Mashabiki mapemaa uwanja wa Karume

Leo saa kumi kamili jioni mabingwa wa nchi Simba watashuka kwenye uwanja wa Karume kuchuana na Biashara United katika mchezo wa kiporo wa ligi kuu ya Tanzania

Simba ilipowasili mkoani Mara jana, shamrashamra za mashabiki zilikuwa kubwa hali hiyo imeendelea mpaka leo ambapo mashabiki walianza kuingia uwanjani tangu saa tatu asubuhi

Mpaka kufika saa 10 jioni huenda mashabiki ambao watachelewa wakalazimika kurudi nyumbani kuushuhudia mchezo huo runingani kwani mpaka sasa uwanja wa Karume unaelekea kujaa

Mashabiki wana shauku ya kuishuhudia Simba ambayo imetua mkoani Mara kwa mara ya kwanza baada ya kupita miaka 15

Simba yasaka alama tatu dhidi ya Biashara United leo

Kikosi cha mabingwa watetezi ligi kuu ya Tanzania Bara Simba kiko mkoani Mara ambapo leo kitashuka kwenye uwanja wa Karume kupepetana na wenyeji wao Biashara United

Baada ya ushindi dhidi ya Alliance na KMC, Simba imeingia Mara ikiwa na shauku yas kupata alama nyingine tatu ili kujisogeza zaidi kileleni mwa msimamo wa ligi

Biashara United imeweka hadharani viingilio vya mchezo huo ambapo VIP ni Tsh 20,000/- Mzunguuko Tsh 5,000/- huku watoto wakiwekewa kiingilio cha Tsh 3,000/-

Mchezo utapigwa kuanzia saa kumi kamili jioni

Kila la kheri mabingwa wa nchi…!

Simba yajifua Mara

Kikosi cha Simba leo jioni kimefanya mazoezi kwenye uwanja wa Karume wilayani Musoma kujiandaa na mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara dhidi ya Biashara United

Mchezo huo utapigwa kesho Jumamosi katika uwanja huo

Msafara wa Simba uliwasili mkoani Mara mapema leo na kupokewa na idadi kubwa ya mashabiki waliokuwa na shauku ya kuwaona mabingwa hao wa nchi

Simba yapata mapokezi makubwa Mara

Kikosi cha Simba kimewasili salama mkoani Mara tayari kwa mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara dhidi ya Biashara United

Mchezo huo utapigwa kesho Jumamosi, April 27 kwenye uwanja wa Karume

Idadi kubwa ya mashabiki wamejitokeza kwa wingi kuulaki msafara wa mabingwa hao watetezi wakati ukiingia Musoma

Waamuzi mchezo wa KMC vs Simba waondolewa

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limewaondoa waamuzi waliochezesha mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara kati ya KMC dhidi ya Simba uliopigwa jana uwanja wa CCM Kirumba


Kulingana na taarifa iliyotolewa na TFF, Waamuzi hao wanatuhumiwa kuchezesha mchezo huo chini ya kiwango
Katika mchezo huo Simba iliibuka na ushindi wa mabao 2-1

Mchezo wa Biashara United vs Simba utapigwa hapa

Simba kesho Jumamosi itandelea na ratiba yake ya ‘bandika-bandua’ kwa kuikabili Biashara United katika mchezo utakaopigwa dimba la Karume wilayani Musoma

Simba tayari imeondoka Mwanza na leo jioni inatarajiwa kujifua kwenye uwanja huo

Hii itakuwa mara ya kwanza kwa Simba kucheza mkoani Mara baada ya kupita miaka 15

Biashara United inanolewa na beki wa zamani wa Simba Amri Said

Manara awapasha Yanga, ‘kalipeni mishahara ya wachezaji wenu’

Afisa Habari wa Simba Haji Manara amewataka mashabiki wa Yanga watumie muda wao kuinusuru timu yao na ‘ukata’ uliowakumba kuliko kupoteza muda mwingi kuifuatilia Simba ambayo inafanikiwa mambo yake

Baada ya mchezo dhidi ya KMC jana, mashabiki wa Yanga walionekana kuisemea KMC kuwa imeonewa na waamuzi huku wachezaji wa timu yao wakigoma kufanya mazoezi wakidai mishahara

Tangu jana wachezaji wa Yanga hawafanyi mazoezi wakishinikiza walipwe madai yao ya mishahara ya miezi mitatu huku wengine wakiwa hawajalipwa fedha za usajili mpaka leo

“Badala ya kuhangaika jinsi ya kuwalipa mishahara wachezaji wenu mnahangaika na timu Bingwa inayowafunga kila siku. Kama nyie wananchi wachangieni hao wachezaji walipwe mishahara,” ameandika Manara kwenye ukurasa wake wa mtandao wa Instagram

Penati hazina mwenyewe, tuwavumilie wachezaji wanapokosa

Katika mchezo wa kwanza wa ligi ya mabingwa dhidi ya TP Mazembe, nahodha John Bocco alikosa mkwaju wa penati tukio ambalo lilimfanya ashushiwe lawama nyingi na mashabiki

Hata hivyo leo katika mchezo dhidi ya KMC, Bocco ameifungia Simba mkwaju muhimu wa penati ulioipandisha Simba hadi nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-1

Hata hivyo katika mchezo huo Meddie Kagere alikosa penati ya kwanza iliyotolewa na mwamuzi

Matukio haya yanadhihirisha kuwa hakuna sababu ya kuwalaumu wachezaji pale wanapokosa mikwaju ya penati kwani hakuna mchezaji mwenye uhakika wa kufunga penati kwa asilimia 100

Katika kikosi cha Simba Bocco ndiye mwenye rekodi nzuri ya kufunga mikwaju ya penati.

Kwenye ligi Bocco amefunga mikwaju yote mitano aliyopiga msimu huu