Tutatetea ubingwa wetu ili tushiriki tena mwakani – Tshabalala

Nahodha Msaidizi wa kikosi cha Simba Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ amesema hatua ya robo fainali waliyofikia kwenye michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika imewapa somo na msimu ujao wakipata nafasi anaamini watafanya vizuri zaidi

Aidha Hussein amesema hatua hiyo imewapa nguvu ya kupambana kwenye ligi ili kuhakikisha wanatetea ubingwa wapate nafasi ya kushiriki michuano hiyo mwakani

“Tulianza kwa Kuandika Kitabu cha Historia Mpya ya Soka Letu baada ya Miaka Mingi Kupita Na Tulitegemea Kuendelea Kukiandika Kitabu Hicho Pale LUBUMBASHI Kabla ya Kukifunga Lakini Haikuwa Bahati,” Tshabalala ameandika kwenye ukurasa wa mtandao wa Instagram

“Uzuri na Utamu wa Mashindano Haya ya CAF CHAMPIONS LEAGUEUnatufanya Kama TEAM Na Mimi binafsi Kupambana Kuhakikisha Mwakani Tunarudi Tena INSHAALLAH”

Simba tayari imerejea nchini kuanza ‘mchakamchaka’ wa kula viporo katika kampeni ya kubakisha ubingwa Msimbazi

FT: Simba 1-4 TP Mazembe

Mchezo wa pili wa robo fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika kati ya TP Mazembe dhidi ya Simba umemalizika kwa wenyeji kusonga mbele hatua ya nusu fainali baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 4-1

Licha ya kutangulia kufunga bao la kuongoza kwenye dakika ya pili kupitia kwa Emmanuel Okwi, Simba ilishindwa kulinda bao hilo huku mfumo wa kujihami zaidi uliotumiwa na kocha Patrick Aussems ukitajwa kuigharimu Simba katika kipindi cha kwanza na kujikuta ikiruhusu mabao mawili mpaka wakati wa mapumziko

TP Mazembe ilitawala zaidi mchezo kwenye kipindi cha pili kwa kutengeneza nafasi nyingi huku ikifanikiwa kutumia nafasi nyingine mbili kujihakikishia ushindi wa mabao 4-1

Licha ya kuondoshwa katika hatua ya robo fainali, mafanikio ya kufika hatua hiyo ni ya kujivunia kwa Simba

Aidha bila shaka Simba itaendeleza hapa ilipoishia kwa kuimarisha zaidi kikosi chake ili kuwa cha ushindani zaidi msimu ujao

Rais Congo kushuhudia mchezo wa TP Mazembe vs Simba

Klabu ya TP Mazembe iimemualika Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Felix Tshisekedi kushuhudia mchezo wa pili wa robo fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika dhidi ya Simba

Ikulu ya DR Congo imethibitisha kuwa Tshisekedi atakuwepo uwanjani kushuhudia mchezo huo unaopigwa leo saa kumi kamili jioni

Mchezo huo utapigwa katika uwanja wa Stade TP Mazembe

Ajib mbioni kurejea kikosini Yanga

Nahodha wa Yanga Ibrahim Ajib amekosekana dimbani kwa takribani wiki tatu akisumbuliwa na majeraha ya nyonga

Kinara huyo wa kutengeneza mabao ligi kuu huenda akarejea kikosini kwenye mchezo ujao dhidi ya Mtibwa Sugar utakaopigwa mkoani Morogoro April 17 2019

Kukosekana kwake katika michezo iliyopita kumeibua maswali mengi miongoni mwa mashabiki wa Yanga hasa baada ya kuibuka tetesi kuwa anataka kurudi katika timu yake ya zamani, Simba

Hata hivyo Msemaji wa Yanga Dismas Ten amesisitiza kuwa Ajib amekosa michezo iliyopita kutokana na kuwa majeruhi na si vinginevyo

Amesema atarejea kikosini baada ya kupona majeraha hayo