja wake wa nyumbani.

Aussems lazima ajue, Wanasimba sasa hivi hawahitaji mbwembwe sana, wanahitaji ushindi muhimu na kutimiza ndoto zao za kucheza fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Simba inakutana na Mazembe ya sasa ambayo si ya kutisha sana, tofauti na ile ya zamani, ingawa bado wapo wachezaji kama Reinford Kalaba, Tresor Mputu, lakini hawana makali kama yale ya miaka ya nyuma.

Lakini ni muhimu kwa benchi hilo la ufundi kujua kwamba Mazembe haijapoteza hata mechi moja ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwenye uwanja wao wa nyumbani kati ya michezo tisa, wakishinda saba na kutoa sare miwili.

Wakali hao wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo wamefunga mabao 24 na kufungwa matatu tu katika michezo hiyo waliyoshuka ndani ya Uwanja wa TP Mazembe.

Katika hatua ya makundi msimu huu, timu hiyo haijaruhusu kufungwa bao lolote kwenye uwanja wao wa nyumbani, walifanikiwa kushinda mabao 2-0 dhidi ya CS Costantine, walishusha kipigo cha 8-0 kwa Club Africain na 2-0 dhidi ya Ismaily.

Makala hii imeandikwa na MWANI NYANGASSA kwa hisani ya Bingwa

DORTMUND: na Callum Hudson Odo

Klabu ya Borussia Dortmund inajipanga kuanza mazungumzo na klabu Chelsea ili kuona uwezekano wa kumpata mshambuliaji wake Callum Hudson Odoi ili kuwa mbadala wa Jadon Sancho endapo atatimkia Man United.
.

Licha ya kusisitiza kuwa hawatamuuza nyota huyo BVB wanahofia huenda wakalazimika kumpiga bei ifikapo mwishoni mwa msimu huu ikiwa kama Sancho atahitaji kuondoka.